Tuesday, February 17, 2026

MSIHAMISHE WATUMISHI KWA KIGEZO CHA KUTOFAA KIUTENDAJI MUWAJENGEE UWEZO “Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Dkt. Kusiluka”

Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka amewataka waajiri katika taasisi za umma kuacha tabia ya kuomba kuhamisha watumishi kutoka katika vituo vyao vya kazi na kuwapeleka kwingine kwa kisingizio cha kutokuwa na uwezo kiutendaji.

Balozi Dkt. Kusiluka amepiga marufuku hiyo leo tarehe 17 Februari, 2026 katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC) jijini Arusha wakati akifungua rasmi mkutano wa sita wa Serikali Mtandao.

Amesema kumekuwa na tabia ya baadhi ya waajiri kupenda kuwahamisha watumishi na kutaka kupewa mbadala ambapo amemuelekeza Katibu Mkuu-UTUMISHI kutofanya hivyo.  “Utumishi msifanye mambo hayo ya kuhamisha hamisha watumishi kwa kigezo cha kutofaa kiutendaji badala yake wapewe mafunzo ili waendane na utendaji kazi wa taaluma husika,” amesisitiza.

Ameongeza kuwa, mtumishi ambaye hayuko vizuri kiutendaji ukimuhamishia kituo kingine hawezi kubadilika kwani kinachotakiwa hapo ni kujengewa uwezo na jukumu hilo ni la mwajiri wa taasisi husika.

Amesema kila mtumishi anatakiwa kupata mafunzo ya mara kwa mara lakini ni muhimu zaidi kwa wataalamu wa TEHAMA kwani teknolojia imekuwa ikibadilika, hivyo mtaalam wa TEHAMA asipopata mafunzo ya mara kwa mara ataachwa nyuma.

Ameongeza kuwa kujengewa uwezo wa kitaaluma unaweza kutekelezwa kwa namna mbalimbali ikiwemo kufanya vikao vya ndani na kuwasikiliza au kuwapeleka katika taasisi nyingine za sekta binafsi kwa mkataba.

Aidha, amewaelekeza waajiri kuweka vizuri utaratibu wa majukumu yao ili kuwarahisishia wataalamu wa TEHAMA pindi wanapotaka kubuni na kusanifu mifumo ya TEHAMA.

Amesema TEHAMA ni kipaumbele cha Serikali na hata Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na Viongozi wengine wamekuwa wakitumia TEHAMA kwa kiwango kikubwa katika utekelezaji wa majukumu ya serikali.

Ameipongeza e-GA kwa kubuni na kusanifu mifumo mbalimbali ya TEHAMA ambayo imekuwa ikirahisisha utendaji kazi wa kila siku serikalini. “Tuliokuwa katika Utumishi wa Umma tangu zamani tunaona, kulikuwa na vikwazo vingi wakati tunataka kuanza kusanifu mifumo yetu, kuna watu wakasema hatutaweza, lakini sasa tumeweza, niwapongeze sana e-GA, niwasisitize kuendana na kasi ya mabadiliko ya teknolijia ili tusiachwe nyuma,” Katibu Mkuu Kiongozi amesisitiza.

Amesema, Serikali inathamini sana mchango wa sekta binafsi katika maendeleo ya TEHAMA na ndio maana imekuwa ikishirikiana nao. “tuendelee kufanya kazi pamoja kwani tunajenga nchi moja, sote tunawahudumia wananchi, tuendeleze ushirikiano ili tuwahudumie wananchi kikamilifu,” amesisitiza na kutoa angalizo la kusanifu mifumo yenye kuleta tija kwa taifa badala ya kusanifu mifumo itakayosababisha uvunjifu wa Amani. “Ninyi ndio mnaobuni na kusanifu mifumo, hivyo mbuni vitu ambavyo havileti shida kwa jamii na kuwaongoza vijana wetu kutumia mifumo hiyo kwa usahihi.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu Ikulu, kabla ya kumkaribisha Katibu Mkuu Kiongozi kuzungumza na washiriki wa mkutano huo, Bw. Xavier Daudi ambaye ni Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora amesema katika kipindi hiki cha mabadiliko ya kasi ya teknolojia, Serikali Mtandao imeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuimarisha utawala bora na ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wananchi.

Amesema Serikali itaendelea kuimarisha Mamlaka ya Serikali Mtandao, kwa kuitengea rasilimali na kuimarisha miundombinu ya TEHAMA kulingana na mahitaji na mabadiliko ya teknolojia.

