Thursday, July 2, 2026

SERIKALI YARIDHISHWA NA MAENDELEO YA MIRADI YA NYUMBA ZA WATUMISHI WA UMMA KIGOMA

 Na. Antonia Mbwambo–Kigoma

Tarehe 2 Julai, 2026

Serikali imeeleza kuridhishwa na Maendeleo ya utekelezaji wa mradi wa Ujenzi wa Nyumba za Watumishi wa Umma Awamu ya Pili katika Mkoa wa Kigoma kufuatia ukaguzi uliofanywa na timu ya Wataalamu kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kushirikiana na Watumishi Housing Investimentsl.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini Bw. Patrick Allute, wakati wakihitimisha ziara ya ukaguzi wa miradi ya makazi ya Watumishi wa Umma Mkoani Kigoma ambapo timu ilikagua mradi ya nyumba za Watumishi katika Shule ya Sekondari Muhunga, Wilaya ya Kasulu, na Kituo cha Afya Muyama, Wilaya ya Buhigwe,Mkoa wa Kigoma

Akizungumza baada ya kuhitimisha ziara hiyo, Bw. Allute amepongeza wasimamizi wa mradi, Watumishi Housing na Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa usimamizi unaowezesha miradi hiyo kutekelezwa kwa ufanisi. Amesema hatua iliyofikiwa inaakisi dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuboresha mazingira ya kazi na ustawi wa Watumishi wa Umma.

Aidha, ameutaja mradi wa nyumba za Watumishi katika Kituo cha Afya Muyama kuwa miongoni mwa miradi iliyofanya vizuri zaidi kati ya miradi 15 iliyokaguliwa katika Mikoa mbalimbali ya Tanzania kutokana na kasi ya utekelezaji na ubora wa kazi inayoendelea kuonekana.

"Mradi wa nyumba za Watumishi katika Kituo cha Afya Muyama umeonesha kiwango cha juu cha utekelezaji. Kazi nyingi muhimu, ikiwemo mfumo wa umeme, zimekamilika na mradi umebakiza hatua chache kabla ya kukamilika na kuanza kutumika," amesema Bw. Allute.

Kwa upande wake, Msimamizi wa Mradi wa Kituo cha Afya Muyama ameishukuru timu ya ukaguzi kwa ushauri na maelekezo yaliyotolewa, akisema yataendelea kufanyiwa kazi ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati na kuanza kutoa huduma kwa Watumishi wa Umma waliokusudiwa kunufaika nao.

 

Wataalamu kutoka Ofisi ya Rais–UTUMISHI na Watumishi Housing Investment (WHI) wakijadili jambo mara baada ya kufanya ukaguzi wa utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa Kituo cha Afya Muyama, Wilaya ya Buhigwe, Mkoani Kigoma

Timu ya wataalamu kutoka Ofisi ya Rais–UTUMISHI na Watumishi Housing Investment (WHI) wakiwa katika picha ya pamoja na Kaimu Mganga Mfawidhi Kituo cha Afya Muyama Bw. Kwima Juma Buanza (wa tatu kutoka kushoto), mara baada ya timu hiyo kukamilisha ukaguzi wa mradi wa ujenzi wa nyumba za watumishi wa kituo hicho kiiilichopo Wilaya ya Kasulu, Mkoa wa Kigoma.


Muonekano wa nyuma wa jengo la mradi wa makazi ya Watumishi wa Umma wa Kituo cha Afya Muyama kwenye Wilaya ya Buhigwe Mkoa wa Kigoma

Mkurugenzi wa Fedha na Uwekezaji kutoka Watumishi Housing Investiment (WHI) Bw. Paskali Massawe (aliyenyoosha mkono) akielezea jambo kwa Wataalamu alioambatana nao katika ukaguzi wa mradi wa ujenzi wa Kituo cha Afya Muyama, Wilaya ya Buhigwe, Mkoani Kigoma, mara baada ya kufika kwenye eneo hilo Julai 2, 2026 

Wataalamu kutoka Ofisi ya Rais–UTUMISHI na Watumishi Housing Investment (WHI) wakijadili jambo mara baada ya kufanya ukaguzi wa utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa nyumba za makazi ya Watumishi wa Shule ya Sekondari Muhunga iliyopo Wilaya ya Kasulu, Mkoa wa Kigoma.

Mkurugenzi wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, kutoka Ofisi ya Rais-UTUMISHI Bw. Patrick Allute (wa tano kushoto) akiteta jambo na Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Mipango na Bajeti, wa Ofisi hiyo, Bi. Julieth Magambo wakati wa ukaguzi wa mradi wa ujenzi wa nyumba ya makazi ya watumishi wa Shule ya Sekondari Muhunga iliyopo Wilaya ya Kasulu, Mkoa wa Kigoma.

Wataalamu kutoka Ofisi ya Rais–UTUMISHI na Watumishi Housing Investment (WHI) wakijadili jambo mara baada ya kufanya ukaguzi wa utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa nyumba za makazi ya Watumishi wa Shule ya Sekondari Muhunga iliyopo Wilaya ya Kasulu, Mkoa wa Kigoma.

Mkurugenzi wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, Bw. Patrick Allute, (aliyenyoosha mikono), akitoa maelekezo kwa Makamu Mkuu wa Shule ya Sekondari Muhunga Mwl. Beatus Damiani,(wa pili kutoka kushoto) wakati wa ukaguzi wa SHule hiyo iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu Mkoa wa Kigoma, leo tarehe 2 Julai, 2026.

Muonekano wa mbele wa jengo la mradi wa makazi ya Watumishi wa Umma Shule ya Sekondari Muhunga iliyopo Wilaya ya Kasulu, Mkoa wa Kigoma.


Mkurugenzi wa Kitengo cha Ufuatiliaji na Tathmini, kutoka Ofisi ya Rais-UTUMISHI Bw. Patrick Allute (wanne kutoka kushoto) akiagana na Kaimu Afisa Elimu Sekondari, Halmashauri ya Mji wa Kasulu Mwl. Jeremiah Ntiboneka mara baada ya Timu ya Wataalamu kutoka Ofisi ya Rais–UTUMISHI na Watumishi Housing Investment (WHI) kukagua mradi wa ujenzi wa Shule ya Sekondari Muhunga iliyopo Wilaya ya Kasulu, Mkoa wa Kigoma.

No comments:

Post a Comment