Saturday, March 16, 2024

KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UTAWALA, KATIBA NA SHERIA YAIPONGEZA OFISI YA RAIS-UTUMISHI KWA KUJENGA MIFUMO YA TEHAMA


Na. Veronica Mwafisi-Dodoma

Tarehe 16 Machi, 2024

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Joseph Mhagama ameipongeza Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kubuni mifumo mbalimbali ya TEHAMA kwa lengo la kuboresha utendaji kazi serikalini.

Dkt. Mhagama amesema hayo leo Machi 16, 2024 Jijini Dodoma wakati Kamati hiyo ilipotembelea Ofisi ya Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Sekretarieti ya Ajira na Tume ya Utumishi wa Umma kwa lengo la kupokea taarifa ya miradi mbalimbali inayotekelezwa na taasisi hizo. 

Aidha, kwa niaba ya Kamati, Dkt. Mhagama ameipongeza Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kupitia taasisi zake kwa kufanya kazi kubwa ya kubuni na kusanifu mifumo ambayo ni muhimu na yenye lengo la kuongeza ufanisi wa utendaji kazi Serikalini.

“Tulizoea kuona nchi za wenzetu zikibuni na kusanifu mifumo mahususi ya TEHAMA kwa maendeleo ya mataifa yao na wakati mwingine kutuuzia na sisi lakini leo tumesikia na kuona kwa macho yetu uwezo mkubwa wa vijana wetu wa ndani ya Serikali ambao wameunda mifumo muhimu kwa ajili ya Serikali yetu, hakika haya ni mapinduzi makubwa yatakayoleta ufanisi unaozingatia haki na wajibu Serikalini” alisema Dkt. Mhagama.

Kadhalika Dkt. Mhagama ameisisitiza Ofisi ya Rais-UTUMISHI kuhakikisha mifumo yote ya TEHAMA iliyopo na inayoendelea kubuniwa na kusanifiwa inakuwa endelevu ili kuboresha utoaji wa huduma kwa umma kwa njia ya TEHAMA.

Kwa upande wake Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete ameishukuru Kamati hiyo kwa kupanga ziara hiyo muhimu na kutoa maelekezo ambayo yatafanyiwa kazi kwa haraka na kutoa mrejesho.

Mhe. Kikwete ameongeza kuwa mifumo yote ikiwemo HCMIS, PEPMIS HR Assessment na mifumo mingine inatumika kwa ufanisi ili kutatua changamoto mbalimbali za kiutumishi kwa wakati.


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Joseph Mhagama akizungumza na Viongozi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na Watendaji wa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Sekretarieti ya Ajira na Tume ya Utumishi wa Umma wakati wa ziara ya kamati hiyo iliyolenga kupokea taarifa za Miradi inayotekelezwa na taasisi hizo, jijini Dodoma.



Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete akitoa neno la shukrani kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria wakati wa ziara ya kamati hiyo katika Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Sekretarieti ya Ajira na Tume ya Utumishi iliyolenga kupokea taarifa ya Miradi ya taasisi hizo jijini Dodoma.


Mkurugenzi wa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Bw. Firimin Msiangi (kushoto) na Katibu wa Tume ya Utumishi, Bw. Mathew Kirama (kulia) wakimsikiliza Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria Mhe. Dkt. Joseph Mhagama wakati Kamati hiyo ilipofanya ziara ya kikazi ya kupokea taarifa ya Miradi ya Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Sekretarieti ya Ajira na Tume ya Utumishi iliyofanyika jijini Dodoma.


Kaimu Katibu wa Sekretarieti ya Ajira katika utumishi wa Umma Bw. Innocent Bomani akifafanua jambo kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo iliyolenga kupokea taarifa ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya taasisi hiyo jijini Dodoma.


