Monday, May 18, 2026

UWEKEZAJI WA MIFUMO YA TEHAMA SERIKALINI KUONGEZA UFANISI NA UWAZI KATIKA UTOAJI WA HUDUMA

 Na. Antonia Mbwambo-Dodoma

Tarehe 18/05/2026

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray amesema uwekezaji wa matumizi ya Mifumo ya Tehama Serikalini utasaidia kwa asilimia kubwa kuongeza ufanisi na Uwazi wa huduma zinazotolewa na Watumishi wa umma kwa wananchi kwa maslahi ya Taifa

Mhe. Qwaray ameyasema hayo Mei 18, 2026 wakati akizungumza na Uongozi wa Kituo cha Utafiti na Ubunifu wa Maendeleo ya Serikali Mtandao (eGovRIDC), Menejimenti pamoja na Watumishi kutoka Taasisi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) mara baada ya Naibu Waziri huyo kutembelea Kituo hicho Jijini Dodoma.

“Ni lazima tufahamu kwamba, katika dunia ya sasa, mageuzi ya kidijiti si chaguo tena bali ni msingi wa ufanisi wa Serikali, ushindani wa kiuchumi na maendeleo ya kijamii”. Mhe. Qwaray alisema.

Amesema,Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwekeza katika mifumo ya TEHAMA ili kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato, kupunguza urasimu na rushwa, kuongeza uwazi, na kurahisisha upatikanaji wa huduma za wananchi popote walipo.

Mhe.Qwaray ameongeza kuwa, Serikali imepata mafanikio makubwa katika matumizi ya mifumo ya Kidijiti katika Sekta mbalimbali ikiwemo kuongeza uwajibikaji, kurahisisha upatikanaji wa huduma na kuboresha utendaji kazi wa Utumishi wa Umma.

Aidha, Mhe Qwaray amesema kituo hicho kimekuwa na mchango chanya katika matumizi ya Mifumo mbalimbali kama vile Mfumo wa   wa kielektroniki unaoiwezesha Serikali kupokea na kushughulikia malalamiko, maoni, pongezi, na maulizo kutoka kwa wananchi kwenda kwenye taasisi zote za umma (e-Mrejesho) pamoja na Mfumo wa Dirisha la Huduma za Serikali ikiwemo tangazo la Gazeti la Serikali na Utoaji wa Vibali vya Likizo bila Malipo.

Mhe. Qwaray ametoa wito kwa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali, Vyuo Vikuu, taasisi za tafiti pamoja na Sekta Binafsi ili tafiti zinazofanyika ziweze kutatua changamoto halisi za wananchi na taasisi za umma.

Vilevile ameitaka Taasisi hiyo kusimamia utekelezaji wa Sheria, Kanuni, na Miongozo ya Serikali Mtandao ili mifumo yote inayotengenezwa iwe salama, yenye kuwasiliana na mifumo mingine na kuleta tija kwa wananchi.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) Mhandisi Benedict Ndomba, amesema Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) ilianzisha Kituo cha Utafiti na Ubunifu wa Maendeleo ya Serikali Mtandao (e-GOVRIDC) kwa lengo la kuratibu shughuli za kitafiti, kubuni na kuendeleza jitihada za Serikali Mtandao, ili kuongeza tija katika utoaji wa huduma kwa umma, kuwajengea uwezo na kukuza vipaji vya vijana wabunifu katika eneo la TEHAMA.

Mhandisi Ndomba amemshukuru Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray kwa kuitikia wito wa kutembelea kituo hicho na kuahidi kwamba wameyapokea na wataenda kuyafanyia kazi maelekezo yote yaliyotolewa na kiongozi huyo.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (kulia) akisalimiana na baadhi ya Viongozi wa Kituo cha Utafiti na Ubunifu wa Maendeleo ya Serikali Mtandao (eGovRIDC) mara baada ya kuwasili katika kituo hicho kilichopo Jijini Dodoma.



Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (kulia) akikaribishwa na viongozi wa kituo cha Utafiti na Ubunifu wa Maendeleo ya Serikali Mtandao (eGovRIDC) mara baada ya kuwasili Kituoni  hapo Jijini Dodoma.

wa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray akizungumza na viongozi, na Watumishi wa Kituo cha Utafiti na Ubunifu wa Maendeleo ya Serikali Mtandao (eGovRIDC), mara baada ya kuwasili na kutembelea miradi mbalimbali ya kituo hicho Mei 18, 2026 jijini Dodoma

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika Kituo cha Utafiti na Ubunifu wa Maendeleo ya Serikali Mtandao (eGovRIDC) katika ziara ya kikazi kituoni hapo Jijini Dodoma.



Menejimenti na Watumishi wa Taasisi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (hayupo pichani) wakati akizungumza nao katika kituo cha Utafiti na Ubunifu wa Maendeleo ya Serikali Mtandao (eGovRIDC) Jijini Dodoma

Watumishi wa Taasisi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (hayupo pichani) wakati akizungumza nao katika kituo cha Utafiti na Ubunifu wa Maendeleo ya Serikali Mtandao (eGovRIDC) Jijini Dodoma.



Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA)   Mhandisi Benedict Ndomba akitoa ufafanuzi wa jambo kwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray kabla Naibu Waziri huyo kuzungumza na Menejimenti na Watumishi wa Taasisi ya Mamlaka ya
Serikali Mtandao (eGA) jijini Dodoma.


Menejimenti na Watumishi wa Taasisi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) wakimsikiliza  Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA)   Mhandisi Benedict Ndomba  (hayupo pichani) akitoa ufafanuzi kwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray kuhusu utendaji wa kituo cha Utafiti na Ubunifu wa Maendeleo ya Serikali Mtandao (eGovRIDC)   kilichopo Jijini Dodoma.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (aliyeka katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Menejimenti ya Taasisi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) mara baada ya Naibu Waziri huyo kuzungumza nao katika ziara ya kutembelea kituo cha Utafiti na Ubunifu wa Maendeleo ya Serikali Mtandao (eGovRIDC) Jijini Dodoma.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Qwaray (aliyekaa katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Watumishi wa Taasisi ya Mamlaka ya
Serikali Mtandao (eGA) mara baada ya kuzungumza nao alipokuwa katika ziara ya kutembelea kituo cha Utafiti na Ubunifu wa Maendeleo ya Serikali Mtandao (eGovRIDC) Jijini Dodoma


Friday, May 15, 2026

WAZIRI RIDHIWANI ASISITIZA UADILIFU, NIDHAMU WAHITIMU TAASISI YA UONGOZI

Na. Jawadu Kinyobwa

Waziri wa Nchi, Ofisi ya ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete amewataka Wahitimu wa Taasisi ya Uongozi kuwa waadilifu, wenye nidhamu na uthubutu ili kuleta maendeleo katika jamii na taifa kwa ujumla.

Mhe. Ridhiwani amebainisha hayo Mei 15, 2026 katika Sherehe ya Tisa ya Mahafali ya Taasisi ya Uongozi yaliyofanyika Mlimani City, Jijini Dar es salaam.

Aidha, amesema katika ulimwengu wa sasa uadilifu ndio sifa kuu ya kiongozi bora na mwenye kuaminika, hivyo watumie maarifa na ujuzi walioupata chuoni kuwa viongozi wanaozingatia haki, uwajibikaji na weledi katika kila jambo.

“Nawakumbusha umuhimu wa kuwa Viongozi Wenye Uzalendo. Tukumbuke msemo wa wahenga: Adhabu ya msaliti ni malipo ya usaliti wake. Usaliti mkubwa katika uongozi wa umma ni sawa na ubadhirifu wa mali za Umma” amesema.

Akizungumza kuhusu umuhimu wa uadilifu katika uongozi, amewasihi wahitimu hao kuwa viongozi wenye maadili mema, wanaolinda mali za umma na kuweka mbele maslahi ya wananchi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Amesema Taifa linahitaji viongozi waaminifu, wenye uwajibikaji na wanaotumia nafasi zao kusukuma mbele maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa manufaa ya Watanzania wote.

