Thursday, November 30, 2023

OFISI YA RAIS-UTUMISHI YATEMBELEWA NA VIONGOZI WA SERIKALI KATIKA MAADHIMISHO YA SIKU YA UKIMWI


Mkurugenzi Msaidizi Anuai za Jamii na Mratibu wa VVU, Ukimwi na Magonjwa Yasiyoambukiza, Ofisi ya Rais, UTUMISHI na Utawala Bora, Bi. Mwanaamani Mtoo (Wa pili kutoka kulia) akifafanua jambo kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Mhe. Jenista Mhagama (Aliyeshika pochi) na Viongozi wengine wa Wizara hiyo walipotembelea banda la maonesho la Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakati wa maonesho ya maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani yatakayofanyika Mjini Morogoro.

Mkurugenzi Msaidizi Anuai za Jamii na Mratibu wa VVU, UKIMWI na Magonjwa Yasiyoambukiza, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Mwanaamani Mtoo (Katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya watumishi wa ofisi hiyo wakati wa maonesho ya maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani yanayofanyika mjini Morogoro.


Baadhi ya viongozi, waratibu na waelimisha rika wa Wizara, Mikoa na Taasisi za Umma wakifuatilia jambo ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani Mjini Morogoro.

 




Tuesday, November 28, 2023

OFISI YA RAIS-UTUMISHI YAIBUKA NA USHINDI KATIKA MBIO ZA NYIKA KWENYE MAADHIMISHO YA SIKU YA UKIMWI

 Na. Veronica Mwafisi-Morogoro

28 Novemba 2023.  

Watumishi wawili wa Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora waibuka na ushindi katika mbio za Nyika zilizoandaliwa kwa lengo la kuhamasisha uchangiaji wa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli za VVU na Ukimwi hapa nchini.

Katika mbio hizo Bw. Kokolo Lusanda ambaye alishiriki mbio za kilometa 5 aliibuka mshindi wa pili na Bi. Juliana Ntukey aliibuka mshindi wa nne katika mbio za kilometa 10.

Bw. Kokolo amesema kuwa mashindano hayo ya mbio za nyika  yamemuongezea ari ya kuendelea kufanya mazoezi na kushiriki katika mashindano mengine yatakayoshirikisha watumishi wa umma kwa kuwa raha ya ushindi ni kuendelea kushiriki na kushinda katika mashindano mengine.

Naye Bi. Juliana alibainisha kuwa mbio za nyika zilikuwa na ushindani mkubwa lakini jitihada zake za kumalizia kama vile ndio anaanza mbio zimemfanya kuwapita wenzake na kupata nafasi hiyo ya nne kwa kishindo.

“Nimefarijika sana kuwa mshindi kwa nafasi ya nne sio haba na kwa mwaka ujao nitaongeza juhudi kubwa ili niweze kushika nafasi ya kwanza kwa kudra za Mwenyezi Mungu” alisema Bi Juliana.

Aidha, washindi hao wameishukuru Menejimemti ya Ofisi ya Rais-UTUMISHI kwa kutoa kibali kwa watumishi wake kushiriki kwenye Maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani ambapo wametumia fursa hiyo kushiriki katika mashindano hayo yaliyoandaliwa wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani, 2023 yanayofanyika Kitaifa Mkoani Morogoro na kuibuka  washindi.

Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, kupitia Idara ya Uendelezaji Sera ipo mkoani Morogoro kwenye Maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani yanayofanyika kitaifa mkoani humo ambapo sehemu ya watumishi wake wameshiriki katika mbio hizo za nyika na kuibuka washindi.

Mkurugenzi Msaidizi Anuai za Jamii na Mratibu wa VVU, Ukimwi na Magonjwa Yasiyoambukiza, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Mwanaamani Mtoo akimpongeza mtumishi wa ofisi hiyo Bw. Kokolo Lusanda aliyepata ushindi wa pili katika mbio za Km. 5 wakati wa maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani, 2023 yanayoendelea mkoani Morogoro.


Sehemu ya watumishi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, wakishiriki mbio za nyika zinazofanyika mkoani Morogoro. Wa kwanza kulia ni Mkurugenzi Msaidizi Anuai za Jamii na Mratibu wa VVU, Ukimwi na Magonjwa Yasiyoambukiza, Bi. Mwanaamani Mtoo.