Mkurugenzi wa Idara ya TEHAMA Serikalini, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Priscus Kiwango akiwasilisha taarifa za mfumo wa HCMIS kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo katika Ofisi ya Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Sekretarieti ya Ajira na Tume ya Utumishi jijini Dodoma.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete (Wa kwanza kushoto) akijadili jambo na Watendaji wa Ofisi yake kabla ya kupokea msafara wa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria katika Ofisi za Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa Jijini Dodoma.

 


 

Thursday, March 14, 2024

TASAF YAJENGA SOKO LA KISASA - MADABA

 Na. Veronica Mwafisi – MADABA, RUVUMA

Tarehe 14 Machi, 2024

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais Menejimeti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete amewapongeza wananchi wa kijiji  cha Lituta katika halmashauri ya Wilaya Madaba mkoa wa Ruvuma kwa kutoa ushirikiano hadi kujengewa Soko la Kisasa.

Mhe. Kikwete amesema kuwa mradi huo wa soko la kisasa uliombwa na wananchi wa Madaba kupitia kwa Mbunge wa Jimbo hilo Mhe Dkt. Joseph Mhagama ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria. 

“Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Ofisi ya Rais UTUMISHI na Utawala Bora alipokea maombi yenu na akaridhia fedha zitengwe na hatimaye kupitishwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria na Bunge kwa jumla ili kuondoa changamoto ya soko katika Kijiji cha Lituta” ameongeza Mhe. Kikwete

Aidha, ujenzi wa Soko hili ni moja ya jitihada mahususi za Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuwatoa wananchi katika wimbi la umaskini kwa kuwa wananchi watafanya biashara katika maeneo safi na wateja wataongezeka, hivyo kuinua uchumi wa wanamadaba.

Pia, amebainisha kuwa awali soko lilikuwa na hadhi ya chini na sasa wananchi wamepata visimba vya hali nzuri. Soko la awali lilikuwa  na vizimba 34 wakati la sasa lina vizimba 80. Usanifu na ujenzi umezingatia mahitaji ya sasa na ya baadae.

Hali kadhalika, Mhe. Dkt. Mhagama amewapongeza viongozi na watendaji wa Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kuisimamia vizuri TASAF na kuhakikisha jitihada kubwa zinazofanywa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan za kutafuta fedha na kuhudumia wananchi wake zinafanyika kwa ufanisi.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akizungumza na wananchi na walengwa wa TASAF wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria iliyolenga kukagua utekelezaji wa mradi wa soko, vyoo na vizimba katika Kijiji cha Lituta, Halmashauri ya Wilaya ya Madaba mkoani Songea.


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Joseph Mhagama akisalimiana na wananchi na walengwa wa TASAF wakati wa ziara ya kamati yake iliyolenga kukagua utekelezaji wa mradi ya TASAF wa soko, vyoo na vizimba katika Kijiji cha Lituta, Halmashauri ya Wilaya ya Madaba mkoani Songea.

Baadhi ya wananchi na walengwa wa TASAF wakimsikiliza Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Joseph Mhagama wakati akizungumza nao alipokuwa kwenye ziara ya kamati yake iliyolenga kukagua utekelezaji wa mradi wa soko, vyoo na vizimba katika Kijiji cha Lituta, Halmashauri ya Wilaya ya Madaba mkoani Songea.

Sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, wakimsikiliza Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Dkt. Joseph Mhagama (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza na walengwa wa TASAF na wananchi wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa mradi wa soko, vyoo na vizimba katika Kijiji cha Lituta, Halmashauri ya Wilaya ya Madaba mkoani Songea.


Muonekano wa Soko linalojengwa kupitia utekelezaji wa mradi wa TASAF katika Kijiji cha Lituta, Halmashauri ya Wilaya ya Madaba mkoani Songea.




 


 





TASAF YAPONGEZWA KWA UJENZI WA STENDI YA KISASA SONGEA

 Na. Veronica Mwafisi – Peramiho, Songea

Tarehe 14 Machi, 2024

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Joseph Mhagama kwa niaba ya Wajumbe wa kamati hiyo amefurahishwa na utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa stendi ya kisasa ya mabasi kwa fedha kidogo.

