Friday, March 19, 2021

Thursday, March 18, 2021

Monday, March 15, 2021

TASAF KUJENGA WODI YA AKINA MAMA NA MAABARA KIJIJI CHA MKAMBARANI

 Na. James K. Mwanamyoto-Morogoro

Tarehe 15 Machi, 2021

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi ameiahidi Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kupitia TASAF kujenga wodi ya kuwahudumia akina mama wajawazito na maabara katika zahanati ya Kijiji cha Mkambarani ili wananchi wa kijiji hicho wapate huduma bora za afya.

Mhe. Ndejembi ametoa ahadi hiyo ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya kamati hiyo ya kudumu iliyoelekeza Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kujenga jengo la kina mama kwa ajili ya kuwapatia huduma stahiki, ikiwa ni pamoja na kujenga maabara itakayotoa huduma bora ya vipimo kwa wananchi wa Kijiji cha Mkambarani.

Mhe. Ndejembi amesema, kutokana na maelekezo yaliyotolewa na kamati ofisi yake itajenga wodi ya akina mama ili kuwe na faragha wakati wa kuwahudumia akina mama wajawazito.

Kuhusu maelekezo ya ujenzi wa maabara, Mhe. Ndejembi ameihakikishia kamati na wananchi wa Kijiji cha Mkambarani kujenga maabara ili kuwaondolea adha wananchi hao ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma ya maabara ambapo pia hulazimika kuingia gharama kubwa.

Mhe. Ndejembi ameongeza kuwa, lengo la Serikali kujenga zahanati ya Mkambarani ni kuwasogezea karibu huduma za afya wananchi wa eneo hilo ikizingatiwa kuwa, walengwa wa TASAF watanufaika pia na huduma zinazotolewa na zahanati hiyo na hatimaye kuwa na afya bora itakayowawezesha kupambana na umaskini kupitia ruzuku ya TASAF wanayoipata.

Awali, akitoa maelekezo kwa Serikali kwa niaba ya kamati yake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Humphrey Polepole (Mb) amesema Kamati imelazimika kutoa maelekezo ya ujenzi wa Wodi ya akina mama na maabara kama sehemu ya kulinda utu wa wananchi hususani akina mama wanaofuata huduma ya uzazi katika zahanati ya Mkambarani.  

Mhe. Polepole amesema, wodi ya akina mama ikijengwa itaongeza usiri na faragha wakati wa kuwahudumia wajawazito tofauti la ilivyo sasa ambapo hakuna usiri wa kutosha wala faragha pindi akina mama wanapohudumiwa.

Kuhusiana na maelekezo ya ujenzi wa maabara, Mhe. Polepole ameeleza kuwa, kamati yake imepata fursa ya kuitembelea zahanati ya Mkambarani na kubaini kuwa hakuna maabara inayokidhi mahitaji ndio maana kamati yake imeielekeza Serikali kujenga maabara itakayokidhi kutoa huduma stahiki kwa wananchi wa Kijiji cha Mkambarani.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa imemaliza ziara ya kikazi ya siku tatu mkoani Dar es Salaam, Pwani na Morogoro iliyolenga kukagua utekelezaji wa miradi inayotekelezwa na taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Humphrey Polepole (Mb) akitoa maelekezo kwa Serikali kuhusu ujenzi wa wodi ya kuwahudumia akina mama wajawazito na maabara katika zahanati ya Kijiji cha Mkambarani.

Baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Mkambarani-Morogoro wakimsikiliza Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Humphrey Polepole (hayupo pichani) wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF kijijini hapo.



Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Humphrey Polepole (Mb) na baadhi ya wajumbe wa kamati yake pamoja na watendaji wa Serikali wakikagua zahanati ya Mkambarani wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF kijijini hapo.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akizungumza kuhusu utekelezaji wa maelekezo ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF katika Kijiji cha Mkambarani - Morogoro.


Mmoja wa wanufaika wa TASAF wa Kijiji cha Mkambarani Mzee Abdallah J. Kinyaku akitoa ushuhuda wa namna alivyonufaika na TASAF kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa mpiradi ya TASAF kijijini hapo.