Awali akitoa neno la utangulizi , Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) Mhandisi Benedict Ndomba amesema e-GA imeendelea kutekeleza jukumu lake la msingi la kuratibu, kusimamia na kukuza jitihada za Serikali Mtandao, kwa kuhakikisha matumizi ya TEHAMA Serikalini yanakuwa shirikishi, salama, yanazingatia Sheria, Viwango na Miongozo ya Serikali Mtandao, ili kuleta tija katika utoaji wa huduma kwa wananchi kama ilivyoelekezwa katika Sheria ya Serikali Mtandao Na. 10 ya Mwaka 2019.

Mhandisi Ndomba alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada zake za kuwekeza katika sekta ya TEHAMA na kuiwezesha Mamlaka kutekeleza majukumu yake ikiwemo,  ujenzi wa Mfumo unaowezesha Mifumo ya Serikali Kuwasiliana na Kubadilishana taarifa, ujulikanao kama Government Enterprises Service Bus (GovESB). Ubadilishanaji wa taarifa kupitia mfumo huu, umechochea kuongezeka kwa ufanisi wa utendaji kazi katika taasisi za umma na utoaji wa huduma kwa wananchi.


Kikao kazi hicho cha siku tatu kinachoongozwa na Kaulimbiu isemayo Kuboresha Utendaji wa Serikali kwa Kuimarisha Utoaji wa Huduma za Umma Kupitia Mifumo Salama na Jumuishi ya Serikali Mtandao” kimewashirikisha zaidi ya wadau1400 na mada 14 kuhusu serikali mtandao zitawasilishwa kwa lengo la kuboresha utendaji kazi wa masuala ya TEHAMA nchini.

Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka akizungumza na Maafisa Masuuli, Maafisa TEHAMA na watumiaji wa Mifumo ya TEHAMA Serikalini wakati akifungua mkutano wa sita wa Serikali Mtandao katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC) jijini Arusha.


Sehemu ya Maafisa Masuuli, Maafisa TEHAMA na watumiaji wa Mifumo ya TEHAMA Serikalini wakiwa kwenye mkutano wa sita wa Serikali Mtandao uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC) jijini Arusha.


Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora, Bw. Xavier Daudi akitoa maelezo ya awali kabla ya kumkaribisha Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka (hayupo pichani) kufungua mkutano wa sita wa Serikali Mtandao ulioshirikisha Maafisa Masuuli, Maafisa TEHAMA na watumiaji wa Mifumo ya TEHAMA Serikalini uliofanyika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC) jijini Arusha.


Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka (katikati mstari wa mbele) akifuatilia jambo wakati wa mkutano wa sita wa Serikali Mtandao uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC) jijini Arusha. Wa kwanza kulia ni Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora, Bw. Xavier Daudi


Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka (katikati) akisikiliza maelezo kuhusu mifumo mbalimbali kutoka kwa Maafisa wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) kabla ya kufungua mkutano wa sita wa Serikali Mtandao uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC) jijini Arusha. Wa kwanza kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA), Mhandisi Benedict Ndomba.


Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora, Bw. Xavier Daudi akimsikiliza Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka (hayupo pichani) wakati akifungua mkutano wa sita wa Serikali Mtandao katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC) jijini Arusha.



Monday, February 16, 2026

WATUMISHI WA UMMA, WANANCHI WAPEWA NYENZO YA KUWASILIANA NA SERIKALI

Na. Veronica Mwafisi- Dodoma.

Tarehe 16 Februari, 2026 

“Mfumo wa e-Mrejesho unalenga kuboresha huduma zinazotolewa na Serikali na ni sehemu ya utekelezaji wa dhana ya Utawala Bora ambayo inajali maslahi ya wengi, kuwa na uwazi, kupiga vita dhidi ya rushwa, kuleta haki na usawa na kuhimiza uwajibikaji”.


Rai hiyo imetolewa na Mkurugenzi Msaidizi wa Ufuatiliaji na Uzingatiaji wa Maadili, Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Bi. Janet Mishinga alipokuwa akiwasilisha mada kuhusu Mfumo wa e-Mrejesho wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Watumishi wa ofisi hiyo jijini Dodoma.

Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kupitia Idara ya Usimamizi Maadili imewahimiza Watumishi wa Umma na Wananchi kutumia Mfumo wa Kielektroni wa Kutuma, Kupokea na Kufuatilia Malalamiko, Mapendekezo, Maulizo na Pongezi Serikalini (e-Mrejesho) ili kuongeza ufanisi katika kushughulikia mrejesho wa masuala mbalimbali ya kiutumishi na kuboresha huduma kwa umma.