Sambamba na hayo, Mhe. Ridhiwani amesisitiza kuwa, uongozi bora na wa kuzingatia misingi ya haki na uwazi utasaidia kuendelea kuitangaza vyema Tanzania pamoja na Taasisi ya Uongozi ndani na nje ya nchi.

Awali akizungumza Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi Bw. Kadari Singo, amesema Taasisi hiyo imetimiza miaka kumi na tano tangu ilipoanzishwa rasmi Julai 2010 kwa Hati ya Rais kama Kituo cha Utaalamu wa Hali ya Juu (Centre of Excellence) cha kujenga na kuimarisha viongozi barani Afrika ili kuleta maendeleo endelevu.

Amebainisha kuwa, Taasisi hiyo imeendelea kufanya kazi kubwa na nzuri katika utoaji wa programu za mafunzo ya uongozi, uandaaji wa mijadala ya kisera, upanuzi wa dimbwi la maarifa kupitia tafiti na machapisho mbalimbali.

Akizungumza kwa niaba ya wahitimu, Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi Zanzibar (ZEEA), Juma Burhan Mohamed amesema mafunzo hayo yamekuwa chachu ya mabadiliko makubwa katika fikra, uwezo wa uongozi na namna ya kufanya maamuzi yenye tija kwa taasisi na jamii.

Amesema mahafali hayo hayakuwa tu sherehe ya kukamilisha mafunzo, bali yalikuwa ishara ya mabadiliko na ukuaji wa kiuongozi walioupata washiriki ndani ya kipindi cha miezi sita ya programu hiyo.

MWISHO.



Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akisoma nyaraka kabla ya kuzungumza na Wahitimu kwenye mahafali ya tisa ya programu za uongozi zitolewazo na Taasisi ya Uongozi yaliyofanyika leo Jijini Dar es Salaam. Kulia ni Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Bw. Juma Mkomi. 


Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora, Bi. Mary Mwakapenda akitunukiwa cheti cha Programu ya Uongozi kwa Wanawake na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete kwenye mahafali ya tisa ya programu za uongozi iliyotolewa na Taasisi ya Uongozi yaliyofanyika leo Jijini Dar es Salaam.


Baadhi ya Wahitimu wa Programu ya Uongozi kwa Wanawake wakiwa mbele mara baada ya kutunukiwa vyeti vyao na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete kwenye mahafali ya tisa ya programu za uongozi zitolewazo na Taasisi ya Uongozi yaliyofanyika leo Jijini Dar es Salaam.


Mkurugenzi Msaidizi sehemu ya Usimamizi wa Rasilimaliwatu, Bi. Mwalibora Mwamtuya kutoka Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora, akitunukiwa cheti cha Programu ya Uongozi kwa Wanawake na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete kwenye mahafali ya tisa ya programu za uongozi zitolewazo na Taasisi ya Uongozi yaliyofanyika leo Jijini Dar es Salaam.



Mkurugenzi Msaidizi, Sehemu ya Ushirikiano wa Kimataifa katika Usimamizi wa Rasilimaliwatu, Bi. Judith Shoo kutoka Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora akitunukiwa cheti cha Programu ya Uongozi kwa Wanawake na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete kwenye mahafali ya tisa ya programu za uongozi zitolewazo na Taasisi ya Uongozi yaliyofanyika leo Jijini Dar es Salaam.


Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi, Bw. Kadari Singo akizungumza na Wahitimu wa Programu ya Uongozi kabla ya wahitimu hao kutunukiwa vyeti vyao na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete kwenye mahafali ya tisa ya programu za uongozi zitolewazo na Taasisi hiyo yaliyofanyika leo Jijini Dar es Salaam.



Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wahitimu wa Programu ya Uongozi mara baada ya wahitimu hao kutunukiwa vyeti vyao na Waziri huyo kwenye mahafali ya tisa ya programu za uongozi zitolewazo na Taasisi hiyo yaliyofanyika leo Jijini Dar es Salaam.