Monday, August 10, 2026

NAIBU KATIBU MKUU LWANGILI ASISITIZA UJUZI NA HAIBA YA UONGOZI KATIKA URITHISHANAJI MADARAKA KWA WATUMISHI WA UMMA

Na Antonia Mbwambo - Dodoma

Tarehe 10 Agosti, 2026

Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Prisca Lwangili, amesisitiza umuhimu wa kuendelea kujenga ujuzi wa kitaalamu na haiba ya uongozi katika kuwaandaa warithi wa madaraka ili kuhakikisha kunakuwa na mwendelezo wa utendaji na utoaji wa huduma bora katika Taasisi za umma.

Bi. Lwangili ameyasema hayo leo, Agosti 10, 2026, wakati akihitimsha mafunzo ya uelewa kuhusu Urithishanaji Madaraka yaliyofanyika katika eneo maalumu la Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Mtumba Jijini Dodoma.

Amesema maandalizi ya urithishanaji madaraka yanapaswa kuanza mapema kwa kuwajengea uwezo unaohitajika katika nafasi za uongozi wanazotarajiwa kuzishika.

Aidha, Bi. Lwangili ameongeza kuwa ujuzi wa kitaalamu (Technical Skills) humwezesha Mtumishi kuwa na maarifa na uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, huku haiba ya uongozi ikimsaidia kuwasiliana vizuri, kujiamini, kushirikiana na wengine, kuwa mwadilifu, kufanya maamuzi na kuwajibika.

“Kuwa na ujuzi wa kitaalamu pekee hakutoshi. Mtumishi anayejengwa kuwa Kiongozi wa baadaye anapaswa pia kuwa na haiba inayomjengea uwezo wa kuwasiliana vizuri, kujiamini, kushirikiana na wengine, kuwa mwadilifu, kufanya maamuzi na kubeba majukumu kwa uwajibikaji,” amesema Bi. Lwangili.

Pia Bi. Lwangili amesisitiza kuwa, Urithishanaji Madaraka si kumwandaa mtu kuchukua nafasi ya Kiongozi aliyepo pekee, bali ni kuimarisha Taasisi kwa kuwa na Watumishi wenye uwezo wa kuendeleza majukumu na huduma za umma.

Kwa upande wake, Mchumi Mkuu kutoka Idara ya Uendelezaji Rasilimaliwatu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Bi. Bertha Bomani, ameeleza kuwa Urithishanaji Madaraka ni mchakato wa kuwaandaa mapema Watumishi wenye uwezo na sifa stahiki kwa ajili ya majukumu ya uongozi.

Bi. Bomani amebainisha mikakati ya Urithishanaji Madaraka katika Utumishi wa Umma ikiwa ni pamoja na kuendelea kutoa elimu ya uelewa na kujenga uwezo kwa Viongozi na Watumishi kuhusu manufaa ya kuandaa na kutekeleza Mpango wa Urithishanaji Madaraka, pamoja na kuwakumbusha Waajiri kutenga fedha katika bajeti za Taasisi zao kwa ajili ya uandaaji na utekelezaji wa mpango huo.

 

Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Prisca Lwangili akizungumza na Watumishi wa Ofisi hiyo (hawapo pichani) wakati Naibu Katibu Mkuu huyo akihitimisha Mada ya mafunzo kuhusu Urithishanaji wa Madaraka leo tarehe 10 Agosti, 2026 Mtumba Jijini Dodoma.


Baadhi ya Wakurugenzi na Watumishi kutoka Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, wakifuatilia mafunzo ya Uelewa kuhusu Urithishanaji Madaraka yaliyofanyika tarehe 10 Agosti,2026 katika eneo maalumu la Ofisi hiyo iliyopo Mtumba Jijini Dodoma

Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Prisca Lwangili (aliyesimama mbele) akizungumza na Watumishi wa Ofisi hiyo wakati Naibu Katibu Mkuu huyo akihitimisha Mada ya mafunzo kuhusu Urithishanaji wa Madaraka leo tarehe 10 Agosti, 2026 Mtumba Jijini Dodoma

Baadhi ya Watumishi kutoka Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, wakifuatilia mafunzo ya Uelewa kuhusu Urithishanaji Madaraka yaliyofanyika tarehe 10 Agosti,2026 katika eneo maalumu la Ofisi hiyo iliyopo Mtumba Jijini Dodoma

Baadhi ya Watumishi kutoka Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, wakifuatilia mafunzo ya Uelewa kuhusu Urithishanaji Madaraka yaliyofanyika tarehe 10 Agosti,2026 katika eneo maalumu la Ofisi hiyo iliyopo Mtumba Jijini Dodoma

Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Prisca Lwangili (wa pili kutoka kulia) akifuatilia mafunzo ya uelewa ambayo hutolewa kila jumatatu ya wiki katika eneo maalumu la Ofisi hiyo Mtumba Jijini Dodoma leo tarehe 10, Agosti, 2026. Wengine ni Wakurugenzi na Wakurugenzi wasaidizi wa Idara na Vitengo vya Ofisi hiyo.

