Monday, September 7, 2026

SERIKALI YASISITIZA UZINGATIAJI WA SHERIA KATIKA UTUMISHI WA UMMA

 Na. Mwandishi wetu-Dodoma

Tarehe7 Septemba, 2026

Serikali imesisitiza umuhimu wa watumishi wa umma kuzingatia Sheria, Sera, Kanuni, Taratibu, Miongozo na Maadili ya Utumishi wa Umma ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Hayo yamesemwa leo Septemba 7, 2026 jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (Mb), alipotembelea Bodi ya Usajili wa Wahandisi kukagua utekelezaji wa zoezi la Ukaguzi wa Uzingatiaji wa Sheria katika Usimamizi wa Utumishi wa Umma kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Mhe. Qwaray amesema ukaguzi huo unaofanywa na Tume ya Utumishi wa Umma ni muhimu kwa Serikali kupata taarifa kuhusu hali ya uzingatiaji wa sheria katika usimamizi wa masuala ya kiutumishi, pamoja na kubaini maeneo yanayohitaji maboresho ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na kwa wakati.

Amesema taarifa zinazotokana na ukaguzi huo huisaidia Serikali kufanya maamuzi na kupanga mipango ya rasilimali watu kwa kuzingatia ushahidi, huku pia zikitoa mrejesho kuhusu utekelezaji wa Sera, Sheria, Kanuni na Taratibu za Utumishi wa Umma na kusaidia kuweka ulinganifu katika tafsiri na utekelezaji wake.

Aidha, ameipongeza Tume ya Utumishi wa Umma kwa kuanzisha Mfumo wa Kielektroniki wa Ukaguzi wa Uzingatiaji wa Sheria katika Usimamizi wa Utumishi wa Umma, akieleza kuwa matumizi ya mfumo huo yanaendana na jitihada za Serikali za kutumia TEHAMA katika kuboresha utendaji na usimamizi wa shughuli za Serikali.

Ameeleza kuwa Serikali imeendelea kujenga mifumo mbalimbali ikiwemo e-Watumishi na e-Utendaji kwa lengo la kuongeza ufanisi katika usimamizi wa watumishi wa umma.

Katika hatua nyingine, Mhe. Qwaray amewataka watumishi na wasimamizi kuzingatia maelekezo ya utekelezaji wa PEPMIS, akibainisha kuwa changamoto ya baadhi ya watumishi kushindwa kufikia asilimia 75 zinazohitajika katika mchakato wa kupandishwa vyeo inaweza kuchangiwa na kutokuzingatiwa ipasavyo kwa majukumu na taratibu za mfumo huo.

Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Regina Qwaray (Mb), akizungumza na Watumishi wa Bodi ya Usajili wa Wahandisi (ERB) (hawapo pichani), mara baada ya Naibu Waziri huyo kuwasili katika zoezi la Ukaguzi wa Uzingatiaji wa Sheria katika Usimamizi wa Utumishi wa Umma leo Septemba 7, 2026 jijini Dodoma

Washiriki kutoka Bodi ya Usajili wa Wahandisi na Tume ya Utumishi wa Umma wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakati Naibu Waziri huyo alipotembele Bodi hiyo kukagua zoezi la Ukaguzi wa Uzingatiaji wa Sheria katika Utumishi wa Umma Jijini Dodoma

Washiriki kutoka Bodi ya Usajili wa Wahandisi na Tume ya Utumishi wa Umma wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakati Naibu Waziri huyo alipotembele Bodi hiyo kukagua zoezi la Ukaguzi wa Uzingatiaji wa Sheria katika Utumishi wa Umma Jijini Dodoma

Baadhi ya Viongozi na Watumishi kutoka Bodi ya Usajili wa Wahandisi (ERB) wakimsikiliza Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Regina Qwaray (hayupo pichani) wakati Naibu Waziri huyo alipokuwa akizungumza nao mara baada ya kupitishwa na kuona namna mfumo wa Kielektroniki wa Ukaguzi wa Uzingatiaji wa Sheria katika Usimamizi wa Utumishi wa Umma unavyofanya kazi leo Septemba 7, 2026 jijini Dodoma.

