Wednesday, May 11, 2022

VIJANA 350 WANAOTARAJIWA KUAJIRIWA NA TAKUKURU WAASWA KUZINGATIA MAFUNZO YA UCHUNGUZI ILI KUOKOA FEDHA ZA UMMA ZINAZOPOTEA KUTOKANA NA UBADHIRIFU

Na. James K. Mwanamyoto-Moshi

Tarehe 11 Mei, 2022

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama amewaasa vijana 350 wanaotarajiwa kuajiriwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kuzingatia mafunzo ya awali ya uchunguzi yanayotolewa kwa vijana hao katika Shule ya Polisi Moshi ili kuokoa fedha za umma zinazopotea kutokana ubadhirifu.

Waziri Jenista ametoa nasaha hizo leo mjini Moshi wakati akifungua mafunzo ya awali ya uchunguzi kwa vijana 350 wanaotarajiwa kuajiriwa na TAKUKURU mara baada ya kufuzu mafunzo hayo.

Mhe. Jenista amesema, kama vijana hao watazingatia mafunzo na kuajiriwa, wataisaidia Serikali kuokoa fedha nyingi zinazopotea kwenye mikono ya watu ambao hawana uzalendo na uchungu wa maendeleo ya watu, vitu na nchi.

“Mtakapofuzu mafunzo haya na kupata ajira ya kudumu, tunataka mtoe mchango katika kudhibiti upotevu wa fedha za umma ili maendeleo ya vitu yaakisi maendeleo ya watu na maendeleo yote hayo yaakisi maendeleo ya taifa kwa ujumla.” Mhe. Jenista amesisitiza.

Mhe. Jenista ameongeza kuwa, vijana hao wakipata mafunzo hayo, yatasaidia pia usimamizi wa miradi mbalimbali ya serikali na kukamilika kwake kwa wakati, hivyo kuleta manufaa makubwa katika kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Aidha, Mhe. Jenista ameeleza kuwa dhamira ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan, TAKUKURU na Viongozi wengine ni kuongeza nguvu kwenye kuzuia rushwa isitokee kwani gharama ya kuziuia rushwa ni ndogo kuliko gharama ya kupambana na rushwa, kwa mantiki hiyo, amewataka vijana hao wanaotarajiwa kuajiriwa na TAKUKURU kuhakikisha wanaunga mkono kwa vitendo dhamira hiyo ya Mhe. Rais na wasaidizi wake.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa TAKUKURU, CP Salum Hamduni amesema, dhamira ya TAKUKURU ni kuona kila mshiriki anatambua kuwa ajira yake ndani ya TAKUKURU pamoja na mambo mengine inategemea sana uadilifu na nidhamu yake wakati wote wa mafunzo na baada ya kuajiriwa.

CP Hamduni amewasihi vijana hao kuzingatia Sheria, Kanuni na Miongozo ambayo wanapatiwa na maelekezo mengine yatakayokuwa yanatolewa na menejimenti ya TAKUKURU pamoja na uongozi wa Shule ya Polisi-Moshi, na kuongeza kuwa hawatamvumilia yeyote atakayekwenda kinyume na maadili ya kiutendaji.

Vijana hao 350 wanaopata mafunzo kwa ajili ya kuajiriwa na TAKUKURU ni matokeo ya kibali cha ajira kilichotolewa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan kupitia Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ili kuiwezesha TAKUKURU kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akifungua mafunzo ya awali ya uchunguzi kwa vijana 350 wanaotarajiwa kuajiriwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) yanayofanyika katika Shule ya Polisi Moshi. 


Vijana wanaotarajiwa kuajiriwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama (hayupo pichani) wakati akifungua mafunzo ya awali ya uchunguzi kwa vijana hao yanayofanyika katika Shule ya Polisi Moshi. 


Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mhe. Steven Kagaigai akitoa salamu za mkoa wake kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama (hayupo pichani) kabla ya Waziri Jenista kufungua mafunzo ya awali ya uchunguzi kwa vijana wanaotarajiwa kuajiriwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) katika Shule ya Polisi Moshi. 


Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) CP Salum Hamduni akielezea umuhimu wa mafunzo ya awali ya uchunguzi kwa vijana wanaotarajiwa kuajiriwa na TAKUKURU kabla ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kufungua mafunzo hayo katika Shule ya Polisi Moshi. 


Mkuu wa Shule ya Polisi Moshi, SACP Ramadhani Mungi akielezea maendeleo ya mafunzo ya awali ya uchunguzi kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kabla ya Mhe. Jenista kufungua mafunzo hayo kwa vijana 350 wanaotarajiwa kuajiriwa na TAKUKURU.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akisalimiana na Maafisa wa Jeshi la Polisi katika Shule ya Polisi Moshi alipoenda kufungua mafunzo ya awali ya uchunguzi kwa vijana wanaotarajia kuajiriwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU). Alioambatana nao ni Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mhe. Steven Kagaigai, Mkurugenzi Mkuu TAKUKURU CP Salum Hamduni na Katibu Tawala wa Mkoa wa Kilimanjaro, Bw. Willy Machumu.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akiwa katika picha ya pamoja na Maafisa wa Jeshi la Polisi na Wakufunzi wa mafunzo ya awali ya uchunguzi kwa vijana wanaotarajiwa kuajiriwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) baada ya kufungua mafunzo hayo yanayofanyika katika Shule ya Polisi Moshi. Anayefuatia kushoto kwake ni Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mhe. Steven Kagaigai na anayefuatia kulia kwake ni Mkurugenzi Mkuu TAKUKURU CP Salum Hamduni.


 

No comments:

Post a Comment