Tuesday, April 29, 2025

OFISI YA RAIS-UTUMISHI YAWAPIGA MSASA WATUMISHI ILI KUIMARISHA MAZINGIRA BORA YA BIASHARA NA UWEKEZAJI NCHINI

 Na Mwandishi wetu-Morogoro

Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora inaendesha mafunzo ya siku tatu kwa Watumishi 100 waliopo katika Taasisi Rekebu zinazohusika na uboreshaji wa mazingira ya biashara na Uwekezaji nchini, ili kuwaongezea ujuzi na kuwajengea uwezo katika utekelezaji wa majukumu yao.

Mafunzo hayo yamefunguliwa leo tarehe 28 Aprili, 2025 mjini Morogoro na mwakilishi wa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Uendelezaji Maadili, Bi. Leila Mavika.

Bi. Mavika amesema mafunzo hayo yanafanyika kufuatia eneo hilo kuwa na changamoto mbalimbali zikiwemo kutumia muda mwingi na gharama kubwa za kifedha wakati wa kuanzisha na  kuendesha biashara, uwepo wa taratibu nyingi na zinazojirudia zinazotakiwa kufuatwa na wawekezaji, pamoja na mapungufu katika baadhi ya Sheria na Kanuni zinazotumiwa na Taasisi Rekebu.

Amesema pamoja na mambo mengine, ilionekana masuala hayo yakifanyiwa kazi yatawezesha Nchi kuwa na mazingira mazuri ya kufanyia biashara ambayo yatavutia wawekezaji wengi zaidi.

Bi. Leila ameongeza kuwa, Serikali imeanza utekelezaji wa Mpango wa Kuboresha Uwekezaji na Mazingira ya Biashara (MKUMBI) awamu ya Kwanza kwa lengo la kufanya mageuzi na kuboresha Mazingira ya Biashara nchini Tanzania ili kuwapunguzia mzigo na vihatarishi wafanyabiashara kwa kuhusianisha mifumo ya udhibiti wa biashara ili kuzuia uwepo wa taratibu nyingi zinazojirudia na mwingiliano wa majukumu ndani ya Taasisi Rekebu na kuhakikisha kunakuwepo na uwazi wa mifumo ya udhibiti wa uwekezaji na biashara kupitia majukwaa mbalimbali ya TEHAMA ambayo hutoa taarifa za taratibu za udhibiti kwa Umma.

Amesema Ofisini hiyo ni mojawapo ya Taasisi iliyopo katika Mpango huu kutokana na jukumu ililonalo la kusimamia mafunzo katika Utumishi wa Umma kwa mujibu wa Hati idhini ya uanzishwaji wa Wizara.

Amesema katika mwaka wa fedha 2023/2024, Ofisi ya Rais-UTUMISHI ilifanya survey kwa baadhi ya Taasisi Rekebu 31 ili kukusanya taarifa za upungufu wa ujuzi katika Taasisi hizo na kuchukua hatua stahiki za kuondosha upungufu huo.

Mafunzo yanayoanza leo yamejikita katika kushughulikia maeneo ya upungufu wa ujuzi yaliobainishwa na survey hiyo ambayo ni Mafunzo mbalimbali kama vile Kuimarisha Mazingira ya Uwekezaji; Ujuzi wa Majadiliano (Negotiation Skills); Utunzaji na Matumizi Sahihi na Salama ya Nyaraka na Kumbukumbu; Uwezo wa Kufikiri Kimkakati na Utoaji wa Maamuzi Sahihi; Utunzaji wa Muda; Namna ya Kuwa Mtumishi wa Thamani katika Taasisi; Akili Hisia; Huduma kwa Mteja na mengine mengi.

Bi. Mavika amewataka Watumishi wote  ambao wanahudumu katika Taasisi Rekebu kuzingatia Maadili ya Utumishi wa Umma wakati wa utekelezaji wa majukumu yao ikiwemo kutumia lugha nzuri, bila upendeleo na kuepuka RUSHWA ili kulinda taswira na heshima ya Utumishi wa Umma na Taifa kwa ujumla.

 “Ni Imani yangu kuwa uchaguzi wa Taasisi hizi haukuwa wa bahati mbaya bali ni wenye makusudi mahsusi yenye dhamira ya kuboresha utendaji kazi wenu kwa kuwaongezea ujuzi ili kuhakikisha Taasisi zenu zinatengeneza mazingira rafiki na wezeshi kwa Wawekezaji wanaokuja kupata huduma.” Amesisitiza Bi. Mavika.  

