Monday, November 20, 2023

MHE. SIMBACHAWENE AWATAKA VIONGOZI WA TAKUKURU KUBADILI CHANGAMOTO KUWA FURSA

 Na. Rainer Budodi na Veronica Mwafisi-Dodoma

Tarehe 20 Novemba, 2023

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene amewataka Viongozi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa  (TAKUKURU) kutafakari kwa kina na kujadili changamoto zinazowakabili katika utendaji kazi na kuzifanya kuwa fursa kwa maendeleo ya Taifa.

Mhe. Simbachawene amesema hayo leo tarehe 20 Novemba, 2023 wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Viongozi wa TAKUKURU-2023 katika ukumbi wa St. Gasper jijini Dodoma.

“Ninaamini mtatumia fursa ya mkutano huu wa mwaka kujadili masuala yote yanayoonekana kuwa ni changamoto katika utendaji kazi ili kupata suluhu ya pamoja” ameongeza Mhe. Simbachawene.

Aidha, katika hotuba yake amebainisha kuwa kila mmoja katika mazingira tofauti na kwa namna ya pekee ameruhusu au ameathiriwa na rushwa, hivyo ametoa rai kwa wananchi wote kuhakikisha wanazuia mianya ya rushwa ili kutoathiri vizazi vijavyo.

Mhe. Simbachawene ameongeza kuwa TAKUKURU inatakiwa kuitumia vizuri programu iliyoianzisha ya TAKUKURU Rafiki kwa lengo la kupanua wigo na kuwashirikisha wananchi katika kupambana na rushwa.

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Kamishna wa Polisi Salum Hamduni amesema ofisi yake inaendelea na utekelezaji wa shughuli zake kwa mujibu wa Sheria na sasa wamejikita zaidi katika kuzuia rushwa.

“Tunaendelea na kazi ya kuelimisha umma kuhusu masuala ya rushwa na kufuatilia utekelezaji wa miradi ya Serikali ambapo tumeokoa fedha nyingi ambazo kama isingekuwa TAKUKURU basi fedha hizo zingeishia mikononi mwa watu binafsi” amesema Bw. Hamduni.

Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Viongozi wa TAKUKURU hufanyika kila mwaka kwa lengo la kubainisha changamoto zinazowakabili katika utendaji kazi wao na kutafuta ufumbuzi wa pamoja. Mkutano huu wa Mwaka kwa mwaka 2023 una kaulimbiu ya Kuzuia rushwa ni jukumu lako na langu, tutimize wajibu wetu.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene akizungumza na Viongozi wa TAKUKURU wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Mwaka 2023 wa Viongozi hao jijini Dodoma.


Sehemu ya Viongozi wa TAKUKURU na Wawezeshaji wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene (hayupo pichani) wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Mwaka 2023 jijini Dodoma.


Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Kamisha wa Polisi, Salum Hamduni akitoa taarifa fupi ya utekelezaji wa majukumu ya ofisi yake kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka 2023 wa Viongozi wa Taasisi hiyo uliofanyika jijini Dodoma.


Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Kamisha wa Polisi, Salum Hamduni akimkabidhi Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene tuzo ya kuthamini mchango wake katika mapambano dhidi ya rushwa wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka 2023 wa Viongozi wa Taasisi hiyo uliofanyika jijini Dodoma.


Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Bi. Neema Mwakalyelye akitoa neno la utangulizi wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka 2023 wa Viongozi wa TAKUKURU uliofanyika jijini Dodoma.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene akisalimiana na Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Kamisha wa Polisi, Salum Hamduni mara baada ya kuwasili katika ukumbi wa St. Gasper jijini Dodoma kwenye ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Mwaka 2023 wa Viongozi wa TAKUKURU. Katikati ni Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Bi. Rosemary Senyamule.



No comments:

Post a Comment