TASAF KUBORESHA BWAWA LA MAJI KIJIJI CHA KALOLENI ILI KUWAPATIA WANANCHI MAJI SAFI NA SALAMA

 Na. James K. Mwanamyoto-Chalinze

Tarehe 14 Machi, 2021

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi ameiahidi Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuboresha mfumo wa bwawa la maji Kijiji cha Kaloleni kata ya Ubena Zomozi iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Chalinze ili kuwapatia wananchi wa eneo hilo maji safi na salama.

Mhe. Ndejembi ametoa ahadi hiyo ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya kamati iliyoitaka Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kurekebisha mfumo wa bwawa hilo ili kuwapatia maji safi na salama wananchi  wa kaloleni na vijiji jirani.

Mhe. Ndejembi amefafanua kuwa, licha ya mradi wa bwawa hilo kujengwa wakati wa awamu ya kwanza ya utekelezaji wa TASAF lakini kutokana na changamoto ya upatikanaji wa maji safi na salama inayowakabili wananchi wa eneo la Kaloleni na vijiji jirani, Serikali itafanya marekebisho kuwawezesha wananchi kupata huduma hiyo ya maji.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF Bw. Ladislaus Mwamanga amesema, ofisi yake itapeleka wataalam mapema iwezekanavyo ili kufanya tathmini ya namna bora ya kuboresha bwawa hilo.

Bw. Mwamanga ameongeza kuwa, fedha ya kufanya maboresho hayo ipo kwani mradi huo ni kipambule cha Serikali katika Utekelezaji wa Mradi wa kipindi cha pili cha Awamu ya Tatu kilichozinduliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli.

Awali akitoa maelekezo juu ya uboreshaji wa bwawa hilo, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa Mhe. Humphrey Polepole (Mb) amesema, kamati imelazimika kutoa maelekezo hayo  kutokana na umuhimu wa bwawa hilo kwa wananchi wa kijiji hicho na vijiji jirani.

Aidha, Mhe. Polepole amewataka wasimamizi wa mradi na wananchi kuhakikisha wanalitunza bwawa hilo ili wanufaike na uwepo wake kama Serikali ilivyokusudia.

Mradi wa bwawa la maji Kaloleni ulijengwa katika kipindi cha kwanza cha utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini Awamu ya Kwanza kwa lengo la kuwapatia maji safi na salama wananchi wa Kaloleni na vijiji jirani, ikiwa ni pamoja na kuiwezesha mifugo yao kupata maji ya kunywa.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Humphrey Polepole (Mb) akitoa maelekezo ya kuboresha mfumo wa bwawa la maji la Kijiji cha Kaloleni kata ya Ubena Zomozi kwa niaba ya kamati anayoiongoza.



Baadhi ya wananchi wa Kaloleni kata ya Ubena Zomozi iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Chalinze wakisikiliza Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Humphrey Polepole (Hayupo pichani) wakati akitoa maelekezo ya kuboresha mfumo wa bwawa la maji la kijiji chao.


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Humphrey Polepole (Mb) akikagua mradi wa bwawa la maji la Kijiji cha Kaloleni kata ya Ubena Zomozi.


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Humphrey Polepole (Mb) akiteta jambo na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi mara baada ya kukagua mradi wa bwawa la maji la Kijiji cha Kaloleni kata ya Ubena Zomozi.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akiiahidi Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuboresha mfumo wa bwawa la maji Kijiji cha Kaloleni kata ya Ubena Zomozi ili kuwapatia wananchi wa eneo hilo maji safi na salama.


Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Bw. Ladislaus Mwamanga akiiahidi Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuleta wataalam kufanya tathmini ya namna bora ya kuboresha bwawa la Kijiji cha Kaloleni kata ya Ubena Zomozi.



Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Humphrey Polepole (Mb) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wajumbe wa kamati yake na watendaji wa Serikali mbele ya mradi wa bwawa la maji la Kijiji cha Kaloleni kata ya Ubena Zomozi.


