Saturday, March 11, 2023

WATUMISHI OFISI YA RAIS-UTUMISHI WAENDELEA KUIMARISHA AFYA KWA MAZOEZI ILI KUTOA HUDUMA BORA KAMA ILIVYOELEKEZWA NA MHE. RAIS DKT. SAMIA SULUHU HASSAN

Na. James K. Mwanamyoto-Dodoma

Tarehe 11 Machi, 2023

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema utaratibu wa kufanya mazoezi unaoendelezwa na watumishi wa ofisi yake ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuimarisha afya ili kuweza kutoa huduma bora kwa wananchi.

Mhe. Kikwete amesema hayo jijini Dodoma, mara baada ya kumaliza kuwaongoza watumishi wa ofisi yake kufanya mazoezi ya kuimarisha afya zao yaliyofanyika katika eneo la Ofisi ya Rais-UTUMISHI lililopo Mji wa Serikali, Mtumba jijini Dodoma.

Mhe. Kikwete amesema, ofisi yake inatekeleza kwa vitendo maelekezo ya Rais wa Awamu ya Sita Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwataka watumishi wa umma wanapomaliza kutekeleza majukumu yao ya kila siku kutenga muda wa kufanya mazoezi ili kuimarisha afya ya akili na mwili kwa lengo la kuendelea kutekeleza majukumu yao kikamilifu pamoja na kutoa mchango katika ujenzi wa taifa.

Aidha, kupitia mazoezi hayo, Mhe. Kikwete ametoa wito kwa watumishi wote wa umma nchini kupitia taasisi zao kushiriki katika mazoezi ya kuimarisha afya zao ili waweze kutekeleza majukumu yao kikamilifu kwa maendeleo ya taifa.

“Watumishi wa umma wenzangu kuimarisha afya ni jambo la msingi, hivyo, tushiriki katika mazoezi ili afya zetu ziimarike na kuweza kufikia malengo yetu kiutendaji,” Mhe. Kikwete amesisitiza.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bw. Juma Mkomi amesema afya ni mtaji kwa mtumishi yeyote kwani bila kuwa na afya nzuri hakuna atakayeweza kutekeleza majukumu yake kikamilifu, hivyo ushiriki wa watumishi katika mazoezi ni jambo linalopaswa kupewa kipaumbele na waajiri pamoja na watumishi wa umma.

Bw. Mkomi amesema anaungana na Mhe. Ridhiwani Kikwete kuwasisitiza watumishi wote wa umma nchini kufanya mazoezi yatakayoimarisha afya zao ili kutoa huduma bora wananchi.

Uongozi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora umeweka utaratibu wa watumishi wake kushiriki mazoezi ya pamoja kila ijumaa ya wiki kwa kutambua umuhimu wa kuwa na rasilimaliwatu yenye tija katika utoaji wa huduma bora kwa wananchi na wadau wa masuala ya utumishi wa umma na utawala bora. 


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani akifurahia jambo na Katibu Mkuu wa ofisi yake Bw. Juma Mkomi, mara baada ya Naibu Waziri huyo kuongoza mazoezi ya kuimarisha afya za watumishi wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI yaliyofanyika katika ofisi iliyopo Mji wa Serikali, Mtumba jijini Dodoma.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani (mwenye nguo nyeusi ya mazoezi) akiongoza mazoezi ya kuimarisha afya za watumishi wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI yaliyofanyika katika ofisi iliyopo Mji wa Serikali, Mtumba jijini Dodoma.


Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bw. Juma Mkomi (wa pili kutoka kulia) akishiriki mazoezi ya viungo wakati Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani (hayupo pichani) akiongoza mazoezi ya kuimarisha afya za watumishi wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI yaliyofanyika katika ofisi iliyopo Mji wa Serikali, Mtumba jijini Dodoma.


Sehemu ya watumishi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, wakishiriki mazoezi ya kuimarisha afya yaliyoongozwa na Naibu Waziri wa ofisi hiyo Mhe. Ridhiwani (hayupo pichani) katika eneo la Ofisi ya Rais-UTUMISHI lililopo Mji wa Serikali, Mtumba jijini Dodoma.


 

No comments:

Post a Comment