Tuesday, August 20, 2024

MHE. SANGU AWATAKA WATUMISHI WA TASAF KUWA WABUNIFU

 Na. Mwandishi wetu

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Deus Sangu ametoa rai kwa watumishi wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kuwa wabunifu ili fedha zinazopelekwa kwa wananchi zisiende kama msaada isipokuwa ziende kwa mantiki ya kuwainua na kuwatoa kwenye wimbi la umaskini.

Mhe. Sangu ametoa rai hiyo leo tarehe 19 Agosti, 2024 jijini Dar es salaam wakati alipofanya ziara ya kujifunza namna taasisi hiyo inavyofanya kazi na kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi.

Amesema, mpango wa kunusuru kaya maskini ni muhimu sana kwa wananchi, hivyo alielekeza menejimenti kuendelea kufikiri na kufungamanisha programu za kunusuru kaya maskini na programu nyingine ili kuwatoa walengwa kwenye umaskini.

Aidha, aliongeza kuwa Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anaendelea kutafuta fedha na kuzipeleka kwa walengwa wengi zaidi, hivyo jitihada za kunusuru kaya maskini zinatakiwa kuimarishwa zaidi na watendaji.

Aidha, Mhe. Sangu ameomba menejimenti na watumishi wa TASAF kumpa ushirikiano hasa anapotaka taarifa za mfuko ili kujibu hoja na kutoa ufafanuzi wa masuala mbalimbali ya TASAF kwa Waheshimiwa Wabunge.

“Mimi milango iko wazi wakati wote, iwapo mtapata changamoto yoyote inayohitaji mawazo au ushauri wangu, niko tayari kuwasaidia kwa kuwa ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu yangu” alisisitiza Mhe. Sangu.

Awali, Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF Bw. Shedrack Mziray alisema malipo ya ruzuku kwa walengwa hufanywa kwa kutoa fedha taslimu kwa kutumia kamati ya usimamizi wa shughuli za mipango kwa jamii chini ya usimamizi wa ngazi ya utekelezaji wa mpango (Halmashauri) na njia ya pili ni ya kieleketroni.

Bw. Mziray ameongeza kuwa njia zote ni muhimu kwa walengwa ingawa njia ya kieletroni ni muhimu zaidi kwa kuwa inarahisisha utoaji wa ruzuku kwa walengwa ingawa kuna changomoto mbalimbali zinazowakabili wanufaika.

Alibainisha kuwa mwaka 2023 TASAF ilifanya tathmini na kubaini kaya za walengwa 394,305 zimeimarika kiuchumi na kukidhi vigezo vya kuhitimu na hivyo hazitaendelea kupewa ruzuku kama ilivyokuwa hapo awali.

Mhe. Sangu amefanya ziara kwa lengo la kujifunza kuhusu majukumu ya Mfuko huo ambao upo chini ya Ofisi anayoiongoza.









No comments:

Post a Comment