 

Saturday, March 13, 2021

CHUO CHA UTUMISHI WA UMMA CHATAKIWA KUENDELEA KUJENGA NIDHAMU NA UADILIFU KWA WATUMISHI WA UMMA


Na. James K. Mwanamyoto-Dar es Salaam

Tarehe 13 Machi, 2021 

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa Mhe. Humprey Polepole (Mb) amesema Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) kina jukumu la kuhakikisha kinaendelea kujenga nidhamu na uadilifu kwa watumishi wa umma na viongozi katika Utumishi wa Umma ili waweze kutoa mchango katika maendeleo ya taifa.

Mhe. Polepole ametoa rai hiyo mara baada ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa anayoiongoza kutembelea makao makuu ya Chuo cha Utumishi wa Umma jijini Dar es Salaam, kwa lengo la kukagua utekelezaji wa majukumu ya chuo hicho chenye dhamana ya kutoa mafunzo kwa Watumishi wa Umma yanayowawezesha kutoa huduma bora kwa wananchi.

Mhe. Polepole amesema, chuo hakina budi kuendelea kutoa mafunzo yenye tija ili kizazi kipya kilichoingia na kinachoendelea kuingia katika Utumishi wa Umma kiendelee kuishi katika mila, utamaduni, desturi na miiko ya Utumishi wa Umma.

Mhe. Polepole amefafanua kuwa, Utumishi wa Umma nchini umejengeka katika mila, utamaduni, na desturi, hivyo Chuo cha Utumishi wa Umma pekee ndio kina jukumu la msingi kuhakikisha kinatoa mafunzo ambayo yatajenga utamaduni utakaoimarisha nidhamu ya utendaji kazi, uadilifu na uzalendo kwa Watumishi wa Umma.

Kwa upande wake, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi ameihakikishia Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuwa, suala la kuwajengea uwezo Watumishi wa Umma kiutendaji na nidhamu limepewa uzito unaostahili na ofisi yake kwa kuwataka waajiri wote kuhakikisha wanatenga bajeti itakayowawezesha watumishi wao kupata mafunzo yanayotolewa katika Chuo cha Utumishi wa Umma.

Aidha, Mhe. Ndejembi amewaomba wajumbe wa kamati hiyo kutumia mamlaka waliyonayo kushirikiana na Ofisi yake kuwahimiza Wakurugenzi wa Halmashauri, Makatibu Tawala wa Mikoa na Wakuu wa Taasisi za Umma kutenga fedha zitakazowawezesha Watumishi wa Umma kupata mafunzo katika Chuo cha Utumishi wa Umma.

Mhe. Ndejembi ameiahidi kufanyia kazi maelekezo yote yaliyotolewa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa ili kuboresha huduma zinazotolewa na Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania. 

Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kilianzishwa kwa lengo la kutoa mafunzo katika Nyanja za uongozi, menejimenti na utawala kwa ngazi za Cheti, Stashada na Astashahada. Pia chuo kinafanya utafiti na kutoa ushauri wa kitaalam.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Humprey Polepole (Mb) akiwahimiza Watumishi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) Kampasi ya Dar es Salaam kutoa mafunzo yatakayowajengea Watumishi wa Umma nchini nidhamu ya Utendaji kazi na uadilifu. 


Baadhi ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa na watumishi wa TPSC wakisikiliza maelekezo ya Mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Humprey Polepole (Mb) wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo yenye lengo la kukagua utekelezaji wa majukumu ya TPSC.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akizungumza na Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa (hawapo pichani) wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo katika Chuo cha Utumishi wa Umma yenye lengo la kukagua utekelezaji wa majukumu ya chuo hicho.


Baadhi ya watumishi wa Chuo cha Utumishi wa Umma, Kampasi ya Dar es Salaam wakimsikiliza Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Humprey Polepole (Mb) wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo yenye lengo la kukagua utekelezaji wa majukumu ya TPSC.



Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa Mhe. Saashisha Mafue ambaye ni mnufaika wa mafunzo yanayotolewa na Chuo cha Utumishi wa Umma akitoa ushuhuda wa namna alivyopata mafunzo katika chuo hicho wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo yenye lengo la kukagua utekelezaji wa majukumu ya TPSC.


Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania Dkt. Emmanuel Shindika akitoa taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya chuo chake kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo yenye lengo la kukagua utekelezaji wa majukumu ya TPSC.


