Na. Veronica Mwafisi-Dar ES Salaam
Tarehe 03 Julai, 2026
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya
Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema miaka 25 ya
Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) ina nafasi ya kipekee katika kujenga
na kuendeleza uwezo wa kiutendaji wa watumishi wa umma ambao ndio watekelezaji
wa majukumu ya Serikali kila siku.
Waziri Kikwete ameyasema hayo leo tarehe 03
Julai, 2026 wakati wa hafla ya kilele cha maadhimisho ya miaka 25 ya TPSC
yaliyofanyika katika Ukumbi wa Kituo cha
Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere kilichopo Jijini Dar es Salaam.
Mhe. Kikwete amesema, Serikali ya Awamu ya
Sita chini ya Uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeendelea
kuweka kipaumbele katika uimarishaji wa Utumishi wa Umma ili kuhakikisha
wananchi wanapata huduma bora, za haraka na zenye tija.
Mhe. Kikwete ameongeza kuwa, Chuo cha
Utumishi wa Umma Tanzania si tu taasisi ya mafunzo, bali ni nguzo muhimu ya
Serikali katika kujenga rasilimaliwatu yenye maarifa, stadi, maadili na
uzalendo unaohitajika katika kutumikia umma kwa ufanisi.
Katika hatua nyingine, Mhe. Kikwete amesema
kuwa, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inatutaka kuwa na Taifa lenye uchumi wa
kisasa, ushindani wa kimataifa, matumizi makubwa ya teknolojia, na huduma za
umma zenye ufanisi wa hali ya juu. Hivyo, mafanikio ya Dira hiyo yatategemea
kwa kiasi kikubwa uwepo wa watumishi wenye sifa, ujuzi na uwezo wa kuongoza
mabadiliko hayo.
“Chuo hiki kina wajibu mkubwa wa kuhakikisha Watumishi wa Umma wanapata maarifa na stadi
zinazolingana na mahitaji ya karne ya ishirini na moja ili kuwepo wa watumishi
wenye sifa, ujuzi na uwezo wa kuongoza mabadiliko hayo,” amesema Waziri
Kikwete.
Aidha, Mhe. Kikwete amewapongeza watangulizi
wake kwa usimamizi mzuri ambao umechangia mafanikio makubwa ya Chuo hicho huku
akimshukuru Katibu Mkuu wa Ofisi yake, Bw. Juma Mkomi kwa kuendelea kusimamia
Chuo hicho kiutendaji.
Vilevile, Waziri Kikwete ameipongeza Bodi ya
Ushauri ya TPSC, Menejimenti, Watumishi, Wanafunzi na wadau wote kwa mchango
wao katika safari ya kutimiza miaka 25 ya mafanikio ya chuo hicho.
Akitoa maelezo ya awali kabla ya kumkaribisha
Mhe. Waziri kuzungumza na wadau katika hafla hiyo, Katibu Mkuu Ofisi ya
Rais-UTUMISHI, Bw. Juma Mkomi ametoa wito kwa waajiri kutumia Kampasi za TPSC
zilizo katika kanda zao ili kuwawezesha watumishi ikiwemo waajiriwa wapya
kupata mafunzo ya awali.
“Kampasi katika Kanda hizo zimewekwa
kimkakati ili kusogeza huduma za chuo katika mikoa mbalimbali, hivyo Waajiri wazitumie
kikamilifu kwa watumishi kupata mafunzo kwa lengo la kuboresha utendaji kazi.”
Amesisitiza Katibu Mkuu Mkomi.
Amezitaja Kampasi hizo kuwa ni Dar es Salaam,
Mbeya, Tanga, Singida, Tabora na Mtwara na kuongeza kuwa Ofisi ya Rais-UTUMISHI
itaendelea kuunga mkono jitihada zinazofanywa na TPSC za kumiliki majengo yao
ambapo Kampasi ya Singida inaendelea na ujenzi wa majengo 30 na Kampasi ya
Tanga majengo 15.
Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya TPSC,
Dkt. Florens Turuka amesema Bodi itaendelea kutoa ushauri ili Chuo kiendelee
kuwa kinara katika masuala mbalimbali ikiwemo kujenga rasilimaliwatu yenye
maadili, na yenye tija kwa taifa.
Akiwasilisha taarifa ya miaka 25 ya TPSC, Mkuu
wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania, Dkt. Ernest
Mabonesho amesema tangu kuanzishwa kwake, Chuo kimepata mafanikio makubwa
katika maeneo mbalimbali ikiwemo taaluma, rasilimaliwatu na miundombinu.
Waziri
wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani
Kikwete akizungumza wakati wa hafla ya kilele cha maadhimisho ya miaka 25 ya
Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) yaliyofanyika katika Ukumbi wa Kituo cha Mikutano
cha Kimataifa cha Julius Nyerere kilichopo Jijini Dar es Salaam.
Viongozi mbalimbali, Wadau na Wanafunzi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza nao wakati wa hafla ya kilele cha maadhimisho ya miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania yaliyofanyika katika Ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere kilichopo Jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya
Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (kushoto) akiteta
jambo na Katibu Mkuu wa ofisi yake Bw. Juma Mkomi (kulia) wakati wa kilele cha
maadhimisho ya miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC)
yaliyofanyika katika Ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere
kilichopo Jijini Dar es Salaam.
Menejimenti,
Wadau na Wanafunzi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) wakimsikiliza Waziri
wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.
Ridhiwani Kikwete (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza nao wakati wa hafla ya
kilele cha maadhimisho ya miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania
yaliyofanyika katika Ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere
kilichopo Jijini Dar es Salaam.
Waziri
wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.
Ridhiwani Kikwete (kulia) akifurahia jambo na Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu, Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC),
Dkt. Ernest Mabonesho (kushoto) wakati wa hafla ya kilele cha
maadhimisho ya miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania yaliyofanyika
katika Ukumbi wa Kituo
cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere kilichopo Jijini Dar es Salaam.
Wanafunzi
wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania
(TPSC) wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya
Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete (hayupo pichani)
alipokuwa akizungumza nao kwenye hafla ya kilele cha maadhimisho ya miaka 25 ya
Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania yaliyofanyika katika Ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha
Kimataifa cha Julius Nyerere kilichopo Jijini Dar es Salaam.
Menejimenti,
Wadau na Wanafunzi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) wakimsikiliza Waziri
wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.
Ridhiwani Kikwete (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza nao wakati wa hafla ya
kilele cha maadhimisho ya miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania
yaliyofanyika katika Ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere
kilichopo Jijini Dar es Salaam.







