Thursday, September 3, 2026

TIMU YA MPIRA WA PETE UTUMISHI YAENDELEA KUIMARIKA, YAICHAPA DOM KINGS 68–42

 Na Eric Amani, Dodoma

Timu ya Mpira wa Pete ya Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imeendelea kuonyesha kiwango kizuri na kuimarika kuelekea mashindano ya SHIMIWI 2026, baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 68–42 dhidi ya timu ya Dom Kings katika mchezo wa mazoezi uliofanyika Agosti 2, 2026 jijini Dodoma.

Katika mchezo huo, Utumishi ilionesha uwezo mzuri wa kiufundi, kasi, umakini na ushirikiano wa wachezaji, hali iliyoiwezesha kutawala mchezo na kupata ushindi wa mabao 68, huku Dom Kings ikiambulia mabao 42.

Mchezo huo ni sehemu ya maandalizi ya timu hiyo kuelekea Mashindano ya Michezo ya Wizara, Idara za Serikali na Mikoa (SHIMIWI) 2026, yanayotarajiwa kufanyika mkoani Kilimanjaro. Maandalizi ya mashindano hayo yameendelea kushika kasi, huku taasisi mbalimbali za Serikali zikiendelea kuimarisha timu zao kupitia mazoezi na michezo ya kirafiki.

Ushindi dhidi ya Dom Kings unaongeza morali kwa kikosi cha Utumishi na kutoa fursa kwa benchi la ufundi kuendelea kutathmini uwezo wa wachezaji, kubaini maeneo yanayohitaji maboresho na kujenga muunganiko bora wa timu kabla ya kuingia kwenye ushindani wa SHIMIWI 2026.

Kwa upande wa wachezaji, ushindi huo umeonesha dhamira yao ya kufanya vizuri katika mashindano hayo, huku wakisisitiza umuhimu wa kuendelea na mazoezi, nidhamu na mshikamano ili kuhakikisha timu inakuwa tayari kwa ushindani mkubwa.









Wednesday, September 2, 2026

SERIKALI KUWEKA MUUNDO MAALUM WA UTUMISHI KWA WATAALAMU WA AFYA WENYE UBOBEZI

Naibu Waziri Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Regina Qwaray amesema Miundo ya Maendeleo ya Utumishi huandaliwa kwa kuzingatia mahitaji ya kiutumishi, majukumu ya kada, pamoja na viwango vya elimu na sifa za kitaaluma vinavyotolewa na taasisi za elimu zilizoidhinishwa.

Mhe. Qwaray amebainisha hayo leo Septemba Mosi 2026 Bungeni Jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Mbulu Vijijini Mhe. Dkt. Emmanuel Qambaji Nuwas, lililouliza Serikali ina mpango gani wa kutambua kwenye Muundo wa Utumishi wa Umma Wataalam wa Kada ya Afya wenye Elimu ngazi ya ubobezi.

Akijibu swali hilo, amesema Ofisi ya Rais Utumishi, ilipokea mapendekezo ya Muundo wa Utumishi kwa Wataalamu wa Kada ya Afya wenye Elimu ngazi ya ubobezi na taratibu kwa ajili ya uchambuzi wa kina na hatua za kupata idhini zinaendelea.



TAALUMA YA UDEREVA KUWA NA STAHA, HADHI NA HESHIMA

Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha taaluma na kazi ya Udereva nchini kwa lengo la kuhakikisha inakuwa na staha, hadhi na heshima sawa na kada nyingine katika Utumishi wa Umma.

Akijibu Swali Na. 59 lililoulizwa Bungeni jijini Dodoma na Mbunge wa Mlalo, Mhe. Rashid Abdallah Shangazi, kuhusu mkakati wa Serikali wa kuhakikisha taaluma na kazi ya udereva inakuwa na staha, hadhi na heshima, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Regina Qwaray amesema Serikali inaendelea kuchukua hatua za kimkakati katika eneo hilo.

Amesema miongoni mwa hatua hizo ni kuboresha Muundo wa Maendeleo ya Utumishi wa Kada ya Udereva, hatua inayolenga kuimarisha nafasi na maendeleo ya watumishi katika kada hiyo pamoja na kuweka mazingira yanayowezesha utekelezaji wa majukumu yao kwa ufanisi.

“Serikali imeendelea kuboresha mafunzo ya kitaaluma na viwango vya elimu kwa kada ya udereva ili kuwawezesha watumishi kuwa na ujuzi na weledi unaoendana na mahitaji ya sasa ya utendaji kazi” amesema Qwaray.

Aidha, amesema Serikali pia inaendelea kuimarisha motisha na maslahi ya kada ya udereva, hatua ambayo inalenga kuongeza morali, ufanisi na tija katika utekelezaji wa majukumu yao.

Amesisitiza kuwa hatua hizo zinaendelea kuzingatia umuhimu wa kuhakikisha kada ya udereva inakuwa na mazingira bora ya utendaji kazi yanayomwezesha mtumishi kukidhi na kumudu mazingira ya utendaji kazi na hivyo kuchangia katika utoaji wa huduma bora kwa wananchi.