Sehemu ya watumishi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, wakifurahia jambo mara baada ya kuhitimisha mbio za nyika ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani, 2023 yanayoendelea mkoani Morogoro.



Monday, November 27, 2023

MHE.SIMBACHAWENE ASEMA UTUMISHI WA UMMA NI KUJITOA KUHUDUMIA WATU

 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene ametoa rai kwa wahitimu kutambua kuwa kwenye utumishi wa umma sio sehemu ya kuvuna utajiri na kujilimbikizia mali bali ni sehemu ya kujitoa kwa ajili ya kutoa huduma bora kwa umma.

Mhe. Simbachawene ametoa rai hiyo wakati wa mahafali ya 38 ya Chuo cha Utumishi wa umma Tanzania yaliyofanyika katika Kampasi ya Chuo cha Utumishi wa Umma Mkoani Tabora.

“Naomba kila mmoja wenu awe na moyo wa kujitoa kwa maendeleo ya taifa na kutumia fursa mbalimbali zinazopatikana katika mazingira yenu na zile zinazotolewa na Serikali katika kujiletea maendeleo na kuhakikisha mnatatua changamoto zinazokabili jamii zinazowazunguka wakati mkidumisha amani, upendo na mshikamano” amesisitiza Mhe. Simbachawene.

Aidha, Mhe. Simbachawene ametumia fursa ya mahafali hayo kutoa wito kwa waajiri wote wa Taasisi za Umma nchini kukitumia Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania katika kuboresha utendaji kazi wa watumishi na Taasisi zao kupitia mafunzo mbalimbali yanayotolewa na Chuo hicho.

Mhe. Simbachawene amesema kuwa baadhi ya taasisi za umma zimekuwa zikisuasua katika kuwapatia waajiriwa wapya Mafunzo Elekezi ya Awali (Induction Training) jambo ambalo linasababisha watumishi hao kushindwa kutambua misingi ya Utumishi wa Umma, Sheria, Kanuni, Miongozo na Taratibu za utendaji kazi na uwajibikaji Serikalini.

Aidha, amewasisitiza Maafisa Masuuli wote katika taasisi za umma kutumia muda wao kufanya uchunguzi kwa makini ili kuona namna wajiriwa hao wapya wanavyopata shida katika utekelezaji wa majukumu yao kwa ufanisi na hivyo kukwamisha jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita ya kutoa huduma bora kwa wananchi.

“Napenda ifahamimike kuwa suala la kuwapatia watumishi wapya mafunzo sio hiari bali ni matakwa ya kisheria na hii ni kwa mujibu wa waraka wa Utumishi Na. 5 wa mwaka 2011. Kwa hiyo ninaelekeza watumishi wote wapya katika utumishi wa umma wapewe mafunzo mara tu wanaporipoti katika vituo vyao vya kazi” amesisitiza Mhe. Simbachawene.

Vilevile, Mhe. Simbachawene Mhe. Simbachawene ameipongeza Bodi, Menejimenti na watumishi wote wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kwa kazi nzuri wanayoifanya kwa kuwa matunda ya kazi yao njema yanaonekana wazi.  Vilevile amewahakikishia kuwa Serikali hii ya Awamu ya sita inayoongozwa na Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, inatambua juhudi wanazofanya na  hivyo, Wizara yake itaendelea kutoa ushirikiano ili kufanikisha malengo ya chuo.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene akihutubia wahitimu na wageni waalikwa wakati wa mahafali ya 38 ya Chuo cha Utumishi wa umma Tanzania yaliyofanyika katika Kampasi ya Chuo hicho Mkoani Tabora.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi mbalimbali wakati wa mahafali ya 38 ya Chuo cha Utumishi wa umma Tanzania yaliyofanyika katika Kampasi ya Chuo hicho Mkoani Tabora.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene akiteta jambo na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Chuo cha Utumishi wa umma Tanzania Dkt. Florens Turuka wakati wa mahafali ya 38 ya Chuo hicho yaliyofanyika katika Kampasi ya Tabora Mkoani Tabora.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Wahitimu wa Chuo cha Utumishi wa umma Tanzania wakati wa mahafali ya 38 yaliyofanyika katika Kampasi ya Chuo hicho Mkoani Tabora.



