Saturday, September 5, 2026

UTUMISHI SC YASHINDA 4-0 DHIDI YA MKONZE VETERANS

Na Eric Amani, Dodoma

Timu ya Utumishi Sports Club (UTUMISHI SC) imeendelea kuonyesha kiwango kizuri baada ya kupata ushindi mnono wa mabao 4-0 dhidi ya Mkonze Veterans katika mchezo wa kirafiki wa soka uliochezwa leo Septemba 05, 2026 katika uwanja wa John Merlin Jijini Dodoma.

UTUMISHI SC ilitawala mchezo kwa kiasi kikubwa, ikionyesha umakini, nidhamu na ushirikiano mzuri wa kikosi katika maeneo yote ya uwanja. Ushindi huo unaongeza morali kwa timu huku ukiendelea kujenga maandalizi na ushindani kuelekea mashindano ya SHIMIWI 2026 Mkoani Kilimanjaro.

Uongozi na wachezaji wa UTUMISHI SC wameendelea kuhimizana kuzingatia maadili ya Utumishi wa Umma ndani na nje ya Viwanja kuwa nidhamu, upendo, mshikamano na kujituma katika kila mchezo, kwa lengo la kuiweka timu katika kiwango bora zaidi ili kuelekea kutetea ubingwa walioutwaa katika mashindano ya SHIMIWI kwa mwaka 2025 ambayo yalifanyika Jijini Mwanza

 










Friday, September 4, 2026

MKURUGENZI FELISTER SHULI AONGOZA MAFUNZO YA MAADILI KWA WANAMICHEZO WA UTUMISHI

Na Eric Amani, Dodoma

Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Maadali, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Bi. Felister Shuli, Leo Septemba 4, 2026 katika Ukumbi wa Sekretariet ya Ajira ameongoza mafunzo ya maadili kwa wanamichezo wa Ofisi hiyo, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuhakikisha wanamichezo wanaoshiriki mashindano kuzingatia misingi ya uadilifu, nidhamu, heshima na weledi.

Mafunzo hayo yamejikita katika kuwaelimisha wanamichezo kuhusu umuhimu wa kuzingatia maadili ya Utumishi wa Umma, sheria, taratibu na kanuni zinazoongoza utendaji wa mtumishi wa umma wakati wa mashindano ya SHIMIWI 2026 na Mengine.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Mkurugenzi Shuli amewataka wanamichezo hao kutambua kuwa wanaposhiriki katika mashindano, wanabeba taswira ya Ofisi ya Rais – Utumishi na hivyo wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa katika nidhamu, mwenendo na matumizi sahihi ya lugha na vitendo.

Mnapokuwa uwanjani, siyo tu mnashindana kama wanamichezo, bali pia mnawakilisha taasisi yenu na Utumishi wa Umma kwa ujumla. Hivyo, kila mmoja anapaswa kuhakikisha mwenendo wake unaendelea kulinda heshima na taswira ya Ofisi,” amesisitiza.

Aidha, amewahimiza wanamichezo hao kutumia mafunzo hayo kama sehemu ya kujijenga katika maisha ya kila siku, kwa kuzingatia misingi ya uwajibikaji, kuheshimu viongozi, waamuzi, wapinzani na wenzao, pamoja na kuepuka vitendo vinavyoweza kuathiri taswira ya taasisi.

Kwa upande wao, wanamichezo walipata fursa ya kuuliza maswali na kupata ufafanuzi kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu maadili, nidhamu na wajibu wao kama watumishi wa umma wanaoshiriki michezo.

Mafunzo hayo ni sehemu ya jitihada za Ofisi ya Rais – Utumishi katika kuimarisha uelewa wa watumishi kuhusu maadili ya Utumishi wa Umma, huku michezo ikiendelea kutumika kama nyenzo ya kujenga afya, mshikamano, ushirikiano na kuongeza tija mahali pa kazi.









Thursday, September 3, 2026

TIMU YA MPIRA WA PETE UTUMISHI YAENDELEA KUIMARIKA, YAICHAPA DOM KINGS 68–42

 Na Eric Amani, Dodoma

Timu ya Mpira wa Pete ya Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imeendelea kuonyesha kiwango kizuri na kuimarika kuelekea mashindano ya SHIMIWI 2026, baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 68–42 dhidi ya timu ya Dom Kings katika mchezo wa mazoezi uliofanyika Agosti 2, 2026 jijini Dodoma.

Katika mchezo huo, Utumishi ilionesha uwezo mzuri wa kiufundi, kasi, umakini na ushirikiano wa wachezaji, hali iliyoiwezesha kutawala mchezo na kupata ushindi wa mabao 68, huku Dom Kings ikiambulia mabao 42.

Mchezo huo ni sehemu ya maandalizi ya timu hiyo kuelekea Mashindano ya Michezo ya Wizara, Idara za Serikali na Mikoa (SHIMIWI) 2026, yanayotarajiwa kufanyika mkoani Kilimanjaro. Maandalizi ya mashindano hayo yameendelea kushika kasi, huku taasisi mbalimbali za Serikali zikiendelea kuimarisha timu zao kupitia mazoezi na michezo ya kirafiki.

Ushindi dhidi ya Dom Kings unaongeza morali kwa kikosi cha Utumishi na kutoa fursa kwa benchi la ufundi kuendelea kutathmini uwezo wa wachezaji, kubaini maeneo yanayohitaji maboresho na kujenga muunganiko bora wa timu kabla ya kuingia kwenye ushindani wa SHIMIWI 2026.

Kwa upande wa wachezaji, ushindi huo umeonesha dhamira yao ya kufanya vizuri katika mashindano hayo, huku wakisisitiza umuhimu wa kuendelea na mazoezi, nidhamu na mshikamano ili kuhakikisha timu inakuwa tayari kwa ushindani mkubwa.