Wednesday, May 27, 2026

KATIBU MKUU-UTUMISHI AWAITA DODOMA WAKUU WA IDARA NA VITENGO VYA UTAWALA NA USIMAMIZI WA RASILIMALIWATU SERIKALINI.

Na Antonia Mbwambo na Eric Amani-Dodoma

Tarehe 26 Mei, 2026

Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI,   Bw. Juma Mkomi, amewasisitiza Wakuu wa Idara na Vitengo vya Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Serikalini kushiriki kikao kazi muhimu kilichopangwa kufanyika tarehe 1-3 Juni, 2026 katika ukumbi wa mabele hall jijini Dodoma.

Bw. Mkomi ametoa msisitizo huo Mei 26, 2026 wakati wa Mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI uliopo Mtumba jijini Dodoma

“Natoa wito kwa Wakuu wa Idara na vitengo vya Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu kuhudhuria wao wenyewe katika kikao hicho bila kukosa kwakuwa kikao hiki kitakuwa na maelekezo mahususi ya kuboresha utendaji kazi.” Bw. Mkomi alisema.

Aidha, Bw. Mkomi amebainisha kuwa kikao hicho kitajadili na kufafanua kuhusu matumizi ya Mifumo mbalimbali ya kidijiti ikiwemo e-uhamisho, e-watumishi, e-utendaji, e-mrejesho na hr-assesment kwa kuzingatia shabaha za vipaumbele vya Taifa kuelekea dira 2050.

Ameongeza kuwa kikao hicho kitatoa nafasi ya kujadili kuhusu changamoto na mafanikio yaliyopo katika utawala na usimamizi wa rasilimaliwatu na mapendekezo ya namna bora ya kuzishughulikia changamoto hizo. Pia washiriki watapata fursa ya kubadilishana uzoefu na kuimarisha utendaji kazi katika Taasisi za Umma.

Bw. Mkomi amewataka washiriki kujisajili katika mfumo kupitia link ya tsms.gov.go.tz huku wakizingatia kwamba mwisho wa usajili ni tarehe 29 Juni, 2026.

Vile vile, Wakuu wa Idara na vitengo vya Usimamizi wa Rasilimaliwatu wamesisitizwa kufika katika ukumbi wa Mabele Hall uliopo jijini Dodoma tarehe 31 Mei, 2026 kuanzia saa 4 asubuhi kwa ajili ya kuchukua vitambulishi vyao vitakavyotumika katika kikao hicho.Kikao kazi hicho kitaongozwa na kauli mbiu isemayo; “Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu katika Utumishi wa ulio Sikivu,Jumuishi wenye Matokeo na Uwajibikaji kuelekea Dira 2050”.

Mwandishi wa Habari kutoka kituo cha habari cha ITV Ndg. Michael Msilo akimuuliza swali katibu Mkuu Ofisi ya Rais – UTUMISHI Bw. Juma Mkomi (hayupo pichani) kwenye mkutano na waandishi hao leo Mei 26, 2026 juu ya Kikao kazi cha Wakuu wa Idara za Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu katika Wizara, Idara zinazojitegemea pamoja na Wakala wa serikali za Mtaa kinachotarajiwa kufanyika Juni 1 hadi 3 jijini Dodoma


Baadhi ya Waandishi wa Habari wakimsikiliza katibu Mkuu Ofisi ya Rais – UTUMISHI Bw. Juma Mkomi (Katikati) wakati walipohudhuria mkutano wa waandishi wa habari katika ukumbi wa ofisi hiyo uliyopo Mtumba Jijini Dodoma Mei 26, 2026




Mwandishi wa Habari kutoka kituo cha habari cha BBC Ndg. Ronald Sonyo akimuuliza swali katibu Mkuu Ofisi ya Rais – UTUMISHI Bw. Juma Mkomi (hayupo pichani) kwenye mkutano na waandishi hao leo Mei 26, 2026 juu ya Kikao kazi cha Wakuu wa Idara za Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu katika Wizara, Idara zinazojitegemea pamoja na Wakala wa serikali za Mtaa kinachotarajiwa kufanyika Juni 1 hadi 3 jijini Dodoma  


Baadhi ya Wakurugenzi Wakuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakimsikiliza Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma Bw. Juma Mkomi (hayupo pichani) wakati akifanya mkutano na waandishi wa habari katika ukumbi wa ofisi hiyo leo Mei 26, 2026 Mtumba, Dodoma.