 Amesema uboreshaji wa mazingira ya ufanyaji Biashara na Uwekezaji katika nchi yetu ni jambo la muhimu kwa kuwa ni eneo linalowezesha Serikali kupata mapato na kuboresha huduma kwa Wananchi.

Mwaka 2018, Serikali kupitia Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji ilizindua Mpango wa Maboresho ya Mazingira ya Biashara, Mpango ambao uliwezesha nchi kufanya mapitio ya mfumo wa mazingira wezeshi ya biashara (BEE) kwa lengo la kuboresha mazingira ya biashara.




Kaimu Katibu Mkuu Bi. Leila Mavika akizungumza na Watumishi wa Umma kutoka Taasisi mbalimbali mara wakati akifungua mafunzo ya kuongeza ujuzi kuhusu uboreshaji wa mazingira ya biashara katika taasisi za umma yanayofanyika kwa muda wa siku tatu kuanzia  leo Aprili, 2025 Mkoani Morogoro

 

 




Baadhi ya Watumishi wa Umma  kutoka Taasisi mbalimbali  wanaoshiriki  mafunzo ya uboreshaji wa mazingira ya biashara katika Taasisi za umma rekebuyanayofanyika kwa muda wa siku tatu kuanzia  leo tarehe 28 Aprili, 2025  Mkoani Morogoro


 Mkurugenzi wa Idara ya Huduma za Kumbukumbu, Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Bw. Gasper Kileo akitoa mafunzo kwa watumishi wa umma  kutoka Taasisi mbalimbali wanaoshiriki mafunzo ya siku tatu kuanzia leo AprilI 28 yanayofanyika Mkoani Morogoro





Wednesday, April 23, 2025

HOTUBA YA WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA, MHE. GEORGE SIMBACHAWENE KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA WA FEDHA 2025/26 BUNGENI JIJINI DODOMA


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene akiwasilisha Hotuba kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora kwa mwaka wa fedha 2025/26 leo Aprili 23, 2025 Bungeni jijini Dodoma.

Viongozi na Wakuu wa Taasisi wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora wakifuatilia Hotuba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi hiyo kwa mwaka wa fedha 2025/26 leo Aprili 23, 2025 Bungeni jijini Dodoma.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene akizungumza jambo na Viongozi wa Ofisi yake baada ya kuwasili Bungeni kwa ajili ya kuwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Ofisi hiyo kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi  kwa mwaka wa fedha 2025/26 leo Aprili 23, 2025 Bungeni jijini Dodoma.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi na Wakuu wa Taasisi wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora kabla ya kuwasilisha Hotuba kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora kwa mwaka wa fedha 2025/26 leo Aprili 23, 2025 Bungeni jijini Dodoma.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene akifurahia jambo na Katibu wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma, Bw. Mick Kiliba. Wa kwanza kulia ni Mkurugenzi Mkuu, Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA), Mhandisi Benedict Ndomba.


Katibu Mkuu-IKULU, Bw. Mululi Mahendeka (kulia) akisalimiana na Katibu Mkuu-UTUMISHI Bw. Juma Mkomi (katikati) na Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Bw. Xavier Daudi (kushoto)


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene akiwasili Bungeni kuwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Ofisi yake kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi  kwa mwaka wa fedha 2025/26 leo Aprili 23, 2025 jijini Dodoma.






HOTUBA YA BAJETI YA OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA







 

HOTUBA YA WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA, MHE. GEORGE SIMBACHAWENE

 


Thursday, April 17, 2025

SERIKALI YA AWAMU YA SITA YAJIVUNIA MAFANIKIO LUKUKI KATIKA KIPINDI CHA MIAKA MINNE YA UONGOZI WA RAIS MHE. DKT. SAMIA SULUHU HASSAN

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kipindi cha miaka minne imepata mafanikio makubwa katika maeneo mbalimbali. 

Amesema mafanikio haya yanatokana na azma ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutaka kuujenga Utumishi wa Umma kuwa wenye tija katika maendeleo ya taifa.

Mhe. Simbachawene ameyasema hayo leo tarehe 17 Aprili, 2025 wakati akizungumza na vyombo vya habari kuelezea mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Sita katika Ukumbi wa Idara ya Habari MAELEZO Jijini Dodoma.

