Wednesday, March 2, 2022

MHE. NDEJEMBI ARIDHISHWA NA UJENZI WA KAMPASI YA TPSC SINGIDA NA KUITAKA MENEJIMENTI KUJENGA KATIKA KAMPASI ZOTE WANAZOPANGA

Na. James K. Mwanamyoto-Singida

Tarehe 2 Machi, 2022

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi ameipongeza Menejimenti ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) kwa kuanza ujenzi wa Kampasi ya Singida ambao utaokoa kiasi cha shilingi milioni 87 zinazolipwa kwa ajili ya kupanga jengo la kuendesha shughuli zake mkoani Singida.

Mhe. Ndejembi ametoa maelekezo hayo mkoani Singida wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa Kampasi ya TPSC Singida.

Mhe. Ndejembi amesema kitendo cha TPSC kuanza ujenzi wa Kampasi ya Singida ni maono ya kuondokana na gharama kubwa za upangaji wa jengo wanalolitumia hivi sasa katika kutekeleza majukumu ya chuo hicho mkoani Singida.

“Ni heri mlivyoamua kujinyima ili kutenga fedha zinazotumika kujenga jengo hili, uamuzi huu ni muafaka kwani utapunguza gharama za uendeshaji wa Kampasi hii,” Mhe. Ndejembi amefafanua.

Aidha, Mhe. Ndejembi kwa kutambua faida ya TPSC kumiliki majengo yake, ameilekeza Menejimenti ya chuo hicho kuangalia uwezekano wa kujenga majengo yao katika kampasi zote ambazo chuo kinagharamia kupanga.

“Ni wakati muafaka kwa menejimenti kuona namna bora ya kuanza ujenzi katika kampasi zote mnazopanga kama mnavyofanya katika Kampasi hii ya Singida.” Mhe. Ndejembi amesisitiza.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhandisi Paskasi Muragili ameipongeza Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na uongozi wa TPSC kwa uamuzi wa kuanza ujenzi wa Kampasi ya TPSC Singida ambayo itahudumia watumishi wa umma na wananchi wa mikoa ya Kanda ya Kati.

Mhandisi Muragili amesema eneo hilo linalojengwa Kampasi ya Singida lilitengwa muda mrefu sana, hivyo bila uamuzi wa dhati wa kuanza ujenzi huo, ni dhahiri kuwa ndoto ya TPSC Kampasi ya Singida kuwa na jengo lake isingetimia.

Akitoa taarifa ya maendeleo ya ujenzi wa Kampasi hiyo ya Singida, Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Dkt. Selemani Shindika amesema timu ya wataalam ilibainisha kuwa eneo hilo kutajengwa majengo 30 ili kuwezesha utekelezaji wa majukumu ya Kampasi ya TPSC Singida.

Dkt. Shindika amefafanua kuwa, kutokana na gharama za ujenzi wa majengo hayo 30 kuwa kubwa, TPSC iliamua kuwa na mpango wa ujenzi wa awamu kwa kutumia fedha za ndani mpaka ujenzi utakapokamilika.

Jumla ya ekari 76 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Kampasi ya Singida.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akiangalia mchoro wa jengo la Chuo cha Utumishi wa Umma, Kampasi ya Singida alipoenda kukagua maendeleo ya ujenzi wa Kampasi hiyo.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akitoa maelekezo kwa uongozi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa jengo la TPSC Kampasi ya Singida.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akizungumza na Watumishi wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC) na kamati ya ujenzi wa jengo la TPSC Kampasi ya Singida alipofanya ziara ya kikazi ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa Kampasi hiyo mkoani Singida.

Mkuu wa Chuo na Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Dkt. Selemani Shindika akiwasilisha taarifa ya utekelezaji ya ujenzi wa jengo la TPSC Kampasi ya Singida kwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo iliyolenga kukagua maendeleo ya ujenzi wa Kampasi hiyo mkoani Singida.

Mkuu wa Wilaya ya Singida, Mhandisi Paskasi Muragili akiishukuru Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kuanza ujenzi wa Chuo cha Utumishi wa Umma katika Mkoa wa Singida wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa Kampasi hiyo mkoani Singida.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akipata maelezo ya mchoro wa jengo la Chuo cha Utumishi wa Umma, Kampasi ya Singida toka kwa Mhandisi Daudi Adam alipofanya ziara ya kikazi ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa Kampasi hiyo mkoani Singida.

 


 

No comments:

Post a Comment