 

Sunday, November 26, 2023

WARATIBU NA WAELIMISHA RIKA WAPATIWA MAFUNZO YA KUTEKELEZA AFUA ZA KUDHIBITI VVU NA UKIMWI

 Na. Veronica Mwafisi-Morogoro

Tarehe 26 Novemba, 2023

Ofisi ya Rais-UTUMISHI kupitia Idara ya Uendelezaji Sera imetoa mafunzo kwa waratibu na waelimisha rika wa Wizara, Mikoa na Taasisi za umma kwa lengo la kuwajengea uwezo na stadi za utekelezaji wa afua kwa ajili ya kuwalinda watumishi wa umma dhidi ya VVU na Ukimwi.

Katika mafunzo hayo Mkurugenzi Msaidizi Anuai za Jamii na Mratibu wa VVU, Ukimwi na Magonjwa Yasiyoambukiza, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Mwanaamani Mtoo amesema Ofisi ya Rais-UTUMISHI inaungana na Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika jitihada za kutokomeza VVU na Ukimwi ili kuendelea kuwa na nguvukazi hususani katika utumishi wa umma yenye afya njema ili iweze kutoa huduma bora kwa wananchi.

Bi. Mtoo ameongeza kuwa mafunzo haya ni endelevu kwa kuwa ni sehemu ya mapambano dhidi ya VVU na Ukimwi ili kuwalinda watumishi wa umma na kuhakikisha taifa linaondokana na vifo vitokanavyo na Ukimwi ifikapo mwaka 2030.

“Tunatoa mafunzo haya kwa waratibu na waelimisha rika wa Wizara, Mikoa na Taasisi wakati wa maadhimisho ya Siku ya Ukimwi ili waende kutoa elimu ya kudhibiti VVU na Ukimwi mahali pa kazi katika Utumishi wa Umma” amefafanua Bi. Mwanaamani.

Naye, mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo ambaye ni Mratibu wa VVU na Ukimwi kutoka Hospital ya Rufaa ya Tumbi-Pwani, Dkt. Hapiness Ruta ameishukuru Ofisi ya Rais-UTUMISHI kwa kutoa mafunzo hayo ya VVU na Ukimwi na kuahidi kuyafanyia kazi ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa watumishi wa umma waliopo katika maeneo yao ya kazi.

Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, kupitia Idara ya Uendelezaji Sera ipo mkoani Morogoro kwenye Maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani yanayofanyika kitaifa mkoani humo kuanzia tarehe 24 Novemba hadi tarehe 02 Disemba, 2023. Kaulimbiu ya maadhimisho hayo ni Jamii iongoze kutokomeza Ukimwi.



Mkurugenzi Msaidizi Anuai za Jamii na Mratibu wa VVU, UKIMWI na Magonjwa Yasiyoambukiza, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Mwanaamani Mtoo akielezea madhumuni ya kikao kazi cha kuwajengea uwezo waratibu na waelimisha rika wa Wizara, Mikoa na Taasisi wakati wa maadhimisho ya Siku ya Ukimwi yanayofanyika Kitaifa mkoani Morogoro.

Afisa Ustawi wa Jamii Mwandamizi na Mratibu wa kitaifa wa kudhibiti VVU, UKIMWI na MSY, Ofisi ya Rais, UTUMISHI na Utawala Bora, Bi. Juliana Ntukey akiwasilisha mada kuhusu sababu za kuwepo kwa Afua za VVU, UKIMWI na MSY mahali pa kazi wakati wa maadhimisho ya Siku ya Ukimwi yanayofanyika Kitaifa mkoani Morogoro. 


Mkurugenzi Msaidizi Anuai za Jamii na Mratibu wa VVU, UKIMWI na Magonjwa Yasiyoambukiza, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Mwanaamani Mtoo akiwa katika picha ya pamoja na waelimisha rika wa Wizara, Mikoa na Taasisi mara baada ya kuhitimisha kikao kazi wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Ukimwi yanayofanyika Kitaifa mkoani Morogoro.



