Saturday, February 25, 2023

VIONGOZI MAMLAKA ZA SERIKALI ZA MITAA WATAKIWA KUTATUA CHANGAMOTO ZINAZOKWAMISHA WANANCHI KUPATA HUDUMA BORA

 Na. James K. Mwanamyoto-Dodoma

Tarehe 26 Februari, 2023

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Deogratius Ndejembi amewataka Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mikoa na Wakuu wa Idara za Utawala na Rasilimaliwatu katika halmashauri kutatua changamoto zinazokwamisha wananchi kupata huduma bora pindi wanapofuata huduma katika maeneo yao ya kazi.

Mhe. Ndejembi ametoa wito huo jijini Dodoma, wakati akifunga kikao kazi cha Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mikoa na Wakuu wa Idara za Utawala na Rasilimaliwatu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kilichofanyika kwa siku tatu katika ukumbi wa Jiji la Dodoma uliopo Mji wa Serikali Mtumba.

Mhe. Ndejembi amesema, viongozi hao wanapaswa kukerwa na changamoto zinazowakabili wananchi pindi wanapofuata huduma katika maeneo yao ya kazi na kuchukua hatua stahiki ya kuwahimiza watendaji wanaowasimamia kuhakikisha wanatoa huduma bora kwa wananchi.

Mhe. Ndejembi amewahimiza viongozi hao, ambao wengi wao wanatoka maeneo ya pembezoni kuhakikisha wanasimamia vema rasilimaliwatu ili wananchi wapate huduma bora, kwani wananchi wengi waishio pembezoni mwa nchi wanalazimika kutumia gharama kubwa kufuata huduma kwenye ofisi za makao makuu ya mikoa na halmashauri za wilaya.

Aidha, Mhe. Ndejembi amewataka viongozi hao kutatua changamoto zinazowakabili watumishi ili wasiwe na sababu ya kutotoa huduma bora kwa wananchi na kuongeza kuwa, anaamini viongozi hao wanatambua wajibu wao katika kutatua kero za watumishi na wananchi kwa ujumla.

“Kuna changamoto ambazo mnahitaji kuwasikiliza tu watumishi au wananchi na kutoa majibu sahihi, lakini mmekuwa na tabia ya kukwepa jukumu hilo na kulielekeza kwa Katibu Mkuu-UTUMISHI jambo ambalo si sahihi kwani lipo ndani ya mamlaka zenu na uwezo wenu kiutendaji,” Mhe. Ndejembi amesisitiza.

Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Utawala na Rasilimaliwatu wa Halmashauri ya Mji Handeni, Bw. Steven Bavu amesema watahakikisha wanatekeleza agizo la Mhe. Ndejembi la kutatua kero za wananchi katika maeneo yao ya kazi.

Naye, Mkuu wa Idara ya Utawala na Rasilimaliwatu wa Halmashauri ya Wilaya ya Rombo, Bi. Judith Mahende amesema Mhe. Ndejembi amewahimiza kutatua kero za wananchi kwasababu katika Serikali za Mitaa ndio kuna wananchi wengi wanaowasilisha changamoto ili zitatuliwe, hivyo watatenga muda wa kuwatembelea na kuwasikiliza ili kutatua changamoto zinazowakabili.

Kikao kazi hicho kilicholenga kuhimiza uwajibikaji kwa Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mikoa na Wakuu wa Idara za Utawala na Rasilimaliwatu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kilifunguliwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Mhe. Anjela Kairuki na kufungwa na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora Mhe. Deogratius Ndejembi kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-UTUMISHI na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akizungumza na Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mikoa na Wakuu wa Idara za Utawala na Rasilimaliwatu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa wakati akifunga kikao kazi cha viongozi hao jijini Dodoma kilicholenga kuboresha utendaji kazi wao.


Sehemu ya Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mikoa na Wakuu wa Idara za Utawala na Rasilimaliwatu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (hayupo pichani) wakati akifunga kikao kazi chao jijini Dodoma kilicholenga kuboresha utendaji kazi wao.


Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi kufunga kikao kazi cha Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mikoa na Wakuu wa Idara za Utawala na Rasilimaliwatu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kilichofanyika jijini Dodoma kwa lengo la kuboresha utendaji kazi katika Utumishi wa Umma.


Mkurugenzi Msaidizi wa Idara Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Sekretarieti ya Mkoa wa Singida, Bw. Pancras Kakwere ambaye alikuwa Mwenyekiti wa kikao kazi cha Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mikoa na Wakuu wa Idara za Utawala na Rasilimaliwatu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa akitoa neno la shukrani mara baada ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi kufunga kikao kazi kikao kazi chao kilicholenga kuboresha utendaji kazi wao.


Mkuu wa Idara ya Utawala na Rasilimaliwatu, Halmashauri ya Mji Handeni, Bw. Steven Bavu akielezea namna watakavyotekeleza maelekezo ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi aliyoyatoa wakati akifunga kikao kazi cha Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mikoa na Wakuu wa Idara ya Utawala na Rasilimaliwatu katika Serikali za Mitaa kilicholenga kuboresha utendaji kazi wao.

 


Mkuu wa Idara ya Utawala na Rasilimaliwatu, Wilaya ya Rombo, Bi. Judith Mahende akiahidi kutekeleza maelekezo ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi aliyoyatoa wakati akfunga kikao kazi cha Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mikoa na Wakuu wa Idara ya Utawala na Rasilimaliwatu katika Serikali za Mitaa kilicholenga kuboresha utendaji kazi wao.

 



No comments:

Post a Comment