Na. Veronica Mwafisi-Nzega
Tarehe 08 Julai, 2026
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya
Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete amezindua nyumba mbili
za Wakuu wa Idara katika Halmashauri ya Mji Nzega na kuwasisitiza kufanya kazi
kwa bidii na weledi katika kuwatumikia wananchi.
Mhe. Kikwete ameyasema hayo leo tarehe 08
Julai, 2026 alipokuwa akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya Mji Nzega
baada ya kuzindua ujenzi wa nyumba hizo zilizojengwa jirani na ofisi za
Halmashauri hiyo.
“Tunayoyaona hapa ni ushuhuda tosha kwamba
Serikali imekuwa ikiwajali watumishi wake, nyumba hizi zimejengwa kwa ustadi wa
hali ya juu, ni nzuri sana, ziko kwenye mazingira mazuri, haya yanatekelezwa
ili mfanye kazi kwa bidii,” amesisitiza.
Amesema amekuwa akipata barua za mara kwa
mara za watumishi wanaoomba uhamisho, “hali hii hainifurahishi hata kidogo na
ndio maana Serikali imekuwa ikijitahidi kuweka mazingira mazuri ili mtulie
kwenye vituo vyenu vya kazi, ukikaa kwenye nyumba kama hii huwezi kufikiria
kuhama,” amesema.
Amesema Serikali imekuwa ikishughulikia
changamoto mbalimbali za watumishi ili waweze kutoa huduma bora kwa umma,
akitolea mfano upandishwaji wa madaraja na malipo ya stahiki mbalimbali, huku
akiwasisitiza waajiri kulipa madai ya watumishi na kuongeza kuwa Serikali
itaendelea kuwajali Watumishi wa Umma wakati wote.
Ameongeza kuwa, maelekezo ya Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.
Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha watumishi wanatatuliwa changamoto
zinazowakabili ili waweze kuwatumikia wananchi kwa ufasaha, hivyo hakuna sababu
ya Waajiri kutoshughulikia changamoto za watumishi.
Mhe. Kikwete yuko katika ziara ya kikazi ya
siku tatu aliyoianza leo mkoani Tabora ambapo ametembelea katika Halmashauri ya
Wilaya ya Igunga na Halmashauri ya Mji Nzega kwa lengo la kukagua shughuli za
maendeleo katika halmashauri hizo ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi wa
Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2025.
Waziri
wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.
Ridhiwani Kikwete (aliyevaa shati jeupe) akipiga makofi mara baada ya kuzindua nyumba mbili za Wakuu wa Idara katika Halmashauri ya Mji
Nzega wakati wa ziara yake ya kikazi
iliyolenga kukagua na kuzindua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo
mkoani Tabora. Wengine ni Viongozi na Watendaji wa mkoa huo.
Mwonekano wa nyumba mojawapo ya Wakuu wa Idara iliyojengwa katika Halmashauri
ya Mji Nzega mkoani Tabora.
Viongozi,
Watendaji na Wananchi wa Halmashauri ya Mji
Nzega wakishuhudia uzinduzi wa nyumba mbili (hazipo pichani) za Wakuu wa Idara
katika Halmashauri hiyo wakati Waziri wa Nchi, Ofisi
ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani
Kikwete alipozizindua baada ya
kuzikagua wakati wa ziara yake ya kikazi mkoani Tabora.
Waziri
wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.
Ridhiwani Kikwete (wapili kutoka kushoto) akifurahia jambo wakati akikagua
nyumba za Wakuu wa Idara katika Halmashauri
ya Nzega wakati wa ziara yake ya kikazi
iliyolenga kukagua na kuzindua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo
katika Halmashauri hiyo mkoani Tabora. Wa
kwanza kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Nzega, Mhe. Naitapwaki Tukai.
Waziri
wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.
Ridhiwani Kikwete (aliyevaa shati jeupe meza kuu) akipokea taarifa kuhusu
utekelezaji wa ujenzi wa nyumba mbili za Wakuu wa Idara katika Halmashauri ya Nzega wakati wa ziara yake ya kikazi
iliyolenga kukagua na kuzindua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo
katika Halmashauri hiyo mkoani Tabora.



No comments:
Post a Comment