Friday, November 24, 2023

MHE.KIKWETE: eGA INAJUKUMU NYETI LA KUIHUDUMIA SERIKALI ILI KUTOA HUDUMA KIDIJITALI

 

Na. Lusungu Helela- Iringa 


Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora   Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) ina jukumu nyeti la kusanifu na kutengeneza mifumo ya TEHAMA ili iweze kutoa huduma kwa umma kwa haraka na ufanisi.

Mhe.Kikwete ametoa kauli hiyo leo wakati alipotembelea Ofisi za eGA-Kituo cha Iringa ili kukagua utendaji kazi wa Mamlaka katika kituo hicho ikiwa ni muendelezo wa ziara yake ya kikazi mkoani humo.

“Dunia inakwenda kasi na teknolojia ni kila kitu kwa sasa, hivyo ni muhimu kwa eGA kufanya utafiti, kubuni na  kutengeneza mifumo ya TEHAMA Serikalini kwa ajili ya kurahisisha utoaji wa huduma kwa umma” amesema Mhe. Kikwete.

Mhe. Kikwete ameongeza kuwa eGA imeweka juhudi kubwa katika kusimamia TEHAMA Serikalini na imetengeneza na inaendelea kutengeneza mifumo ya TEHAMA ambayo imewarahisishia wananchi kupata huduma kwa haraka, mahali popote na kwa gharama nafuu na kuchagiza utawala bora.

Aidha, Mhe. Kikwete ameridhishwa na utendaji kazi wa Mamlaka ya Serikali Mtandao katika ofisi zake zilizopo Iringa na amewataka watumishi wa Mamlaka kwa jumla kuendelea kubuni Mifumo ya TEHAMA inayotatua changamoto zilizopo nchini pamoja na kuwa wazalendo kwa maslahi ya Taifa.

Vile vile, amewasisitiza eGA kuhakikisha mifumo inayotengenezwa na iliyopo inakuwa na uwezo wa kuwasiliana ili kuleta ufanisi katika kuwahudumia wananchi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao, Eng. Benedict Ndomba amemshukuru Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete kwa kutenga muda wake kutembelea kituo hicho cha Iringa na kuahidi kutekeleza maagizo yote aliyotoa.




  Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora   Mhe. Ridhiwani Kikwete akizungumza na Watumishi wa   Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) wa Kituo cha Iringa ikiwa ni ziara yake ya kikazi mkoani humo  




 Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora   Mhe. Ridhiwani Kikwete akiangalia eneo ambalo    Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) inatarajia kujenga   Kituo chake Mkoani  Iringa.


3 Sehemu ya Watumshi Watumishi wa   Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) wa Kituo cha Iringa ikiwa ni zaira yake ya kikazi mkoani humo wakimsiliza  Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora   Mhe. Ridhiwani Kikwete 
 

 Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora   Mhe. Ridhiwani Kikwete akizungumza na Watumishi wa   Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) wa Kituo cha Iringa ikiwa ni zaira yake ya kikazi mkoani humo  


MHE.KIKWETE ASIKITISHWA NA WIMBI KUBWA LA WATUMISHI WANAOTAKA KUHAMA HALMASHAURI YA KILOLO


Na. Lusungu Helela- Kilolo

Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.Ridhiwani Kikwete amesikitishwa na wimbi kubwa la wafanyakazi hususan walimu  wanaotuma maombi ya kutaka kuhama katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo, Mkoani Iringa.


Mhe.Kikwete ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na Watumishi wa Halmashuuri ya Kilolo ikiwa ni muendelezo wa ziara yake ya  kikazi Mkoani humo ya  kuzungumza na kusikiliza kero za  watumishi na kuzitafutia ufumbuzi.

Amesema Watumishi walio wengi wanaotaka kuhama wamekuwa wakitaja sababu zinazofanana jambo ambalo lina walakini huku akisema kuna matatizo ya kiuongozi katika Halmashauri hiyo .

Ametaja moja ya sababu zinazopelekea  Watumishi hao kutaka kuhama ni pamoja na kupuuzwa na  kutokusikilizwa pindi watumshi hao  wanapokuwa na changamoto.