Mkurugenzi Idara ya Uendelezaji Rasilimaliwatu kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Leila Mavika akitoa ufafanuzi kuhusu Urithishanaji Madaraka mara baada ya muwezeshaji ambaye pia ni Mchumi Mkuu wa Ofisi hiyo, Bi. Bertha Bomani, kutoa maelezo kuhusu mada hiyo leo tarehe 10 Agosti, 2026 Jijini Dodoma

Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Prisca Lwangili (wa kwanza kutoka kushoto) akiteta jambo na Mkurugenzi wa TEHAMA Serikalini Bw. Priscus Kiwango (wa pili kutoka kushoto) wakati wa mafunzo ya uelewa kwa Watumishi wa Ofisi hiyo yaliyofanyika katika eneo maalumu la Ofisi hiyo iliyopo Mtumba Jijini Dodoma


Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Prisca Lwangili (wa kwanza kutoka kulia) akifuatilia mafunzo kuhusu Urithishanaji Madaraka kutoka kwa Mchumi Mkuu Idara ya Uendelezaji Rasilimaliwatu, Bi. Bertha Bomani leo tarehe 10 Agosti, 2026 Mtumba jijini Dodoma. Kulia kwake ni Wakurugenzi na Wakurugenzi wasaidizi wa Vitengo vya Ofisi hiyo.

Baadhi ya Wakurugenzi wasaidizi na Watumishi kutoka Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, wakifuatilia mafunzo ya Uelewa kuhusu Urithishanaji Madaraka yaliyofanyika tarehe 10 Agosti,2026 katika eneo maalumu la Ofisi hiyo iliyopo Mtumba Jijini Dodoma


Mchumi Mkuu kutoka Idara ya Uendelezaji Rasilimaliwatu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Bi. Bertha Bomani, akielezea dhana ya Urithishanaji Madaraka kwa Watumishi wa Ofisi hiyo wakati wa Mafunzo ambayo hufanyika kila jumatatu ya wiki kwa lengo la kuwajengea Watumishi hao uwezo wa kiutendaji Mtumba Jijini Dodoma

Baadhi ya Viongozi na Watumishi kutoka Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, wakifuatilia mafunzo ya Uelewa kuhusu Urithishanaji Madaraka yaliyofanyika tarehe 10 Agosti,2026 katika eneo maalumu la Ofisi hiyo iliyopo Mtumba Jijini Dodoma


Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Prisca Lwangili (wa kwanza kutoka kushoto) akisalimiana na baadhi ya Wakurugenzi wa Ofisi hiyo, mara baada ya Naibu Katibu Mkuu huyo kuhitimisha mafunzo ya uelewa kuhusu Urithishanaji Madaraka yaliyofanyika Jijini Dodoma.

Friday, August 7, 2026

KATIBU MKUU MKOMI ATEMBELEA MAONESHO YA NANENANE, APONGEZA HUDUMA ZINAZOTOLEWA KWA WANANCHI

Na. Mwandishi Wetu-Dodoma

Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bw. Juma Mkomi ametembelea baadhi ya mabanda yaliyopo katika Maonesho ya Kitaifa ya Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela, Nzuguni Jijini Dodoma.

Katibu Mkuu Mkomi, amepongeza utoaji wa huduma zinazotolewa kwa Watumishi wa Umma na Wananchi ambapo amewahimiza kufika katika maonesho hayo kwa ajili ya kupata huduma mbalimbali.

“Nashukuru nami nimepata nafasi ya kufika katika viwanja hivi kuona shughuli na huduma mbalimbali ambazo zinatolewa katika viwanja hivi, nipongeze waandaaji wa Maonesho ya Kitaifa ya Wakulima (Nanenane), huduma zinazotolewa ni nyingi hivyo niwahimize Watumishi wa Umma na Wananchi kufika katika maonesho hayo kwa ajili ya kupata huduma mbalimbali”, amesema Bw. Mkomi













Thursday, August 6, 2026

KIKWETE AFUNGUA PAREDI YA MIFUGO NA KITUO CHA HUDUMA KWA WATEJA NANENANE

Na Eric Amani, Dodoma

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete amesisitiza wafugaji kuendelea kutumia mbinu bora za ufugaji katika kuongeza thamani ya mifugo ili kukidhi matakwa ya soko la ushindani wa mifugo ndani na nje ya nchi.