Mhe. Dkt. Mhagama ameyasema hayo tarehe 14 Machi, 2024 katika Kijiji cha Lundusi kata ya Peramiho katika halmashauri ya Wilaya ya Songea wakati wa ziara ya kamati hiyo ya kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya Serikali.

“Nikiangalia nyuso za wanakamati zinanipa ishara ya kuwa wameridhika na utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa stendi ya kisasa ya mabasi kwa kuwa unapofika katika eneo la mradi huu unaanza kuona moja kwa moja thamani ya fedha ya umma” amesema Mhe. Dkt. Mhagama.

Aidha, Mhe. Dkt. Mhagama amewapongeza viongozi na watendaji wa Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kuisimamia vizuri TASAF na kuhakikisha jitihada kubwa zinazofanywa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan za kutafuta fedha na kuhudumia wananchi wake zinafanyika kwa ufanisi.

Naye, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais Menejimeti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete ameieleza na kuihakikishia Kamati hiyo kuwa hakuna kitu kitakachopungua katika mradi na atahakikisha TASAF inasimamiwa ipasavyo hadi kukamilika kwa mradi huo.

Mhe. Kikwete afafanua kuwa mradi huo wa  kisasa wa stendi ya mabasi uliibuliwa na wananchi wenyewe wa Kijiji cha Lundusi mwaka 2022 kupitia mkutano wao halali wa jamii ambapo walimuomba fedha Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia TASAF waweze kujengewa stendi hiyo.

“Mheshimiwa Mwenyekiti kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene  tunashukuru Kamati yako kwa kupitisha maombi ya bajeti ya ujenzi wa stendi hiyo na huu ndio utekelezaji wa bajeti hiyo. Mradi huu utaongeza uchumi na kipato kwa Wanaperamiho na Songea kwa jumla” aliongeza Mhe. Kikwete.

Hadi kukamilika kwa mradi huu, kituo cha mabasi kitakuwa na maduka 36, vibanda vya walizi, kituo cha polisi, matundu 8 ya vyoo na uzio.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Joseph Mhagama akizungumza na walengwa wa TASAF na wananchi waliofika kuona maendeleo ya ujenzi wa jengo la stendi ya mabasi Peramiho-Lundusi ambalo litatumika mara baada ya kukamilika.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (kulia) akitazama nyaraka inayoelezea maendeleo ya ujenzi wa stendi ya mabasi Peramiho-Lundusi. Katikati ni Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Bw. Shedrack Mziray.


Baadhi ya watumishi wa Halmashauri ya Songea wakimsikiliza Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Joseph Mhagama (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza nao wakati wa ziara ya kikazi ya kamati yake iliyolenga kukagua ujenzi wa stendi ya mabasi Peramiho-Lundusi kupitia mradi wa TASAF.


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Joseph Mhagama na wajumbe wa kamati hiyo wakitoka kukagua ujenzi wa stendi ya mabasi Peramiho-Lundusi wakati kamati hiyo ilipofanya ziara ya kikazi kwa lengo la kukagua mradi huo kupitia TASAF. Wengine ni Viongozi na Watendaji wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI na wananchi wa eneo hilo.


Sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, wakimsikiliza Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Dkt. Joseph Mhagama (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza na walengwa wa TASAF na wananchi wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo iliyolenga kukagua mradi wa ujenzi wa stendi ya mabasi Peramiho-Lundusi kupitia TASAF.


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Joseph Mhagama akiteta jambo na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete mara baada ya kamati ya Mhe. Dkt. Mhagama kukagua maendeleo ya ujenzi wa stendi ya mabasi Peramiho-Lundusi mkoani Songea inayojengwa kupitia mradi wa TASAF. 

Muonekano wa Jengo la stendi ya mabasi Peramiho Lundusi inayojengwa kupitia mradi wa TASAF mkoani Songea.