MRADI WA TANZANIA YA KIDIJITALI (DTP) UMELETA MAPINDUZI MAKUBWA YA MAWASILIANO YA KIMTANDAO YALIYORAHISISHA UTOAJI WA HUDUMA KWA UMMA
Wednesday, September 16, 2026
Tuesday, September 15, 2026
NAIBU WAZIRI MHE. QWARAY AWAAGIZA WAAJIRI KUTATUA CHANGAMOTO ZA WATUMISHI KWA WAKATI
Na. Antonia Mbwambo na Lusungu
Helela
Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti
ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray, amewaagiza
waajiri kuhakikisha changamoto na stahiki za watumishi wa umma zinashughulikiwa
kwa wakati, hatua inayolenga kuongeza ufanisi na kuimarisha utoaji wa huduma
kwa wananchi.
Mhe. Qwaray ametoa agizo hilo leo Septemba 15, 2026 wakati akizungumza na watumishi wa umma wa Halmashauri ya Wilaya
ya Buchosa mkoani Mwanza kwa lengo la kusikiliza changamoto za
watumishi na kujadili namna ya kuboresha utendaji katika Utumishi wa Umma.
Amesema masuala yanayohusu kupandishwa
vyeo, uhamisho, malimbikizo ya mishahara na mafao yanapaswa kushughulikiwa kwa
wakati na mamlaka husika, badala ya kuendelea kucheleweshwa.
"Nawaagiza waajiri wote kuhakikisha
changamoto na stahiki za watumishi, ikiwemo kupandishwa vyeo, uhamisho,
malimbikizo ya mishahara na mafao, zinashughulikiwa kwa wakati,” amesema
Mhe Qwaray.
Aidha, amesisitiza kuwa madai ya
watumishi yanapaswa kuhakikiwa ipasavyo na kuwasilishwa yakiwa na nyaraka zote
muhimu ili kuwezesha malipo kufanyika kwa wakati.
Katika hatua nyingine, Mhe. Qwaray
amezitaka Mamlaka za Ajira na Nidhamu kusimamia haki na wajibu wa watumishi kwa
kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu za Utumishi wa Umma, huku akiwataka
kuachana na utendaji wa mazoea.
Amesema mambo yaliyo ndani ya mamlaka za
waajiri na Mamlaka za Ajira na Nidhamu yanapaswa kushughulikiwa katika ngazi husika
badala ya kuendelea kuwasilishwa Ofisini kwake.
Aidha, Mhe. Qwaray amesisitiza umuhimu wa watumishi kutumia mifumo
ya kidijitali iliyobuniwa na Serikali katika kusimamia utendaji na kupata
huduma za kiutumishi.
Mifumo hiyo ni pamoja na e-Watumishi,
Watumishi Portal, e-Utendaji (PEPMIS) na e-Mrejesho, ambayo imeimarishwa kwa
ajili ya kurahisisha upatikanaji wa huduma, kuongeza uwajibikaji na kutoa fursa
kwa wananchi na watumishi kuwasilisha maoni, pongezi, malalamiko na
mapendekezo.
Amesema matumizi sahihi ya mifumo hiyo
ni sehemu ya jitihada za kujenga Utumishi wa Umma unaozingatia haki, wajibu,
uwajibikaji, ufanisi na matumizi ya teknolojia.
Awali Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri
ya Buchosa, Bw. Benson Mihayo amesema changamoto za watumishi zitaendelea
kushughulikiwa kutokana na bajeti iliyopo huku akibainisha kuwa mwitikio wa
watumishi katika suala ujazaji PEPMIS limekuwa
na mwitikio mkubwa ukilinganisha na hapo awali
hali inayopelekea malalamiko ya watumishi kupungua wakati wa upandaji wa
madaraja.
Naye Mbunge wa Buchosa, Mhe. Erick
Shigongo ametumia fursa hiyo kuwashukuru Watumishi wa Halmashauri ya Buchosa
kwa huduma bora wanazoendelea kutoa kwa wananchi wa Halmashauri hiyo.
" Hatua ya maendeleo unayoyaona leo
hapa Buchosa ni kutokana na uwepo wa watumishi wazalendo waliojitoa kwa lengo
la kuwahudumia wananchi" amesisitiza Mhe. Shigongo
Naibu Waziri wa Ofisi
ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray
akiwa na baadhi ya viongozi wakimsikiliza
Katibu Tawala wa wilaya hiyo Bw.
Cuthbert Midala mara baada ya kumaliza
kuzungumza leo na Watumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Buchosa iliyopo
mkoani Mwanza
Naibu Waziri wa Ofisi
ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray
akizungumza na watumishi wa Ofisi ya
Halmashauri ya Buchosa Mkoani Mwanza mara baada ya kuwasili leo
mkoani humo kwa lengo la kuzungumza na kusikiliza changamoto zinazowakabili
watumishi na kuzitafutia ufumbuzi
3. Watumishi wa Ofisi ya
Halmashauri ya Buchosa iliyopo Mkoani Mwanza wakiwa kwenye maombi kabla
ya Naibu Waziri wa Ofisi ya
Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray kuanza
kuzungumza nao
Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray akisalimiana na baadhi ya watumishi wa Ofisi ya Mkoa wa Mwanza mara baada ya kuwasili leo mkoani humo kwa lengo la kuzungumza na kusikiliza changamoto zinazowakabili watumishi na kuzitafutia ufumbuzi Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray akizungumza na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe. CP Salum Hamduni mara baada Naibu Waziri huyo kuwasili mkoani humo kwa lengo la kuzungumza na kusikiliza changamoto zinazowakabili watumishi na kuzitafutia ufumbuzi.












