Tuesday, October 11, 2022

MHE. NDEJEMBI AWATAKA WATUMISHI KUTOHOFIA KUELEZA CHANGAMOTO WANAZOKABILIANA NAZO ILI ZITATULIWE KAMA MHE. RAIS ALIVYOELEKEZA

 Na. James K. Mwanamyoto - Lindi

Tarehe 11 Oktoba, 2022

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi amewataka watumishi wa umma nchini kutoogopa kuwasilisha changamoto zinazowakabili kwa kuwahofia waajiri kuwajengea chuki na kuwaahidi kuwa, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora itawalinda kwasababu Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan anataka kupata mrejesho utakaoiwezesha Serikali kuujenga Utumishi wa Umma wenye uadilifu na unaowajibika kwa masilahi ya taifa.

Mhe. Ndejembi ametoa wito huo kwa watumishi wa umma nchini, wakati akizungumza kwa nyakati tofauti na watumishi wa Sekretarieti ya Mkoa wa Lindi, Manispaa ya Lindi, Halmashauri ya Wilaya ya Mtama na wa taasisi za umma mkoani Lindi.

“Sisi viongozi tunaomsaidia Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kusimamia Utumishi wa Umma tunapowatembelea msiogope kuelezea changamoto zinazowakabili kwani tunakuja kuzitatua, hivyo tutawalinda na iwapo mtaogopa mtajinyima fursa ya kuwasilisha changamoto zenu ili zitatuliwe kama Mhe. Rais alivyoelekeza,” Mhe. Ndejembi amesisitiza.

Mhe. Ndejembi amesema Ofisi ya Rais-UTUMISHI haitosita kumchukulia hatua stahiki Afisa Utumishi au mwajiri atakayebainika kumuonea mtumishi aliyejitokea kuwasilisha changamoto zinazomkabili.

Akiwasilisha hoja kuhusu watumishi wa umma kupata changamoto ya kubadilishiwa miundo ya kiutumishi (recategorization), mmoja wa watumishi wa Idara ya Elimu Sekondari mkoani Lindi, Bw. Sharif Daudi Kiao amehoji ni kwanini mtumishi aliyejiendeleza kielimu kwa ajili ya kuutumikia umma pindi anapomuomba mwajiri kumbadilishia kada analazimika kushushwa mshahara wake ili apate sifa ya kukitumikia cheo kipya.

Akitoa ufafanuzi kuhusiana na hoja iliyowasilishwa na mtumishi huyo, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi ametoa ushauri kwa watumishi wa umma nchini pindi wanapotaka kujiendeleza kielimu kuhakikisha wanazingatia uhitaji wa mwajiri kwa wakati huo ili wakihitimu wawe na tija kiutendaji ambayo inamshawishi mwajiri  kumbadilishia kada (recategorization) ili aweze kutoa mchango katika Utumishi wa Umma.

Akizungumzia hoja ya mtumishi anayeomba kubadilishiwa kada kulazimika kushushwa mshahara wake, Mhe. Ndejembi ameeleza kuwa kwa watumishi wanaojiendeleza ndani ya kada zao kama vile Afisa Kilimo Msaidizi (Diploma) kuwa Afisa Kilimo (Degree) wakibadilishwa kada wanaombewa kibali cha mshahara binafsi, lakini kwa yule atakayeomba kubadilishiwa kada kwa ajili ya kukidhi matilaba binafsi (job satisfication) atalazimika kuanza na cheo cha kuingilia  na mshahara wa cheo kipya kwa kada husika na atakuwa amekosa sifa ya kuombewa kibali cha mshahara binafsi.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi yuko mkoani Lindi kwa ajili ya ziara ya kikazi ya siku tatu, inayolenga kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa umma  mkoani humo ikiwa ni pamoja na kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kuzinusuru Kaya Maskini  unaoratibiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) nchini.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb) akizungumza na watumishi wa Sekretarieti ya Mkoa wa Lindi, Manispaa ya Lindi na wa taasisi za umma mkoani Lindi (hawapo pichani) wakati wa ziara yake ya kikazi mkoani Lindi yenye lengo la kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa umma.


Baadhi ya watumishi wa Sekretarieti ya Mkoa wa Lindi, Manispaa ya Lindi na wa taasisi za umma mkoani Lindi wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (hayupo pichani) wakati wa ziara yake ya kikazi mkoani Lindi iliyolenga kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa umma.


Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Mhe. Shaibu Ndemanga akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb) kuzungumza na watumishi wa Sekretarieti ya Mkoa wa Lindi, Manispaa ya Lindi na wa taasisi za umma wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo mkoani Lindi yenye lengo la kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa umma.


Mmoja wa watumishi wa Idara ya Elimu Sekondari mkoani Lindi, Bw. Sharif Daudi Kiao akiwasilisha changamoto ya kiutumishi kwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb) wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo mkoani Lindi iliyolenga kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa umma mkoani humo.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb) akitoa ufafanuzi wa masuala ya kiutumishi kwa watumishi wa Sekretarieti ya Mkoa wa Lindi, Manispaa ya Lindi na wa taasisi za umma mkoani humo wakati wa kikao kazi chake na watumishi hao kilicholenga  kutatua changamoto zinazowakabili watumishi hao.



Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (kulia) akiteta jambo na Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Mhe. Shaibu Ndemanga wakati wa kikao kazi cha Naibu Waziri huyo na watumishi wa Sekretarieti ya Mkoa wa Lindi, Manispaa ya Lindi na wa taasisi za umma kilicholenga kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa umma mkoani Lindi.



No comments:

Post a Comment