Monday, October 24, 2022

RAIS SAMIA AMEDHAMIRIA KUTOA MAFUNZO YA UONGOZI KWA VIONGOZI ILI WAMSADIE KATIKA KUWATUMIKIA VEMA WANANCHI NA KULETA MAENDELEO

Na. James K. Mwanamyoto-Dodoma

Tarehe 24 Oktoba, 2022

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama amesema, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan tangu aingie madarakani amedhamiria kuendelea kutoa kipaumbele cha kuwapatia mafunzo viongozi ili kuwajengea uwezo kiutendaji, utakaowawezesha kumsaidia vema jukumu la kuwatumikia wananchi na kuleta maendeleo.

Mhe. Mhagama ameeleza dhamira hiyo ya Mhe. Rais, wakati akifunga mafunzo ya Sanaa ya Uongozi (The Art of Leadership) kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa (USEMI) yaliyotolewa na Taasisi ya UONGOZI jijini Dodoma.

Mhe. Mhagama amesema, mara baada ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kuapa na kuanza kulitumikia taifa, moja ya eneo ambalo alielekeza lipewe kipaumbele ni kutoa mafunzo kwa viongozi akitambua kuwa mafunzo ndio njia pekee ya kuwawezesha viongozi kuwa na ufanisi kiutendaji, hivyo ofisi yake imetekeleza kwa vitendo agizo hilo kwa kuwapatia mafunzo wajumbe wa kamati ya USEMI.

“Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ana maono na ndio maana anatambua kuwa sisi tuliopewa dhamana ya kuwa viongozi tunahitaji kujengewa uwezo ili kupata ujuzi utakaoendana na mazingira yaliyopo ikiwa ni pamoja na kwenda sambamba na maendeleo ya teknolojia,” Mhe. Mhagama amefafanua.

Kwa upande wake, mmoja wa Wajumbe wa Kamati ya USEMI, ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Makete, Mhe. Festo Sanga amesema toka awe Mbunge hajawahi kupata mafunzo mazuri ya uongozi kama ambayo Taasisi ya UONGOZI imewapatia kwani yamemjengea uelewa kwenye eneo la akili hisia (emotional intelligence) utakaomuwezesha kuzungumza vizuri na wananchi na kupokea yale ambayo wananchi anaowaongoza wanahitaji kutekelezewa.

“Mafunzo haya kama Mbunge na Mjumbe wa kamati ya USEMI yamekuwa na manufaa makubwa kwani yamenipatia elimu ya namna ya kuisaidia Serikali katika ufuataliaji wa utekelezaji wa  miradi mbalimbali ya maendeleo, pamoja  na kusimamia matumizi ya fedha za umma ambazo  Serikali ya Awamu ya Sita imekuwa ikizitoa katika maeneo mbalimbali nchini ili kuleta maendeleo,” Mhe. Sanga amesisitiza.

Naye, Dkt. Alice Kaijage (Mb) ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya USEMI amesema kuwa, kwa ujumla wajumbe wote wa kamati ya USEMI waliopatiwa mafunzo wameridhika na maudhui ya mafunzo na kushauri yaendelee kutolewa kwa muda mrefu zaidi ili viongozi wapate ujuzi utakaowaongezea ufanisi kiutendaji.

Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa (USEMI) wamepatiwa Mafunzo ya Sanaa ya Uongozi  (The Art of Leadership) na  Taasisi ya UONGOZI  kwa muda wa siku mbili, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ya kuitaka taasisi hiyo kuendelea kuwajengea uwezo viongozi ili wawe na tija katika maendeleo ya taifa.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akifunga mafunzo ya Sanaa ya Uongozi (The Art of Leadership) kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge na Utawala na Serikali za Mitaa (USEMI) yaliyotolewa na Taasisi ya UONGOZI jijini Dodoma. 


Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Michael Mwakamo (wa kwanza kushoto) akiwa na baadhi ya Wajumbe wa Kamati ya USEMI, wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama (hayupo pichani) wakati Waziri huyo akifunga mafunzo ya Sanaa ya Uongozi (The Art of Leadership) yaliyotolewa na Taasisi ya UONGOZI kwa wajumbe wa kamati hiyo jijini Dodoma. 


Sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa (USEMI) wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama (aliyesimama) wakati waziri huyo akifunga mafunzo ya Sanaa ya Uongozi (The Art of Leadership) yaliyotolewa na Taasisi ya UONGOZI jijini Dodoma. 


Mjumbe wa Kamati ya USEMI ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Makete, Mhe. Festo Sanga akieleza faida ya mafunzo ya Sanaa ya Uongozi (The Art of Leadership), waliyopatiwa na Taasisi ya UONGOZI jijini Dodoma kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kiutendaji. 


Mjumbe wa Kamati ya USEMI,  Dkt. Alice Kaijage akieleza namna  wajumbe wa Kamati ya USEMI walivyonufaika na Mafunzo ya Sanaa ya Uongozi (The Art of Leadership), waliyopatiwa na Taasisi ya UONGOZI jijini Dodoma kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kiutendaji. 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Kamati ya USEMI na baadhi ya Watendaji wa Serikali, mara baada ya waziri huyo kufunga mafunzo ya Sanaa ya Uongozi (The Art of Leadership) yaliyotolewa na Taasisi ya UONGOZI kwa wajumbe wa kamati hiyo jijini Dodoma. 


 

No comments:

Post a Comment