Aidha Bi. Mishinga alifafanua kuwa, ufuatiliaji wa utekelezaji wa mfumo wa e-Mrejesho una lengo la kubaini mafanikio na changamoto ili kuimarisha uadilifu katika kushughulikia mrejesho wa wananchi ikiwa ni pamoja na kufanya tathmini ya utendaji wa taasisi katika kuhudumia wananchi.

Pia, alibainisha kuwa utaratibu wa kushughulikia mrejesho kuhusu mfumo huo unaongeza ushirikishwaji kwa watumishi wa umma na wananchi.

Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Bw. Xavier Daudi (kushoto) akifuatilia wasilisho la mada kuhusu Mfumo wa e-Mrejesho wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Watumishi wa ofisi hiyo ambayo hutolewa kila siku ya Jumatatu kwenye ofisi hiyo iliyopo Mtumba jijini Dodoma.


Mkurugenzi Msaidizi wa Ufuatiliaji na Uzingatiaji wa Maadili, Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Bi. Janet Mishinga akifafanua jambo alipokuwa akiwasilisha mada kuhusu Mfumo wa e-Mrejesho wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Watumishi wa ofisi hiyo jijini Dodoma.


Wakurugenzi wa Idara na Vitengo kutoka Ofisi ya Rais-UTUMISHI wakifuatilia wasilisho la mada kuhusu Mfumo wa e-Mrejesho wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Watumishi wa ofisi hiyo yaliyofanyika katika ofisi hiyo jijini Dodoma.


Wakurugenzi Wasaidizi kutoka Ofisi ya Rais-UTUMISHI wakifuatilia wasilisho la mada kuhusu Mfumo wa e-Mrejesho wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Watumishi wa ofisi hiyo ambayo hufanyika katika ofisi hiyo iliyopo Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma. Wengine ni Watumishi wa ofisi hiyo.


Sehemu ya Watumishi wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI wakifuatilia wasilisho la mada kuhusu Mfumo wa e-Mrejesho wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Watumishi wa ofisi hiyo ambayo hufanyika katika ofisi hiyo iliyopo Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.


Sehemu ya Watumishi wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI wakifuatilia wasilisho la mada kuhusu Mfumo wa e-Mrejesho wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Watumishi wa ofisi hiyo ambayo hufanyika katika ofisi hiyo iliyopo Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.


 

 



 

Thursday, February 12, 2026

ZINGATIENI MAADILI YA UTENDAJI, DHAMANA YENU NI KUBWA KWA MASILAHI MAPANA YA TAIFA” - Waziri Kikwete awaambia Watunza Kumbukumbuku

Na Antonia Mbwambo-Njombe

Tarehe 12  Februari, 2026

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete amewataka wanataaluma ya Menejimenti ya Taarifa, Kumbukumbu na Nyaraka kuzingatia maadili ya utendaji kazi kutokana na dhamana kubwa waliyonayo kwa maslahi mapana ya Taifa.

 Mhe. Kikwete ameyasema hayo leo tarehe 12, Februari, 2026 alipokuwa akifunga kikao kazi cha mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji wanataaluma ya Menejimenti ya Taarifa, Kumbukumbu na Nyaraka mkoani Njombe.

“Tambueni dhamana yenu ni kubwa sana kwa maslahi ya Taifa letu. Ni vizuri utaalamu wenu uzingatie maadili ya utendaji kazi ili kuepuka kuvuja kwa siri na kuepusha madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na siri kuvuja,” amesisitiza Mhe. Kikwete.

 Amesema kaulimbiu ya kikao kazi hicho isemayo “Kumbukumbu Sahihi leo, Maamuzi Sahihi kesho; Tunza siri kwa heshima ya Taifa” inaakisi kikamilifu mwelekeo wa Serikali katika kusimamia rasilimaliwatu na mifumo ya utendaji kazi na umuhimu wa kutunza siri kwa heshima ya Taifa. Na kuongeza kuwa hilo halina ubishi kwamba siri za nchi hii zinatakiwa kulindwa kwa wivu mkubwa. Hivyo, wataalamu wa kada hiyo wanalo jukumu kubwa la kuhakikisha kwa namna yoyote ile mtu yoyote haruhusiwi kuikanyaga taaluma hiyo wala kuvujisha siri.

Mhe. Kikwete amesema Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ndio msimamizi wa Chama cha Wanataaluma hao (TRAMPA), hivyo itaendelea kuhakikisha Nyaraka za serikali zinabaki salama kwa kuendelea kutoa miongozo mbalimbali pamoja na kusimamia utekelezaji wake.