Ameyataja miongoni mwa mafanikio yaliyopatikana kuwa ni pamoja na

kusimamia Mikataba ya Utendaji Kazi Serikalini ambapo Serikali ilijenga mfumo wa Usimamizi wa Utendaji Kazi katika Utumishi wa Umma (e-UTENDAJI - PEPMIS/PIPMIS) unaotumika kusimamia utendaji kazi wa watumishi wa umma na taasisi za umma ili kuwezesha kubaini kiwango cha utendaji kazi na uwajibikaji wa viongozi na watumishi wa umma.

Kusimamia Mipango na Uendelezaji Rasilimaliwatu katika Utumishi wa Umma baada ya kuona kuna tatizo la upungufu wa watumishi katika maeneo mengi, ilitafuta namna bora ya kuondoa changamoto hiyo kwa kujenga Mfumo wa Tathmini ya Mahitaji ya Rasilimaliwatu (HR-Assessment).

“Mfumo huu wa Tathmini ya Mahitaji ya Rasilimaliwatu ni msaada mkubwa kwani unabainisha idadi ya watumishi walioko katika kila kituo cha kazi na upungufu au ziada iliyopo ili kuwa na idadi ya watumishi sahihi katika sehemu sahihi za utekelezaji wa majukumu yao.” ameeleza Mhe. Simbachawene

Katika eneo la Usimamizi wa Maslahi na Stahiki za Watumishi wa Umma Mhe, Simbachawene amesema, Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameyaangalia maslahi ya watumishi wa umma kwa jicho la pekee ikiwemo kupunguza kodi ya mapato (PAYE) kutoka 9% hadi asilimia 8%, kufuta tozo (retention fee) ya 6% iliyokuwa ikitozwa kutoka katika mishahara ya watumishi wa Umma walionufaika na Mikopo ya Elimu ya Juu, kulipa malimbikizo ya mshahara, kupandisha vyeo, kubadilisha kada pamoja na kuundwa kwa Mfumo wa Huduma Mtandao kwa Watumishi (Watumishi Portal) unaowawezesha Watumishi wa Umma kupata huduma mbalimbali za kiutumishi moja kwa moja bila kulazimika kwenda kwenye Ofisi za Waajiri wao.

Mhe. Simbachawene amefafanua kuwa hadi kufikia tarehe 31 Machi, 2025 madai ya malimbikizo ya mishahara ya watumishi 148,137 yenye jumla ya Sh. 248,528,998,254.79 yalipokelewa na kushughulikiwa. Aidha, katika kipindi hicho, madai ya malimbikizo ya mishahara ya watumishi wastaafu 10,022 kutoka kwa waajiri yenye jumla ya Sh. 33,290,109,780.75 yamepokelewa na kushughulikiwa na wahusika wamelipwa kupitia kwa waajiri wao.

Ameongeza kuwa mpaka kufikia tarehe 31 Machi, 2025 Jumla ya watumishi wa umma 610,733 wamepandishwa vyeo, 42,515 wamebadilishwa kada, 3,208 wamepata uteuzi, 157,512 wamesafishiwa taarifa zao za kiutumishi, 10,725 wamebadilishiwa vyeo, 3,877 wamerekebishiwa majina, 9,269 wamefanyiwa mabadiliko ya mshahara binafsi, 2,558 wamerejeshwa kwenye utumishi wa umma na 133,317 wameajiriwa katika Taasisi mbalimbali za umma. Aidha, katika kipindi hicho, Jumla ya nafasi za ajira 155,008 zimetolewa na jumla vibali vya ajira mbadala 41,673 vimetolewa ili kujaza nafasi zilizobaki wazi kwa sababu mbalimbali. 

Mhe. Simbachawene amesema, Mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Sita kwa kipindi cha miaka minne yameonekana pia kwa upande wa Mfuko wa maendeleo ya Jamii (TASAF) kwani, Mpango wa Miradi ya Kutoa Ajira za Muda kwa Walengwa kufikia Desemba, 2024, jumla ya miradi 27,863 ya kutoa ajira za muda kwa walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini imetekelezwa.

Kwa upande wa TAKUKURU, Mhe. Simbachawene amesema, TAKUKURU imetekeleza majukumu yake kwa ufanisi kwa kuimarisha mapambano dhidi ya rushwa nchini ambapo Programu ya TAKUKURU Rafiki ilizinduliwa ili kuleta mafanikio makubwa na kero nyingi zilizoibuliwa zilitatuliwa ikiwamo sekta za afya, elimu, maji, nishati, mawasiliano, maendeleo ya jamii, mazingira, ujenzi, ardhi, kilimo, ufugaji, usafirishaji, usalama na haku jinai, hivyo kuzuia vitendo vya rushwa na kuboresha huduma zinazotolewa kwa umma.

