Thursday, October 13, 2022

KAMATI ZA NIDHAMU ZATAKIWA KUHITIMISHA KWA WAKATI MASHAURI YA KINIDHAMU YA WATUMISHI ILI KUIPUNGUZIA GHARAMA SERIKALI

Na. Veronica Mwafisi - Arumeru

Tarehe 13 Oktoba, 2022

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama amezitaka Kamati za Nidhamu kuhitimisha kwa wakati mashauri ya kinidhamu ya watumishi wa umma ili kuipunguzia serikali gharama kubwa ambayo imekuwa ikiingia kwa kuwalipa mishahara watumishi waliopoteza sifa ya kuendelea kuwa watumishi, ikiwa ni pamoja kupunguza gharama za kuendesha mashauri ya kinidhamu kwa muda mrefu.

Akizungumza na watumishi wa Halmashauri za Wilaya ya Arusha na Meru wakati wa ziara yake ya kikazi Wilayani Arumeru, Mhe. Jenista amesema Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kuwalipa watumishi ambao pengine baada ya kuhitimishwa kwa mashauri yao wanatakiwa kuondolewa katika utumishi wa umma.

“Naziagiza Kamati za Nidhamu zote nchini kuhakikisha mashauri yote ya kinidhamu ya watumishi wa umma yanahitimishwa kwa wakati kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu zilizopo ili haki itendeke, kwani Serikali imekuwa ikiwagharamia watumishi ambao wameshapoteza sifa ya kuwa watumishi wa umma na wanalazimika kutofanya kazi yoyote pindi wanaposubiri hatma ya mashauri yao,” Mhe. Jenista amesisitiza.

Ameongeza kuwa,  mtumishi anapotuhumiwa kuwa na kosa la kinidhamu na kufunguliwa  shauri la kinidhamu, hatima yake ni aidha kuondolewa katika utumishi wa umma au kuendelea na utumishi wa umma, hivyo ni vema Kamati ziwe na utamaduni wa kuharakisha mchakato wa uendeshaji wa mashauri ya kinidhamu ili kuokoa fedha za serikali ambazo zitakazotumika kuboresha huduma mbalimbali za kijamii.

Aidha, Mhe. Jenista amewataka watumishi wa umma kufanya kazi kwa uadilifu, ubunifu na weledi katika utekelezaji wa majukumu yao ili kuwa na   tija katika maendeleo ya taifa.

Waziri Jenista amesema, kila mtumishi kwa nafasi yake anao uwezo mkubwa wa kuitumia taaluma yake katika kuchangia maendeleo ya taifa na ndio maana Serikali ya Awamu ya Sita inaendelea kuboresha maslahi yao ili kuwajengea morali ya utendaji kazi.

“Lengo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan ni kuona taifa lake linapata maendeleo makubwa na sisi watumishi kila mmoja kwa nafasi yake tunaowajibu wa kuhakikisha tunatimiza ndoto ya Mhe. Rais,” Mhe. Jenista amesisitiza.

Akimkaribisha Mhe. Jenista kuzungumza na watumishi wa Halmashauri za Wilaya ya Arusha na Meru, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. John Mongella amemshukuru na kumpongeza Mhe. Jenista kwa kuwa na utaratibu wa kufanya vikao kazi na watumishi wa umma ili kutatua changamoto zao na kuhimiza uwajibikaji.

Mhe. Mongella amesema, mafanikio makubwa yanayopatikana nchini hivisasa yanatokana na uchapakazi wa watumishi wa umma ambao unachagizwa na watumishi kuridhishwa na namna serikali inavyowajali hivyo kuwaongezea morali ya kufanya kazi kwa bidii.

Waziri Jenista ameendelea na ziara yake ya kikazi mkoani Arusha inayolenga kutatua changamoto zinazowakabili, kuhimiza uwajibikaji na kukagua utekelezaji wa shughuli za Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge (MKURABITA).

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akizungumza na Watumishi wa Halmashauri za Wilaya ya Arusha na Meru wakati wa ziara yake ya kikazi wilayani Arumeru iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi hao.


Watumishi wa Halmashauri za Wilaya ya Arusha na Meru wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza nao wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri huyo wilayani Arumeru iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi hao.


Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. John Mongella akitoa salamu za mkoa wake kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kuzungumza na watumishi wa Halmashauri za Wilaya ya Arusha na Meru wakati wa ziara ya kikazi ya Mhe. Jenista wilayani Arumeru iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa wilayani humo.



Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Mhe. Mhandisi Richard Ruyango akitoa salamu za wilaya yake kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama wakati wa ziara ya kikazi ya Mhe. Jenista wilayani Arumeru iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa wilaya hiyo.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akiteta na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. John Mongella wakati wa ziara ya kikazi ya Mhe. Jenista wilayani Arumeru iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa wilaya hiyo.


Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru, Bi. Zainab Makwinya akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa halmashauri yake kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama wakati wa ziara ya kikazi ya Mhe. Jenista wilayani Arumeru iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa wilaya hiyo.


Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Arusha, Bw. Seleman Msumi akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa halmashauri yake kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama wakati wa ziara ya kikazi ya Mhe. Jenista wilayani Arumeru iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa wilaya hiyo.

 


 

No comments:

Post a Comment