Amewapongeza waajiri waliotenga bajeti na kuwaruhusu watumishi wao kushiriki kikao kazi hicho huku akimuagiza Katibu Mkuu-UTUMISHI kuwaandikia barua waajiri wote serikalini kutenga bajeti ya ushiriki wa watumishi walio chini yao kwani vikao hivyo ni muhimu katika kukua kitaaluma.

Aidha, amesema Serikali itaendelea kushirikiana na TRAMPA katika kutekeleza majukumu yake ya kitaaluma na kiutumishi ikiwemo kuhamasisha matumizi ya mifumo ya kidijitali katika usimamizi wa Kumbukumbu na Nyaraka, hususani katika Ofisi za Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, ili kuongeza ufanisi, usalama wa taarifa,Uwajibikaji  na upatikanaji wa kumbukumbu kwa wakati.

“Kwenye hili Mkurugenzi wa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa ninakuagiza kushirikiana na TRAMPA kuzitambua na kuziorodhosha halmashauri ambazo zinazorota katika kukamilisha hili ili ziweze kupewa msukumo kwa maandishi,” ameongeza Waziri Kikwete.

Akizungumza kabla ya kumkaribisha Waziri Kikwete kuhitimisha kikao kazi cha wanataaluma hao, Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Antony Mtaka alimshukuru Mhe. Kikwete kwa kuwapa heshima wanataaluma hao na wenyeji wa Mkoa wa Njombe kwa kufika mwenyewe kuhitimisha kikao kazi hicho.

Mhe. Mtaka amewaasa watumishi hao kuthamini kazi walizo nazo kwa kutekeleza majukumu yao kwa bidii, nidhamu na uadilifu kwani watu wengi wanatafuta kazi usiku na machana lakini hawapati.

Naye Mwenyekiti wa TRAMPA, Bi. Devotha Mrope amesema mada mbalimbali zimewasilishwa katika kikao kazi hicho ili kuwajengea uwezo wa kiutendaji wanataaluma hao.

Amesema takribani wanataaluma wa Menejimenti ya Taarifa, Kumbukumbu na Nyaraka 1900 wameshiriki kikao kazi hicho cha siku 4


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akizungumza na Wanataaluma ya Menejimenti ya Taarifa, Kumbukumbu na Nyaraka (hawapo pichani) wakati alipokuwa akifunga kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wanataaluma hao leo tarehe 12 Februari, 2026 Mjini Njombe.


Wanataaluma ya Menejimenti ya Taarifa, Kumbukumbu na Nyaraka wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (hayupo pichani) walipokuwa katika kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Mjini Njombe leo tarehe12 Februari, 2026


Mwenyekiti wa chama cha TRAMPA Bi. Devotha Mrope akitoa taarifa fupi ya kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wanataaluma ya Menejimenti ya Taarifa, Kumbukumbu na Nyaraka (hawapo pichani) kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (hayupo pichani) kabla ya Waziri huyo kufunga kikao hicho leo tarehe 12 Februari, 2026 Mini Njombe.

Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Antony Mtaka akitoa neno la shukrani kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete kufunga kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wanataaluma hao leo tarehe 12 Februari, 2026 Mini Njombe.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na Kamati ya Usalama ya mkoa wa Njombe baada ya waziri huyo kufunga kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wanataaluma hao leo tarehe 12 Februari, 2026 Mini Njombe.


Wanataaluma ya Menejimenti ya Taarifa, Kumbukumbu na Nyaraka wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (hayupo pichani) walipokuwa katika kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Mjini Njombe leo tarehe12 Februari, 2026


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (kulia) akiteta jambo na Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Mhe. Antony Mtaka (kushoto) wakati waziri huyo akifunga kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wanataaluma hao leo tarehe 12 Februari, 2026 Mini Njombe

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akisaini Kitabu cha wageni baada ya kuwasili katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Njombe alipokuwa akifunga kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wanataaluma hao leo tarehe 12 Februari, 2026 Mjini Njombe.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Ofisi ya Rais –UTUMISHI baada ya waziri huyo kufunga kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wanataaluma hao leo tarehe 12 Februari, 2026 Mjini Njombe.

Mtunza kumbukumbu na Nyaraka kutoka Halmashauri ya Mkoa wa Njombe, Bw. Dotto Nyerere akipokea zawadi ya Mfanyakazi Bora katika taaluma hiyo kutoka kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete, baada ya Waziri huyo kufunga kikao kazi cha Mafunzo maalum ya kuwajengea uwezo wa kiutendaji Wanataaluma hao leo tarehe 12 Februari, 2026 Mjini Njombe.