Waziri Simbachawene ameongeza kuwa, katika kuhakikisha Tanzania inakuwa ya kidijitali, Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) imetekeleza agizo la Mhe. Rais kwa kujenga na kusanifu mfumo wa pamoja wa Ubadilishanaji Taarifa Serikalini (Government Enterprise Service Bus-GovESB) ili kuimarisha utoaji wa huduma bora kwa wananchi sambamba na kupunguza mianya ya rushwa, kuondoa urasimu na kurahisisha utekelezaji wa majukumu ya kila siku ya Serikali,

Aidha, katika kutengeneza Mfumo shirikishi utakaowezesha Mifumo ya Taasisi kuwasiliana na kubadilishana taarifa, mifumo 202 ya taasisi za umma 179 imeunganishwa na inabadilishana taarifa ikiwemo Taasisi za Sekta ya Haki Jinai zinazojumuisha Mahakama, TAKUKURU, Polisi na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka.

Mhe. Simbachawene amempongeza na kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa maelekezo na kusimamia kikamalifu kuhakikisha yametekelezwa kwa ufanisi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene akizungumza wakati wa Mkutano wake na Waandishi wa Habari kuhusu Mafanikio ya Miaka 4 ya Serikali ya Awamu ya Sita kwenye eneo la Utumishi wa Umma na Utawala Bora leo tarehe 17, Aprili 2025 jijini Dodoma.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. George Simbachawene (wa kwanza kushoto) akimsikiliza Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari Maelezo, Bw. Rodney Thadeus (hayupo pichani) wakati akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Waziri huyo kuzungumza na Waandishi wa Habari kuhusu Mafanikio ya Miaka 4 ya Serikali ya Awamu ya Sita kwenye eneo la Utumishi wa Umma na Utawala Bora leo tarehe 17, Aprili 2025 jijini Dodoma. Kushoto kwake ni Katibu Mkuu wa Ofisi yake Bw. Juma Mkomi.


Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Bw. Shedrack Mziray (wa kwanza kushoto), Mkurugenzi wa Fedha na Utawala-TASAF, Bw. Godwin Mkisi (katikati) na Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Bi. Mary Mwakapenda (wa kwanza kulia) wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene wakati akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu Mafanikio ya Miaka 4 ya Serikali ya Awamu ya Sita kwenye eneo la Utumishi wa Umma na Utawala Bora leo tarehe 17, Aprili 2025 jijini Dodoma.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene akifafanua jambo wakati wa Mkutano wake na Waandishi wa Habari kuhusu Mafanikio ya Miaka 4 ya Serikali ya Awamu ya Sita kwenye eneo la Utumishi wa Umma na Utawala Bora leo tarehe 17, Aprili 2025 jijini Dodoma.



  

Wednesday, April 16, 2025

SEKRETARIETI YA AJIRA YAPONGEZWA KWA KUFANYIA KAZI USHAURI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UTAWALA, KATIBA NA SHERIA

Na Veronica Mwafisi-Dodoma

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria imeipongeza Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma kwa kuzingatia maoni na ushauri unaotolewa na kamati hiyo ili kuhakikisha mchakato wa ajira unafanyika kwa ufanisi mkubwa na uwazi wa hali ya juu.  

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Dkt. Joseph Mhagama ametoa pongezi hizo leo jijini Dodoma kwa niaba ya Kamati yake wakati wa ziara ya kikazi ya Kamati hiyo iliyolenga kutembelea na kujifunza utendajikazi wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma.

Mhe. Dkt. Mhagama ametolea mfano maoni ambayo Kamati yake iliyatoa kuhusu usaili kufanyika katika ngazi za mikoa badala ya kuwalazimu waombaji kazi wote kufika jijini Dodoma kumeleta matokeo chanya kwa waombaji kazi hao.

Vilevile Dkt. Mhagama amezungumzia matumizi ya mfumo wa Ajira Portal kwa waombaji kazi kuondokana na dhana tofauti ya upendeleo wa kupata ajira katika Utumishi wa Umma.

“Mfumo wa Ajira Portal umeondoa  dhana ya kuwepo kwa upendeleo  kwa waombaji kazi, ninaamini wengi wamepata ajira serikalini pasipo kupitia kwa mtu yeyote.” amesema Mhe. Dkt. Mhagama. 