'" Kuna watumishi hapa hawajapandishwa vyeo kwa muda miaka tisa na wengine hapa licha ya kujiendeleza kielimu mishahara yao haijabadilika lakini ninyi Maafisa Utumishi wenye jukumu la kufuatilia UTUMISHI  na kuwapa majibu mpo tu, hili sio sawa hata kidogo" amesisitiza Mhe.Kikwete.


Amefafanua kuwa katika Halmashauri hiyo Maafisa Utumishi na Maafisa Tawala wamekuwa miungu watu  badala ya kuwa suluhisho la matatizo yanayowakabili watimishi wanaowasimamia.

Amesema licha ya watumishi wengi wanaotaka kuhama kutaja sababu inayofanana,  kuwa ni uwepo wa baridi kali na hivyo kusumbuliwa na "athma" jambo ambalo si kweli, ukweli ni kwamba hakuna mahusiano mazuri kati ya Watumishi na Uongozi wa Halmashauri hiyo.

Kufuatia hatua hiyo Mhe.Kikwete amemtaka  Mkurugenzi kufanyia kazi changamoto zinazowakabili watumishi hao ikiwemo kufanya vikao vya mara kwa mara na watumishi  kwa ajili ya kuwasikiliza pamoja na kuzingatia stahili zao ikiwepo posho za likizo.


Katika hatua nyingine Mhe.Kikwete amewatak Maafisa Utumishi na Maafisa Tawala kuwa kimbilio la watumishi badala ya kuwa vikwazo katika kufanyia kazi changamoto za watumishi.

" Kazi yenu Maafisa Utumishi na Maafisa Tawala ni kusikiliza, kupendekeza watumishi wenu katika kupandishwa vyeo lakini mlio wengi mmekuwa ni watu wenye roho mbaya na mnaopenda kuwakomoa wenzenu, acheni hizo " amesisitiza Mhe.Kikwete

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kilolo, Estomin Kyando ametumia nafasi hiyo kumshukuru Naibu Waziri Kikwete kwa kufika kwa ajili ya kuzungumza na watumishi anawaongoza huku  akiahidi kufanyia kazi maelekezo yote aliyoyatoa ili watumishi waweze kufurahi kufanya kazi katika Halmashauri hiyo.


 Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete akizungumza na Watumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Kilolo  mkoani Iringa ikiwa ni muendelezo wa ziara yake ya kikazi ya kuzungumza na  kusikiliza changamoto zinazowakabili watumishi hao.



Sehemu ya watumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Kilolo wakimsikiliza  Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete alipokuwa akizungumza nao ambapo ameahidi kushirikiana nao katika kutatu changamoto mbalimbali zinazowakabili



 Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete akifurahia jambo kbala ya kuanza kuzungumza na  na Watumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Kilolo  mkoani Iringa ikiwa ni muendelezo wa ziara yake ya kikazi ya kuzungumza na  kusikiliza changamoto zinazowakabili watumishi hao.
Mtumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Kilolo Mkoani Iringa, Felister Mnyawami akizungumza mbele ya Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete wakati alipotoa nafasi ya watumishi hao kuzungumza changamoto zao zinazowakabili ili aweze kuzitafutia ufumbuzi.


Wednesday, November 22, 2023

MHE. RIDHIWANI KIKWETE AFURAHISHWA NA MIRADI YA TASAF IRINGA


Na. Lusungu Helela- Iringa 

Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora  Mhe Ridhiwani Kikwete ameupongeza uongozi wa Mkoa wa Iringa kwa usimamizi mzuri katika utekelezaji wa miradi inayotekelezwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii -TASAF.

Amesema kupitia usimamizi mzuri wa utelekezaji wa miradi hiyo, TASAF imeweza kutatua changamoto mbalimbali za kiuchumi na kijamii katika kaya za walengwa pamoja na wananchi katika maeneo ya utekelezaji.

Mhe Ridhiwani amesema hayo mkoani Iringa wakati akizungumza na Walengwa wa Tasaf  wa Kata ya Ruaha iliyopo katika Manispaa ya Iringa  mara baada ya kukagua daraja lilojengwa katika eneo la Kingemgosi  ikiwa ni utekelezaji wa shughuli za Mpango wa Kunusuru Kaya Masikini unaotekelezwa na TASAF.

