Na Eric Amani, Dodoma
Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais –
Menejimenti ya Utumishi, Bw. Juma Mkomi, amewaaga na kuwatakia kila la
kheri wanamichezo wa Utumishi Sports Club (UTUMISHI SC) wanaokwenda
kuiwakilisha Ofisi katika Mashindano ya Michezo ya Wizara, Idara za Serikali na
Mikoa (SHIMIWI 2026) yanayotarajiwa kufanyika mkoani Kilimanjaro.
Akizungumza wakati wa kuwaaga
wanamichezo hao katika Ukumbi wa Ofisi hiyo iliyopo Mji wa Serikali, Mtumba Bw.
Mkomi amewataka kwenda kushindana kwa kuzingatia nidhamu, mshikamano, heshima, na
uadilifu, huku wakitambua kuwa wanapokuwa uwanjani wanawakilisha siyo tu
UTUMISHI SC, bali pia Ofisi ya Rais – Utumishi.
“Nawatakia kila la kheri katika
mashindano haya. Nendeni mkaiwakilishe Ofisi yetu kwa vizuri. Ushindi ni
muhimu, lakini zaidi ya yote tunataka kuona mnakuwa mabalozi wazuri wa Utumishi
wa Umma,” amesema Bw. Mkomi.
Aidha, amewapongeza wanamichezo na
viongozi wa UTUMISHI SC kwa juhudi na maandalizi waliyofanya kuelekea
mashindano hayo. UTUMISHI SC imeendelea kufanya maandalizi kupitia michezo ya
kirafiki, ikiwemo ushindi wa mabao 4–0 dhidi ya Mkonze Veterans katika mchezo
uliofanyika Septemba 5, 2026 jijini Dodoma.
UTUMISHI SC inaingia katika
mashindano hayo ikiwa na dhamira ya kufanya vizuri, baada ya kutwaa ubingwa wa
SHIMIWI mwaka 2025 yaliyofanyika jijini Mwanza.
![]() |
| Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bw. Juma Mkomi, akiwaaga na kuwatakia kila la kheri wanamichezo wa Utumishi Sports Club |
![]() |
| Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Prisca Lwangili, akiwaaga na kuwatakia kila la kheri wanamichezo wa Utumishi Sports Club |
![]() |
Baadhi ya wanamichezo wa Utumishi
SC wakimsikiliza Katibu Mkuu Bw. Juma Mkomi (Hayupo pichani) wakati wanamichezo
hao wakiagwa na kutakiwa kila la Kheri kwenye ushiriki wa mashindano ya SHIMIWI
2026 |
![]() |
Picha ya pamoja ya wanamichezo wa mchezo
wa Soka kutoka Ofisi ya Rais – UTUMISHI wakati wa kuwaaga kuelekea mashindano
ya SHIMIWI 2026 Mkoani Kilimanjaro |
![]() |
Picha ya pamoja ya Uongozi wa
UTUMISHI SC wakiwa na Katibu Mkuu Bw. Juma Mkomi Ofisi ya Rais – UTUMISHI wakati
wa kuwaaga kuelekea mashindano ya SHIMIWI 2026 Mkoani Kilimanjaro |
![]() |
Picha ya pamoja ya wanamichezo wa michezo
ya Jadi kutokea Ofisi ya Rais - UTUMISHI |



















