Tuesday, October 11, 2022

MHE. JENISTA ATOA WITO KWA WAJASIRIAMALI MKOANI ARUSHA KUTUMIA KITUO JUMUISHI CHA URASIMISHAJI NA UENDELEZAJI WA BIASHARA ILI KUKUZA BIASHARA ZAO NA KUONGEZA PATO LA TAIFA

Na. Veronica Mwafisi-Arusha

Tarehe 11 Oktoba, 2022.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama ametoa wito kwa wafanyabiashara ndogondogo mkoani Arusha kukitumia Kituo Jumuishi cha Urasimishaji na Uendelezaji wa Biashara kilichoanzishwa na Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge (MKURABITA) kwa kushirikiana na Halmashauri ya Jijiji la Arusha ili kukuza biashara zao na kuongeza pato la taifa nchini.

Mhe. Jenista ameyasema hayo wakati akizindua rasmi kituo hicho kilichopo katika Kata ya Kati, Mtaa wa Pangani, Halmashauri ya Jiji la Arusha.

Mhe. Jenista amesema kituo hicho kimeanzishwa mahususi kwa ajili ya kuwasaidia wajasiriamali hao kujifunza mambo mbalimbali pamoja na kupatiwa mbinu tofauti za kibiashara hivyo ni fursa kwao kukitembelea ili kupata huduma hiyo.

“Kituo hiki kitasaidia kurasimisha biashara zenu na kuweza kutambulika na taasisi za kifedha ili muweze kupata mikopo katika taasisi hizo kwa lengo la kuinua biashara zenu kwa maendeleo yenu binafsi na taifa kwa ujumla,” Mhe. Jenista amesisitiza

Katika kuhakikisha wajasiriamali hao wanapata huduma bora katika kituo hicho, Waziri Jenista amezitaka taasisi zote zinazotoa huduma jumuishi kushiriki kikamilifu kutoa huduma ili wafanyabiashara hao wasipate kadhia wanapoenda kupata huduma katika kituo hicho.

“Serikali kupitia MKURABITA imetumia fedha nyingi kuanzisha kituo hicho kikubwa chenye ubora, hivyo taasisi zote jumuishi zinatakiwa zitoe huduma na kuondoa kadhia kwa wafanyabiashara hao kwa kuwapatia huduma inayostahili kama ilivyokusudiwa,” Mhe. Jenista amesisitiza.

Ameongeza kuwa maono ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ni kuona wamiliki wa ardhi na biashara ndogondogo wanapiga hatua kubwa ya maendeleo kwa kupata mikopo ya kuanzisha shughuli mbalimbali za kuwaongezea kipato.

Aidha, Mhe. Jenista amewataka watumishi wote wanaotoa huduma katika kituo hicho kuzingatia maadili katika utekelezaji wa majukumu yao ili kutoa huduma bora kwa walengwa wanaopata huduma katika kituo hicho.

“Kila mtumishi wa umma atakayefanya kazi katika kituo hicho atekeleze majukumu yake kwa kuzingatia maadili ya utumishi wa umma, tunataka watumishi wote wawe mfano wa kituo hiki na wananchi waone umuhimu wa kazi zinazofanywa na watumishi hao wa Jiji la Arusha,” Mhe. Jenista ameongeza.

Kwa upande wake, Mratibu wa MKURABITA, Dkt. Seraphia Mgembe amemhakikishia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kushirikiana na Halmashauri ya Jiji la Arusha katika mambo mbalimbali ya kuwawezesha wafanyabiashara hao ikiwemo katika kutoa mafunzo ili waweze kuendeleza biashara zao.

Kituo Jumuishi cha Urasimishaji na Uendelezaji wa Biashara kimeanzishwa ili kuwasaidia na kuwarahisishia wafanyabiashara wa Jiji la Arusha kupata huduma zote za ushauri wa biashara pamoja na kupata mahitaji yote ya kibiashara katika sehemu moja.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akifurahi pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Mhe. Said Mtanda (kushoto) na Watendaji wengine wa Serikali mara baada ya Waziri Jenista kuzindua rasmi kituo Jumuishi cha Urasimishaji na Uendelezaji wa Biashara kilichopo katika Kata ya Kati, Mtaa wa Pangani Halmashauri ya Jiji la Arusha


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akizungumza na baadhi ya watumishi wanaotoa huduma katika kituo Jumuishi cha Urasimishaji na Uendelezaji wa Biashara kilichopo katika Kata ya Kati, Mtaa wa Pangani Halmashauri ya Jiji la Arusha mara baada ya Waziri huyo kuzindua rasmi kituo hicho


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akizungumza na wajasiriamali wanaopata huduma katika kituo Jumuishi cha Urasimishaji na Uendelezaji wa Biashara kilichopo katika Kata ya Kati, Mtaa wa Pangani Halmashauri ya Jiji la Arusha alipokuwa akizindua rasmi kituo hicho akiwa katika ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa shughuli za MKURABITA mkoani Arusha.




Baadhi ya wajasiriamali wanaopata huduma katika kituo Jumuishi cha Urasimishaji na Uendelezaji wa Biashara kilichopo katika Kata ya Kati, Mtaa wa Pangani Halmashauri ya Jiji la Arusha wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama alipokuwa akizungumza nao mara baada ya Waziri huyo kuzindua rasmi kituo Jumuishi cha Urasimishaji na Uendelezaji wa Biashara mkoani Arusha.


Mkuu wa Wilaya ya Arusha, Mhe. Said Mtanda akitoa maelezo ya awali kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kuzindua rasmi kituo Jumuishi cha Urasimishaji na Uendelezaji wa Biashara kilichopo katika Kata ya Kati, Mtaa wa Pangani Halmashauri ya Jiji la Arusha.


Kaimu Mkurugenzi wa Jiji la Arusha, Bw. Hargeney Chitukuro akiwasilisha taarifa ya utekelezaji ya kituo Jumuishi cha Urasimishaji na Uendelezaji wa Biashara kilichopo katika Kata ya Kati, Mtaa wa Pangani Halmashauri ya Jiji la Arusha kabla ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kuzindua rasmi kituo hicho.


Mratibu wa Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA), Dkt. Seraphia Mgembe akielezea majukumu ya taasisi yake kabla ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kuzindua kituo Jumuishi cha Urasimishaji na Uendelezaji wa Biashara kilichopo katika Kata ya Kati, Mtaa wa Pangani Halmashauri ya Jiji la Arusha mkoani Arusha.

 


 

No comments:

Post a Comment