Tuesday, May 26, 2026

HERI YA SIKUKUU YA EID AL ADHA

 


KATIBU MKUU MKOMI AWATAKA WATUMISHI WA UMMA KUWA NA UHUSIANO MZURI KAZINI NA NJE YA KAZI

 Na Eric Amani. Mtumba-Dodoma.

Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bw. Juma Mkomi amewataka watumishi wa umma kujenga na kudumisha uhusiano mzuri katika maeneo yao ya kazi na nje ya kazi ili kuongeza ufanisi wa utendaji kazi, kuimarisha mshikamano na kujenga taswira nzuri ya Utumishi wa Umma kwa jamii.

Akizungumza leo Mei 25, 2026 wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji watumishi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Mkomi amesema kuwa mazingira mazuri ya kazi hujengwa kupitia ushirikiano, kuheshimiana, mawasiliano bora na kuthaminiana miongoni mwa watumishi.

“Watumishi wa Umma tunapaswa kuwa mfano mzuri kwa jamii kwa kuzingatia maadili, nidhamu na kujenga mahusiano chanya siyo tu ofisini bali hata nje ya maeneo ya kazi. Umoja wetu una mchango mkubwa katika kuongeza tija na ubora wa huduma tunazozitoa kwa Umma,” amesema Bw. Mkomi.

Aidha, amewapongeza watumishi kwa kuendelea kushiriki kikamilifu katika mafunzo hayo ya kila Jumatatu ambayo yamekuwa yakisaidia kuongeza uelewa, kuimarisha utendaji kazi na kujenga ari mpya ya kuwahudumia wananchi kwa weledi na uwajibikaji mkubwa zaidi.

Katibu Mkuu Mkomi pia amewataka watumishi kuendelea kushikamana, kusaidiana na kudumisha heshima baina yao ili kuifanya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kuwa mfano wa kuigwa katika utoaji wa huduma bora Serikalini.

Mafunzo hayo hutolewa kila siku ya Jumatatu katika eneo la Ofisi hiyo Mtumba, jijini Dodoma kwa lengo la kuwajengea uwezo watumishi katika maeneo mbalimbali ya kiutendaji, maadili ya Utumishi wa Umma pamoja na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma Bw. Juma Mkomi akitoa neno kwa watumishi wa Ofisi hiyo wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo watumishi hao Mei 25, 2026 Mtumba, Jijini Dodoma.

Naibu katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Ummma na Utawala Bora Bw. Xavier Daudi( Wa kwanza Kulia)  akiwa na Baadhi ya Wakurugenzi na Wakurugenzi Wasaidizi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mei 25, 2026 wakimsikiliza mwezeshaji SACP Ibrahim Mahumi (Hayupo kwenye Picha) wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo yanayofanyika kila jumatatu katika eneo la Ofisi hiyo Mtumba, Dodoma. 

Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Utumishi wa Umma SACP. Ibrahim Mahumi akitoa mafunzo ya kuwajengea uwezo watumishi wa Ofisi ya Rais – UTUMISHI Mei 25, 2025 Mtumba, Dodoma.


Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma Bw. Juma Mkomi (Aliyevaa Suti ya Blue) akiwa pamoja na Naibu katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Ummma na Utawala Bora Bw. Xavier Daudi (watatu kutokea kushoto) wakimsikiliza mwezeshaji (hayupo pichani) wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo watumishi wa ofisi hiyo. 

Baadhi ya Watumishi wa Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakisikiliza mafunzo kutoka kwa mwezeshaji (hayupo pichani) Mei 25, 2026 katika eneo la ofisi hiyo iliyopo mji wa Serikali Mtumba, Dodoma.