Watumishi kutoka Bodi ya Usajili wa Wahandisi (ERB) wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakati Naibu Waziri huyo alipotembelea Bodi hiyo kuona zoezi la Ukaguzi wa Uzingatiaji wa Sheria katika Utumishi wa Umma linavyoendeshwa Jijini Dodoma

Watumishi kutoka Bodi ya Usajili wa Wahandisi (ERB) wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakati Naibu Waziri huyo alipotembelea Bodi hiyo kuona zoezi la Ukaguzi wa Uzingatiaji wa Sheria katika Utumishi wa Umma linavyoendeshwa Jijini Dodoma

Watumishi kutoka Bodi ya Usajili wa Wahandisi (ERB) wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakati Naibu Waziri huyo alipotembelea Bodi hiyo kuona zoezi la Ukaguzi wa Uzingatiaji wa Sheria katika Utumishi wa Umma linavyoendeshwa Jijini Dodoma

Mtumishi kutoka Tume ya Utumishi wa Umma akifafanua jambo kuhusu Mfumo wa Ukaguzi wa Uzingatiaji wa Sheria katika Usimamizi wa Utumishi wa Umma unavyofanya kazi mara baada ya Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Regina Qwaray kuwasili katika Bodi ya Usajili wa Wahandisi kuoa (ERB) kuona zoezi hilo leo Septemba 7, 2026 jijini Dodoma.


Saturday, September 5, 2026

UTUMISHI SC YASHINDA 4-0 DHIDI YA MKONZE VETERANS

Na Eric Amani, Dodoma

Timu ya Utumishi Sports Club (UTUMISHI SC) imeendelea kuonyesha kiwango kizuri baada ya kupata ushindi mnono wa mabao 4-0 dhidi ya Mkonze Veterans katika mchezo wa kirafiki wa soka uliochezwa leo Septemba 05, 2026 katika uwanja wa John Merlin Jijini Dodoma.

UTUMISHI SC ilitawala mchezo kwa kiasi kikubwa, ikionyesha umakini, nidhamu na ushirikiano mzuri wa kikosi katika maeneo yote ya uwanja. Ushindi huo unaongeza morali kwa timu huku ukiendelea kujenga maandalizi na ushindani kuelekea mashindano ya SHIMIWI 2026 Mkoani Kilimanjaro.

Uongozi na wachezaji wa UTUMISHI SC wameendelea kuhimizana kuzingatia maadili ya Utumishi wa Umma ndani na nje ya Viwanja kuwa nidhamu, upendo, mshikamano na kujituma katika kila mchezo, kwa lengo la kuiweka timu katika kiwango bora zaidi ili kuelekea kutetea ubingwa walioutwaa katika mashindano ya SHIMIWI kwa mwaka 2025 ambayo yalifanyika Jijini Mwanza

 










Friday, September 4, 2026

MKURUGENZI FELISTER SHULI AONGOZA MAFUNZO YA MAADILI KWA WANAMICHEZO WA UTUMISHI

Na Eric Amani, Dodoma

Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Maadali, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Bi. Felister Shuli, Leo Septemba 4, 2026 katika Ukumbi wa Sekretariet ya Ajira ameongoza mafunzo ya maadili kwa wanamichezo wa Ofisi hiyo, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuhakikisha wanamichezo wanaoshiriki mashindano kuzingatia misingi ya uadilifu, nidhamu, heshima na weledi.

Mafunzo hayo yamejikita katika kuwaelimisha wanamichezo kuhusu umuhimu wa kuzingatia maadili ya Utumishi wa Umma, sheria, taratibu na kanuni zinazoongoza utendaji wa mtumishi wa umma wakati wa mashindano ya SHIMIWI 2026 na Mengine.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Mkurugenzi Shuli amewataka wanamichezo hao kutambua kuwa wanaposhiriki katika mashindano, wanabeba taswira ya Ofisi ya Rais – Utumishi na hivyo wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa katika nidhamu, mwenendo na matumizi sahihi ya lugha na vitendo.

Mnapokuwa uwanjani, siyo tu mnashindana kama wanamichezo, bali pia mnawakilisha taasisi yenu na Utumishi wa Umma kwa ujumla. Hivyo, kila mmoja anapaswa kuhakikisha mwenendo wake unaendelea kulinda heshima na taswira ya Ofisi,” amesisitiza.

Aidha, amewahimiza wanamichezo hao kutumia mafunzo hayo kama sehemu ya kujijenga katika maisha ya kila siku, kwa kuzingatia misingi ya uwajibikaji, kuheshimu viongozi, waamuzi, wapinzani na wenzao, pamoja na kuepuka vitendo vinavyoweza kuathiri taswira ya taasisi.

Kwa upande wao, wanamichezo walipata fursa ya kuuliza maswali na kupata ufafanuzi kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu maadili, nidhamu na wajibu wao kama watumishi wa umma wanaoshiriki michezo.

Mafunzo hayo ni sehemu ya jitihada za Ofisi ya Rais – Utumishi katika kuimarisha uelewa wa watumishi kuhusu maadili ya Utumishi wa Umma, huku michezo ikiendelea kutumika kama nyenzo ya kujenga afya, mshikamano, ushirikiano na kuongeza tija mahali pa kazi.