Friday, March 25, 2022

MHE. JENISTA AZINDUA MFUMO WA KIELEKTRONIKI UNAOISADIA SERIKALI KUPATA TAARIFA YA HALI YA RASILIMALIWATU KISAYANSI

 Na. James K. Mwanamyoto-Dodoma

Tarehe 25 Machi, 2022

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama, amezindua Mfumo wa Kielektroniki wa Tathmini ya Hali ya Rasilimaliwatu katika Utumishi wa Umma utakaoisaidia Serikali kupata taarifa sahihi ya hali ya rasilimaliwatu kisayansi ili kuwapangia vituo vya kazi watumishi kulingana na mahitaji ya huduma katika eneo husika.

Mhe. Jenista amesema uzinduzi wa mfumo huo alioufanya jijini Dodoma ni sehemu ya utekelezaji wa azma ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ya kutaka Serikali yake kuwa na mifumo ya kielektroniki itakayosimamia utendaji kazi wa watumishi na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Mhe. Jenista amethibitisha kuwa, mfumo huo umeshaanza kusaidia kukusanya, kuchakata na kuchambua taarifa za watumishi kwa njia ya kisayansi zaidi ambao unaiwezesha Serikali kutambua mahitaji halisi ya watumishi katika taasisi za umma.

“Mfumo huu utaisaidia Serikali kuwa na tathmini ya kisayansi ya hali ya watumishi wa umma waliopo na wanaohitajika kuwahudumia wananchi katika maeneo mbalimbali, hivyo Serikali ikakuwa na takwimu sahihi zinazopatikana kupitia mfumo huu niliouzindua,” Mhe. Jenista amefafanua.

Waziri Jenista amesema, mfumo huo pia utasaidia Serikali kubaini taasisi ambazo zina watumishi wa ziada ili kuwapeleka kwenye taasisi za umma ambazo zina upungufu mkubwa wa watumishi watakaowezesha kutoa huduma bora kwa wananchi.

Aidha, Mhe. Jenista amewasisitiza na kuwaagiza waajiri wote katika taasisi za umma kuhakikisha wanawasimamia wakurugenzi na wakuu wa idara zinazosimamia rasilimaliwatu, kukamilisha wajibu wao wa kuingiza taarifa za watumishi katika mfumo huo.

Mhe. Jenista amezitaka taasisi zote ambazo hazijakamilisha wajibu wa kuingiza taarifa za watumishi kwenye mfumo huo kuhakikisha zinakamilisha zoezi hilo kabla ama ifikapo tarehe 31 Machi, 2022 na kuongeza kuwa, taasisi zitakazoshindwa kukamilisha zoezi hilo zitakuwa zimekiuka maelekezo ya Serikali na zitachukuliwa hatua na mamlaka husika.

Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora inaendelea kusanifu na kujenga mifumo ya utendaji kazi ya TEHAMA itakayoongeza ufanisi wa taasisi za umma katika kutoa huduma bora kwa wananchi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akizungumza na viongozi wa Ofisi yake na Waandishi wa Habari wakati wa uzinduzi wa Mfumo wa Kieletroniki wa Tathmini ya Hali ya Watumishi wa Umma katika Taasisi za Umma uliofanyika jijini Dodoma.



Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Xavier Daudi akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kuzungumza na waandishi wa habari wakati wa uzinduzi wa Mfumo wa Kieletroniki wa Tathmini ya Hali ya Watumishi wa Umma katika Taasisi za Umma uliofanyika jijini Dodoma. Wakwanza kulia ni Mkurugenzi wa Idara ya TEHAMA Serikalini, Bw. Priscus Kiwango.


Baadhi ya Wakuu wa Idara na Vitengo wa Ofisi ya Rais – UTUMISHI wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama wakati wa uzinduzi wa Mfumo wa Kieletroniki wa Tathmini ya Hali ya Watumishi wa Umma katika Taasisi za Umma uliofanyika jijini Dodoma.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akiwaonesha waandishi wa habari   Taasisi zilizofanya vizuri na ambazo hazijafanya vizuri katika kuingiza taarifa kwenye Mfumo wa Kieletroniki wa Tathmini ya Hali ya Watumishi wa Umma katika Taasisi za Umma wakati akizindua mfumo huo jijini Dodoma.






No comments:

Post a Comment