Monday, March 8, 2021

WATUMISHI WANAWAKE NI WACHAPAKAZI MAHIRI KATIKA UTUMISHI WA UMMA

 Na. James K. Mwanamyoto-Dodoma

Tarehe 08 Machi, 2021

Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Francis Michael amesema Watumishi wa Umma wanawake ni wachapakazi mahiri katika Utumishi wa Umma nchini.

Dkt. Michael amepongeza uchapakazi wa watumishi wanawake mapema leo wakati akitoa ujumbe maalum wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI kuhusu Maadhimisho ya Siku ya Wanawake duniani Machi 8, 2021 ikiwa ni sehemu ya ofisi yake kutambua mchango wa Watumishi wa Umma wanawake katika utoaji huduma kwa wananchi.

 Dkt. Michael amesema, kutokana na uchapakazi wa watumishi wanawake, Ofisi ya Rais-UTUMISHI iliona kuwa ina wajibu wa kuhakikisha watumishi wanawake wanashirikishwa kikamilifu kwenye nafasi za uongozi.

 Amefafanua kuwa, kwa upande wa nafasi za Ukurugenzi ambapo ofisi ina jumla ya Wakurugenzi 13, wanawake wapo 6 sawa na asilimia arobaini na sita (46%) wakati wanaume wapo 7 ambao ni asilimia hamsini na nne (54%).

Ameongeza kuwa, kwa upande wa Wakurugenzi Wasaidizi ofisi ina jumla ya Wakurugenzi Wasaidizi 22, kati ya hao 12 ni wanawake ambao ni sawa na asilimia hamsini na tano (55%) wakati 10 ni wanaume ambao ni sawa na asilimia arobaini na tano (45%).

“Ukitazama takwimu ya idadi ya Wakurugenzi na Wakurugenzi Wasaidizi waliopo katika Ofisi yetu inadhihirisha kuwa, Ofisi imetoa fursa za uongozi kwa wanawake ambao pasipo na shaka yoyote wameuthibitishia umma kuwa, wana uwezo kiutendaji kwa kutekeleza majukumu yao kikamilifu”, amefafanua Dkt. Michael.

Dkt. Michael ametoa wito kwa waajiri katika Taasisi za Umma kuhakikisha wanawashirikisha watumishi wanawake katika masuala muhimu yanayohusu maendeleo ya taasisi zao kwani wanao uwezo kiutendaji  katika kuhakikisha taifa linapata maendeleo.

Aidha, ametoa wito kwa Watumishi wa Umma katika Taasisi zote za Umma kuwapa ushirikiano wa dhati viongozi wanawake walioteuliwa na mamlaka mbalimbali ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi.

Sanjali na hilo, amewataka Watendaji Wakuu katika Taasisi za Umma kuwapendekeza wanawake katika nafasi mbalimbali za uongozi ili kutoa fursa kwa wanawake kushiriki katika ujenzi wa taifa.

Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kama msimamizi wa masuala ya kiutumishi na utawala bora nchini inaungana na Watanzania na wadau wote Kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani Machi 8, 2021, ikiwa ni sehemu ya kutambua mchango wa viongozi wanawake katika Utumishi wa Umma kama kaulimbiu ya maadhimisho ya mwaka huu inavyojianisha kuwa “Wanawake katika Uongozi: Chachu kufikia Dunia yenye Usawa”.

Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Francis Michael akitoa ujumbe kuhusu Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Machi 8, 2021, ikiwa ni sehemu ya kutambua mchango wa Watumishi wa Umma wanawake katika kutoa huduma kwa wananchi.



Afisa Habari wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Bi. Veronica Mwafisi akifanya mahojiano na Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Francis Michael kuhusu Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani Machi 8, 2021. 


Baadhi ya Watumishi wa Umma wanawake wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya kushiriki Maadhimisho ya Siku ya Wanawake kimkoa Machi 8, 2021 jijini Dodoma.


Baadhi ya Watumishi wa Umma wanawake wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakiwa katika maandamano ya Siku ya Wanawake kimkoa Machi 8, 2021 jijini Dodoma.