Saturday, February 18, 2023

MHE. NDEJEMBI AZITAKA TAASISI ZA UMMA KUISHIRIKISHA eGA KUTENGENEZA MIFUMO YA TEHAMA ILI ITOE HUDUMA BORA KWA UMMA

 Na. Veronica E. Mwafisi-Iringa

Tarehe 18 Februari, 2023

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Deogratius Ndejembi amezitaka Taasisi za umma nchini kuishirikisha Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) kutengeneza mifumo ya TEHAMA ya utoaji huduma kwa umma ili iweze kukidhi mahitaji na viwango katika kutoa huduma bora kwa wananchi.

Mhe. Ndejembi ametoa maelekezo hayo alipotembelea ofisi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini kwa lengo la kukagua utendaji kazi wake na kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi wa ofisi hiyo.

Mhe. Ndejembi amesema, Mamlaka ya Serikali Mtandao ipo tayari kushirikiana na taasisi za umma kusanifu mifumo, hivyo amezihimiza taasisi zote zenye nia ya kutengeneza mifumo, kuhakikisha zinaishirikisha eGA ili kutimiza malengo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwa na serikali ya kidijitali.

 “Taasisi za umma itumieni Mamlakaka ya Serikali Mtandao (eGA) ipasavyo kutengeneza mifumo itakayokidhi viwango vya kutoa huduma bora kwa wananchi kwa lengo la kutimiza azma ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuwa na serikali mtandao,” Mhe. Ndejembi amesisitiza.

Akizungumzia maeneo ambayo jiografia yake haipo vizuri, Mhe. Ndejembi amesema maeneo hayo yanapaswa kuwa na miundombinu ya TEHAMA itakayowezesha upatikanaji wa huduma za kimtandao zilizosanifiwa na Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA).

Katika kukabiliana na changamoto za kijiografia zinazokwamisha utoaji huduma kwa umma, Mhe. Ndejembi ametoa wito kwa eGA kutumia ubunifu na weledi wake kusanifu mifumo itakayorahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) Mhandisi Benedict Ndomba amesema kuwa, taasisi za serikali 14 zimehifadhi mifumo yake katika kituo kilichopo Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini ambapo jumla ya mifumo 189 imehifadhiwa ikiwemo GePG, GMS, e-office, e-vibali, m-government na mingineyo.

Mhandisi Ndomba amesema, Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) kupitia mpango mkakati wa 2021/2022 hadi 2025/2026 imejipanga kuongeza vituo vya ubunifu vingine zaidi ili kuboresha utoaji huduma kwa taasisi za umma zinazotaka kutengeneza mifumo ya TEHAMA.

Aidha, Mhandisi Ndomba, amemshukuru Naibu Waziri Ndejembi kwa kutembelea Ofisi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao Kanda ya Nyanda za Juu Kusini mkoani Iringa kwa lengo la kukagua utendaji kazi wake na kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi wa ofisi hiyo.

Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) ni taasisi ya umma iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Serikali Mtandao Na. 10 ya mwaka 2019, kwa lengo la kuratibu, kusimamia na kukuza jitihada za Serikali Mtandao pamoja na kuhimiza utekelezaji wa Sera, Sheria, Kanuni, Viwango na Miongozo ya Serikali Mtandao katika taasisi za umma.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akizungumza na watumishi wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini mkoani Iringa alipotembelea ofisi hiyo kwa lengo la kukagua utekelezaji wa majukumu na kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi hao.

Sehemu ya watumishi wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (meza kuu katikati) wakati akizungumza nao kwenye ofisi hiyo mkoani Iringa kwa lengo la kukagua utekelezaji wa majukumu na kuhimiza uwajibikaji.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) Mhandisi Benedict Ndomba (aliyesimama) akielezea majukumu ya taasisi yake kwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (katikati) kabla ya Naibu Waziri huyo kuzungumza na watumishi wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini mkoani Iringa alipotembelea ofisi hiyo kwa lengo la kukagua utekelezaji wa majukumu na kuhimiza uwajibikaji.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (katikati) akimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) Mhandisi Benedict Ndomba (wa kwanza kulia) wakati akifafanua jambo kwa Naibu Waziri huyo alipotembelea ofisi ya Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini mkoani Iringa kwa lengo la kukagua utekelezaji wa majukumu na kuhimiza uwajibikaji.






 

No comments:

Post a Comment