Kwa Upande wake Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu ameishukuru Kamati hiyo kwa kutoa maoni na ushauri mara zote ambao kwa kiasi kikubwa umesaidia kutekeleza majukumu ya Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma kikamilifu.

Aidha, Naibu Waziri Sangu amewaomba Wajumbe wa Kamati hiyo kuendelea kuwa Mabalozi wazuri wa Sekretarieti ya Ajira Katika Utumishi wa Umma ili kuwahakikishia wananchi kuhusu uwazi wa namna ajira katika Utumishi wa Umma zinavyopatikana kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu zilizowekwa na Sekretarieti hiyo wakati wa kuomba kazi.

Akielezea mafanikio baada ya kutumia mfumo wa Ajira Portal, Kaimu Katibu wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma, Mhandisi Samweli Tanguye amesema, kupitia mifumo wameweza kuajiri Rasilimaliwatu yenye uwezo wa kufanya kazi na kutoa matokeo chanya pamoja na kuondoa hoja za kuajiri kwa dhana ya upendeleo.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Kizito Mhagama (katikati) akizungumza na Viongozi na Watendaji wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma wakati wa ziara ya Kamati hiyo iliyolenga kutembelea na kujifunza kuhusu utendajikazi wa ofisi hiyo jijini Dodoma.


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Kizito Mhagama (watatu kutoka kulia) akifuatilia wasilisho kuhusu mchakato wa usaili wa ajira unavyofanyika wakati wa ziara ya kamati hiyo iliyofanyika jijini Dodoma. Kushoto kwake ni Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu na wa kwanza kulia ni Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Bw. Nolasco Kipanda.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Kizito Mhagama (hayupo pichani) wakati wa ziara ya Kamati yake iliyofanyika katika ofisi za Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma jijini Dodoma.

 

Sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Utawala, Katiba na Sheria wakifuatilia wasilisho kuhusu mchakato wa ajira unavyofanyika wakati wa ziara ya kamati hiyo katika Ofisi ya Sekretarieti ya Ajira Katika Utumishi wa Umma iliyofanyika jijini Dodoma.


Wakurugenzi wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Viongozi na Watendaji wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma wakimsikiliza Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Kizito Mhagama (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza nao wakati wa ziara ya kamati yake katika ofisi hiyo iliyofanyika jijini Dodoma.


Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Utawala, Katiba na Sheria Mhe. Omar Kombo akiwasilisha hoja wakati wa ziara ya Kamati hiyo katika ofisi ya Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma iliyolenga kutembelea na kujifunza kuhusu utendajikazi wa ofisi hiyo jijini Dodoma.


Kaimu Katibu wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma, Mhandisi Samweli Tanguye akiwasilisha mada kuhusu TEHAMA ilivyoboresha mchakato wa ajira wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Utawala, Katiba na Sheria iliyolenga kutembelea na kujifunza kuhusu utendajikazi wa ofisi hiyo jijini Dodoma.


Kaimu Naibu Katibu, Menejimenti ya Ajira, Bi. Somwana Manjenga akiwasilisha mada kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Utawala, Katiba na Sheria kuhusu mchakato wa ajira wakati wa ziara ya kikazi ya Kamati hiyo iliyolenga kutembelea na kujifunza kuhusu utendajikazi wa ofisi hiyo jijini Dodoma.


Sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Utawala, Katiba na Sheria wakifuatilia wasilisho kuhusu mchakato wa ajira unavyofanyika wakati wa ziara ya kamati hiyo katika Ofisi ya Sekretarieti ya Ajira Katika Utumishi wa Umma iliyofanyika jijini Dodoma.


Sehemu ya Maafisa kutoka Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma wakisikiliza maoni ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Utawala, Katiba na Sheria wakati wa ziara ya kikazi ya Kamati hiyo iliyolenga kutembelea na kujifunza kuhusu utendajikazi wa ofisi hiyo jijini Dodoma.



 WANAMICHEZO UTUMISHI WAPEWA HAMASA KUELEKEKEA MASHINDANO YA MEI MOSI SINGIDA

“Ninaamini wote tuna afya njema na tuko tayari kupambana na kuendelea kulinda taswira njema ya ofisi yetu, kwa hiyo twendeni tukashiriki mashindano hayo tukiwa na umoja na ari kubwa, tukilenga kurudi na vikombe vingi zaidi ya mwaka 2024”

Wito huo umetolewa na Kaimu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Bw. Xavier Daudi wakati wa kikao kifupi kilichofanyika katika jengo la ofisi za Utumishi, Mtumba jijini Dodoma kwa lengo la kuwaaga Viongozi na Wanamichezo wa ofisi yake wanaokwenda Mkoani Singida kushiriki Mashindano ya Michezo ya Siku ya Wafanyakazi Duniani.

