Saturday, May 21, 2022

KITUO CHA HUDUMA KWA MTEJA OFISI YA RAIS-UTUMISHI KIMEWAPUNGUZIA GHARAMA WATUMISHI NA WANANCHI KUFUATILIA MASUALA YA KIUTUMISHI - Mhe. Jenista

Na. Veronica E. Mwafisi-Dodoma

Tarehe 21 Mei, 2022

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama amesema, Kituo cha Huduma kwa Mteja (Call Centre) cha ofisi yake tangu kianze kutoa huduma, kimewapunguzia gharama watumishi wa umma na wananchi waliokuwa wakilazimika kusafiri umbali mrefu kufuatilia utekelezaji wa masuala yao ya kiutumishi yaliyowasilishwa ofisini kwake jijini Dodoma kwa ajili ya kufanyiwa kazi.

Mhe. Jenista amesema hayo jijini Dodoma, alipofanya ziara ya kikazi katika moja ya Idara yake ya Ukuzaji Maadili iliyoko Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) ili kujionea namna Kituo cha Huduma kwa Mteja kinavyofanya kazi.

Waziri Jenista amesema toka kituo hicho kianze kutoa huduma rasmi imeonekana kuwa, kina faida kubwa katika kuwapunguzia gharama watanzania wanaofualia masuala yao ya kiutumishi na wanaohitaji ufafanuzi wa masuala yao ya kiutumishi katika ofisi yake.

“Watoa huduma katika kituo chetu wamekuwa wakipokea baadhi ya hoja zinazoihusu ofisi yangu na nyingine nyingi zinahusu taasisi nyingine za Serikali hivyo, ofisi yangu imekuwa ikitoa ufafanuzi na elimu kwa watanzania ili wawasilishe hoja zao mahala sahihi,” Mhe. Jenista amefafanua.

Mhe. Jenista amesisitiza kuwa, kituo hicho kimeisaidia ofisi yake kufuatilia mwenendo mzima wa hali na ustawi wa Utumishi wa Umma nchini, ikiwa ni pamoja na kuwasaidia watumishi wa umma kuwa karibu na ofisi yake iliyopewa dhamana ya kusimamia masuala ya kiutumishi na utawala bora.

Mhe. Jenista amefafanua kuwa, kituo hicho kinatoa huduma siku za kazi kuanzia jumatatu hadi ijumaa kuanzia saa mbili na nusu hadi saa kumi jioni.

“Ukitaka kupata huduma katika kituo chetu tumia namba 0262 160 240 na kila atakayeipata namba hii ampatie na mwingine ili ofisi yangu itoe huduma, ikiwa ni sehemu ya kuuunga mkono jitihada za Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan za kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi,” Mhe. Jenista amesisitiza.

Akizungumzia maadili ya watoa huduma wa kituo hicho, Mhe. Jenista amesema watoa huduma wote wamepatiwa mafunzo ya maadili hivyo ni waadilifu na wanatoa huduma kwa kuwajali wateja.

Aidha, Mhe. Jenista amepata fursa ya kutoa huduma kwa watumishi wa umma waliopiga simu katika kituo hicho, hivyo kutatua changamoto za kiutumishi zilizokuwa zikiwakabili watumishi hao.

Kituo cha Huduma kwa Mteja (Call Centre) cha Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kiilianza kutoa huduma rasmi mwezi Juni, 2021. 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akizungumza na baadhi ya Watendaji wa ofisi yake (hawapo pichani) mara baada ya kumaliza ziara yake ya kikazi ya kutembelea Idara yake ya Ukuzaji Maadili na kukagua utendaji kazi wa Kituo cha Huduma kwa Mteja (Call Centre) kilichopo katika ofisi zake ziIlizoko UDOM Jijini Dodoma


Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Maadili, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Leila Mavika akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Idara yake kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama wakati wa ziara ya kikazi ya Mhe. Jenista katika Idara hiyo iliyolenga kukagua utendaji kazi wa Kituo cha Huduma kwa Mteja (Call Centre).


Mkurugenzi wa Idara ya Ukuzaji Maadili, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bi. Leila Mavika akimuonyesha Kanuni za Maadili ya Utendaji katika Utumishi wa Umma Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama wakati wa ziara ya kikazi ya Mhe. Jenista ya kukagua utendaji kazi wa Idara hiyo.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akimhudumia mtumishi aliyepiga simu kwenye Kituo cha Huduma kwa Mteja (Call Centre) alipowatembelea watoa huduma wa kituo hicho kwa lengo la kujionea utendaji kazi wao. Wengine ni baadhi ya watendaji wa Ofisi yake alioambatana nao.



Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akifurahia jambo na Watendaji wa ofisi yake mara baada ya kumhudumia Mtumishi aliyepiga simu katika Kituo cha Huduma kwa Mteja (Call Centre) cha ofisi yake, alipokitembelea kituo hicho ili kujionea utendaji kazi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akifuatilia namna ambavyo mtoa huduma wa kituo cha huduma kwa mteja (Call Centre) wa Ofisi yake anavyotoa huduma kwa mteja aliyepiga simu kwa ajili ya kupata huduma kwenye kituo hicho.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akiwasili katika Ofisi yake iliyopo UDOM kwa lengo la kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi wa Idara ya Ukuzaji Maadili wa ofisi yake.




No comments:

Post a Comment