Kwa mujibu wa taarifa ya TASAF mkoa wa Iringa inaonesha kuwa jumla ya miradi 474 ikiwemo uchimbaji wa visima vya asili, utengenezaji wa barabara, uzibaji wa makorongo na kuanzishwa kwa mashamba ya korosho ilitekelezwa kati ya Julai 2022 na Juni 2023.

Pia,  mkoa ulipokea  jumla ya  shilingi  bilioni 10.3, kati ya hizo shilingi bilioni 8.9 zilitolewa kwa Walengwa 30,988 kutoka vijiji 585 wakati shilingi  bilioni 21.6 zilikuwa ni kwa ajili ya usimamizi  ngazi ya mkoa na halmashauri.

“Nimefarijika sana kwa namna shughuli za TASAF zinavofanyika hapa katika mkoa wa Iringa likiwemo daraja lililojengwa katika eneo la Kigenamgosi,  haya ni matokeo ya ushirikiano thabiti kati ya uongozi wa mkoa na watendaji wote wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii,” amesema.

Kwa upande wake, Mwakilishi Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF Oscar Maduhu amewahakikishia na walengwa wa TASAF kuwa waendelea kubuni miradi ya kimaendeleo kwani serikali imetanga jumla ya Sh. 51 bilioni kwa ajili ya Walengwa hao.

 “TASAF inaendelea kuhakikisha walengwa wote wanahudumiwa ipasavyo ili kuwaondoa katika hali ya umasikini uliokithiri kupitia ruzuku,miradi ya ajira za muda pamoja na kuwapa elimu ya kuweka na kukopa katika vikundi mbalimbali,” alisema Maduhu.

Awali, Mkuu wa wilaya ya Iringa Mjini, Mhe. Veronika Kessy amesema mpango wa TASAF umesaidia kuinua hali za uchumi kwa walengwa pamoja na kuchechemua biashara mbalimbali kwa wananchi wenye kipato cha chini.

Amesema, utoaji fedha za Mpango umewezesha kaya za walengwa kuboresha makazi na kujenga nyumba za matofali ya kuchoma na kuezeka kwa bati badala ya nyasi.

“Hadi kufikia mwezi Juni 2023, jumla ya walengwa 918 wa TASAF katika mkoa wa Iringa waliweza kuboresha makazi yao,” amesema.


Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete akizungumza na wanufaika wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii  (TASAF) mara baada ya kukagua daraja lilijengwa na wanufaika hao kataika eneo la Kinegamgosi, Kata ya Ruaha mkoani Iringa
Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete akiwa ameambatana na baadhi ya viongozi wa mkoa wa Iringa wakikagua daraja lilijengwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii  (TASAF)  wanufaika hao katika eneo la Kinegamgosi, Kata ya Ruaha mkoani Iringa
Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Oscar Maduhu akizungumza  wanufaika wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii  (TASAF)     mara baada ya Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Ridhiwani Kikwete  kuzungumza nao.
Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Iringa , Mhe. Rita Kabati akizungumza  wanufaika wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii  (TASAF)     mara kabla ya Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Ridhiwani Kikwete  kuzungumza nao.
Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini , Mhe. Jesca Msambatavangu akizungumza  wanufaika wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii  (TASAF)     mara kabla ya Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Ridhiwani Kikwete  kuzungumza nao.


 Sehemu ya wanufaika wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii  (TASAF) wakifurahia jambo wakati Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete alipokuwa akizungumza nao katika kata ya Ruaha iliyopo katika Manispaa ya Iringa

 


Tuesday, November 21, 2023

WAZIRI KIKWETE AFUNGUA MAFUNZO YA MFUMO MPYA WA UTENDAJI KAZI KWA WATUMISHI WA UMMA MKOANI IRINGA

 

Na.Lusungu Helela-Iringa 
21/11/2023 

Naibu  Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete amefungua mafunzo ya  mfumo mpya wa usimamizi wa utendaji kazi wa mtumishi na taasisi katika utumishi wa umma (PEPMIS & PIPMIS)   mkoani Iringa ambapo amesema mfumo huo utakuwa mwarobaini kwa watumishi wasiotekeleza wajibu wao.

 Aidha, Mhe. Kikwete amefungua pia mafunzo ya  mfumo wa tathmini ya mahitaji ya rasilimaliwatu utakaowezesha kubainisha mahitaji ya rasilimaliwatu katika Taasisi husika.