Bw. Daudi aliwasisitiza viongozi na wanamchezo hao kushiriki michezo yote kikamilifu na kuzingatia sheria na kanuni za michezo zilizoandaliwa ili kupata ubingwa na vikombe vingi zaidi kuliko kipindi kilichopita.

Aidha, aliwataka watumishi hao kuwa na nidhamu na kuzingatia maadili ya utumishi wa umma kwa kuwa wamebeba sura chanya ya ofisi ambayo ndiyo yenye dhamana ya kusimamia maadili ndani ya Utumishi wa Umma.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Uendelezaji Taasisi na Mlezi wa Wanamichezo hao Bw. Nolasco Kipanda alisema kuwa mwaka 2024 wakati wa mashindano ya SHIMIWI Ofisi ilishinda Makombe Matatu (3) ikiwa ni pamoja na kombe la mpira wa miguu, hivyo amewahimiza wanamichezo hao kuongeza jitihada zaidi ili kuleta heshima kubwa hata katika mashindano ya Mei Mosi.

Bw. Kipanda kwa niaba ya Wanamichezo hao amewashukuru na kuwapongeza Viongozi na Timu ya Menejimenti kwa upendo na ushirikiano wanaoonesha katika michezo hadi kupata mafaniko ya kushinda makombe katika mashindano mbalimbali.

Naye, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Maadili Bi. Leila Mavika amewataka wanamichezo hao kuwa na maadili mema wakati wote na kuepuka unywaji wa pombe kupita kiasi na kukosa staha.

“Nawakumbusha kutunza mbinu na taarifa nyingine za kambi na kuheshimu sheria, kanuni na miongozo inayoongoza Utumishi wa Umma na michezo ambayo tunaenda kishiriki” alisisitiza Bi. Mavika

Awali, Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Bw. Musa Magufuli amesema jumla ya Watumishi 57 wameruhisiwa kwenda Mkoani Singida kwa ajili ya kushiriki mashindano ya siku ya Wafanyakazi Duniani na Ofisi itashiriki michezo mbalimbali ikiwa ni pamoja na mpira wa miguu, mpira wa pete, karata, riadha na bao ambayo inatarajiwa kuanza Aprili 15, 2025.

Kaimu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, UTUMISHI na Utawala Bora Bw. Xavier Daudi akizungumza na Viongozi na Wanamichezo wa ofisi yake wanaokwenda Mkoani Singida kushiriki Mashindano ya Michezo ya Siku ya Wafanyakazi Duniani wakati wa kikao kifupi cha kuwaaga kilichofanyika katika jengo la ofisi za Utumishi, Mtumba jijini Dodoma


Mratibu wa Michezo Ofisi ya Rais, UTUMISHI na Utawala Bora Bw. Charles Shija akitoa ufafanuzi wa ushiriki wa Ofisi ya Rais UTUMISHI katika michezo ya Mei Mosi mbele ya Kaimu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Bw. Xavier Daudi


Kaimu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, UTUMISHI na Utawala Bora Bw. Xavier Daudi akiwasikiliza Wanamichezo wa ofisi yake wanaokwenda Mkoani Singida kushiriki Mashindano ya Michezo ya Siku ya Wafanyakazi Duniani wakati wa kikao kifupi cha kuwaaga kilichofanyika katika jengo la ofisi za Utumishi, Mtumba jijini Dodoma

Timu ya Wanawake ya Mpira wa Pete na Kikapu ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ikiwa katika picha ya pamoja baada ya kuagwa na Kaimu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Bw. Xavier Daudi (Hayupo pichani) ili kushiriki Mashindano ya Michezo ya Siku ya Wafanyakazi Duniani yanayofanyika Mkoani Singida. 

Timu ya Wanawake ya Mpira wa Pete na Kikapu ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ikiwa katika picha ya pamoja baada ya kuagwa na Kaimu Katibu Mkuu wa Ofisi hiyo Bw. Xavier Daudi (Hayupo pichani) ili kushiriki Mashindano ya Michezo ya Siku ya Wafanyakazi Duniani yanayofanyika Mkoani Singida.