Mhe. Kikwete amebainisha hayo leo tarehe 5 Agosti, 2026 wakati akifungua Paredi ya Mifugo katika Maonesho ya Kitaifa ya Wakulima maarufu kama Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela Jijini Dodoma.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa paredi hiyo, Mhe. Kikwete alisema kuwa sekta ya mifugo ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa taifa kupitia uzalishaji, biashara na ajira. Hivyo, hatuna budi kuongeza juhudi na jitihada za kuimarisha mbinu za ufugaji bora kwa maslahi ya taifa.

Vile vile, Mhe. Kikwete aliwataka wadau wa sekta ya mifugo kuendelea kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa sera na programu mbalimbali zinazolenga kuboresha huduma za ugani, udhibiti wa magonjwa ya mifugo na kuimarisha miundombinu ya masoko.

Nitumie fursa kuwahamasisha wafugaji wote nchini kubadilisha mtazamo wa ufugaji wa kimazoea kwenda ufugaji unaotumia sayansi, takwimu na teknolojia na pia kushiriki na kuleta mifugo yao kwa ajili ya gwaride na mashindano kwa mwaka ujao 2027” alisema Kikwete.

Aidha,  Paredi hiyo ilihusisha maonesho ya aina mbalimbali za mifugo ikiwemo ng'ombe, mbuzi na mifugo mingine ambapo wafugaji na taasisi mbalimbali walipata fursa ya kuonesha ubora wa mifugo yao pamoja na teknolojia na ubunifu unaotumika katika kuendeleza sekta hiyo.

Waziri Kikwete pia alitoa rai kwa taasisi za fedha nchini kuendelea kutoa mikopo yenye masharti nafuu na kubuni huduma za kifedha zinazokidhi mahitaji ya wafugaji, hususan wanawake na vijana, ili waweze kuwekeza katika sekta hii.

Pamoja na ufunguzi wa paredi ya mifugo, Mhe. Kikwete amezindua rasmi kituo cha huduma kwa wateja cha Wizara ya Kilimo na Uvuvi ambacho kitakuwa mahususi kwa ajili ya kutoa nakupokea taarifa za Kilimo na Uvuvi.

Amewataka watumishi watakaokuwa katika kituo hicho kupokea na kujibu hoja za wakulima, wafugaji na wavuvi kwa wakati ili kurahisisha zoezi la uzalishaji na uuzaji wa bidhaa za kilimo.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete akihotubia Wadau wa Sekta ya Mifugo na Uvuvi na wananchi (Hawapo Pichani) katika Siku ya Mifugo iliyofanyika katika viwanja vya nanenane kwenye sikukuu ya wakulima (nanenane) Agosti 05, 2026.

Mkuu wa Wilaya ya Singida Mjini Bw. Godwin Gondwe ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Singida katika maonesho ya sikukuu ya Mkulima (nanenane) akisikiliza hotuba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – UTUMISHI Mhe. Kikwete (hayupo pichani) Agosti 05, 2026 katika viwanja vya nanenane 

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Ng’wasi Damas Kamani akizungumza na Wadau wa Sekta ya Mifugo na Uvuvi na wananchi (Hawapo Pichani) katika Siku ya Mifugo iliyofanyika katika viwanja vya nanenane kwenye sikukuu ya wakulima (nanenane) Agosti 05, 2026. Aidha Mgeni Rasmi katika Siku hiyo alikuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete (Hayupo Pichani)

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete alipowasili katika viwanja vya nanenane kwa ajili ya kufungua kwa paredi ya mifugo Agosti 05, 2026 Jijini Dodoma

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete alipotembelea banda la Sekretariati ya Ajira katika maonesho ya nanenane katika viwanja vya malecela vilivyopo Nzuguni Dodoma


Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete akikata utepe baada ya kuzindua rasmi kituo cha huduma wa mteja kutoka Wizara ya Uvuvi na Mifugo katika Viwanja vya nanenane wakati wa maadhimisho ya sikukuu ya wakulima Agosti 05, 2026


Sehemu ya Wadau wa sekta ya uvuvi na mifugo wakisikiliza hotuba kutoka kwa Waziri Wa Nchi Ofisi ya Rais – UTUMISHI Mhe. Ridhiwani Kikwete (ayupo pichani) wakati wa Ufunguzi wa Paredi ya Mifugo katika viwanja vya nanenane Jijini Dodoma