Akizungumza leo Mkoani Iringa na watumishi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa zilizopo mkoani Iringa pamoja  na Taasisi na Mashirika ya umma,  Mhe. Kikwete amesema mifumo hiyo imelenga katika  kuboresha utendaji kazi unaojali matokeo na tija katika kutoa huduma bora kwa wananchi.

‘’Tumetuma watalaamu nchi nzima kwa  ajili ya kujenga uelewa wa namna ya kutumia mifumo hiyo ya kidigitali ambayo tunaamini itasaidia watumishi wa umma kuwahudumia wananchi kwa viwango vya juu’’ amesema Mhe. Kikwete.

Hata hivyo, Mhe. Kikwete amesema mwanzo  Serikali ilikuwa ikitumia mfumo wa wazi wa mapitio na upimaji wa utendaji kazi (OPRAS) kusimamia utendaji kazi wa watumishi wa umma lakini kutokana na changamoto zake imeamua kuja na mfumo mpya ambao utajibu changamoto za mfumo wa OPRAS. 

Awali, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Halima Dendego amesema Mkoa ameishukuru Ofisi ya  Rais, UTUMISHI kwa kufika Iringa kwa ajili ya kutoa mafunzo ya namna ya kutumia mifumo hiyo ya kidigitali kwa ajili ya kupima utendaji kazi wa watumishi wake ambapo ameihakikishia ofisi hiyo kupata ushirikiano wa kutosha .

Timu ya wataalamu kutoka Ofisi ya Rais, UTUMISHI ikiongozwa na Mkurugenzi wa Idara ya  Mikataba    ya Utendaji Kazi, Bi. Zainab Kutengezah ipo mkoani Iringa kwa ajili ya kutoa mafunzo kwa watumishi ya namna bora ya kutumia mifumo hiyo

Naibu  Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akizungumza na Watumishi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa zilizopo mkoani Iringa pamoja  na Taasisi na Mashirika ya umma wakati akifungua mafunzo ya  mfumo mpya wa usimamizi wa utendaji kazi wa mtumishi na taasisi katika utumishi wa umma (PEPMIS & PIPMIS/ HRA
Naibu  Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akizungumza na Watumishi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa zilizopo mkoani Iringa pamoja  na Taasisi na Mashirika ya umma wakati akifungua mafunzo ya  mfumo mpya wa usimamizi wa utendaji kazi wa mtumishi na taasisi katika utumishi wa umma (PEPMIS & PIPMIS/ HRA
Mkurugenzi wa Mikataba na  Utendaji Kazi Serikalini , Bi. Zainab Kutengezah akiwa na baadhi ya Viongozi wa Taasisi za Umma Mkoani Iringa   akimskiliza Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumshi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwan Kikwete wakati akifungua  wakati akifungua mafunzo ya  mfumo mpya wa usimamizi wa utendaji kazi wa mtumishi na taasisi katika utumishi wa umma (PEPMIS & PIPMIS/ HRA 
Mkuu wa Mkoa wa Iringa Mhe.Halima Dendego akizungumza kabla ya kuumkaribisha Naibu  Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete na Watumishi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa zilizopo mkoani Iringa pamoja  na Taasisi na Mashirika ya umma wakati akifungua mafunzo ya  mfumo mpya wa usimamizi wa utendaji kazi wa mtumishi na taasisi katika utumishi wa umma (PEPMIS & PIPMIS/ HRA
Naibu  Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akisoma  taarifa ya hali ya watumishi Mkoani  Iringa kabla ya   kufungua mafunzo ya  mfumo mpya wa usimamizi wa utendaji kazi wa mtumishi na taasisi katika utumishi wa umma (PEPMIS & PIPMIS/ HRA



Baadhi ya timu ya wataalamu kutoka Ofisi ya Rais, UTUMISHI ikiongozwa na Mkurugenzi wa Mikataba na  Utendaji Kazi, Bi. Zainab Kutengezah ambayo ipo mkoani Iringa kwa ajili ya kutoa mafunzo kwa watumishi ya namna bora ya kutumia mifumo hiyo wakimsikiliza Naibu  Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete wakati akifungua mkutano huo .