Sunday, September 18, 2022

KAMATI YA USEMI YAELEKEZA UMILIKI WA HATI MILIKI ZA ARDHI ZA FAMILIA UWE WA AKINA MAMA NA BABA

 Na. James K. Mwanamyoto-Chamwino

Tarehe 18 Septemba, 2022

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Abdallah Chaurembo ameipongeza MKURABITA kwa kuwapatia Hati Miliki za Ardhi za Kimila wananchi wa Kijiji cha Manyemba wilayani Chamwino, na kuelekeza hati zote zinazohusisha familia pindi zinapoandaliwa umiliki wake uwe na majina ya akina mama pia badala ya majina ya akina baba pekee.

Mhe. Chaurembo ametoa maelekezo hayo akiwa katika Kijiji cha Manyemba wakati wa ziara ya kikazi ya kamati yake wilayani Chamwino, iliyolenga kukagua utekelezaji wa shughuli za Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge (MKURABITA) wilayani humo.

Mhe. Chaurembo amesema, MKURABITA licha ya kutekeleza vizuri wajibu  wa kujenga masijala na kuwapatia wananchi wa kijiji hicho hati miliki za ardhi, lakini wanapaswa kuzingatia kuwa hati zote za kifamilia umiliki wake uwe na majina ya akina mama na akina baba kwani wote wana haki sawa katika umiliki wa ardhi.

“Kama eneo ni la familia, baba na mama wanamiliki hakikisheni majina ya wote wawili yameandikwa kwenye hati, jina la mama liwepo na la baba liwepo kwani si dhambi kwa hati moja kuwa na jina zaidi ya moja, hivyo tunapaswa kujenga utamaduni wa akina mama nao wawe sehemu ya kumiliki ardhi,” Mhe. Chaurembo amesisitiza.

Naye, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi amesema kuwa, MKURABITA katika Kijiji cha Manyemba imefanya kazi kubwa sana ya kutoa hati zilizosaidia kutatua migogoro mingi ya umiliki wa ardhi.

Mhe. Ndejembi ameongeza kuwa, mara baada ya MKURABITA kuwezesha upimaji wa ardhi kwenye kijiji hicho, migogoro mingi na mikubwa ya ardhi imekwisha na kubaki changamoto ndogo ndogo zinazotatulika ambapo kipindi cha nyuma kulikuwa na migogoro mikubwa sana ya ardhi.

Mmoja wa wananchi wa Kijiji cha Manyemba aliyekabidhiwa hati ya kumiliki ardhi, Bw. Timothy Lesi ameishukuru MKURABITA kwa kuwapatia hati ambazo zitatatua migogoro ya ardhi inayotokana na wageni katika kijiji chao kuvamia ardhi za wenyeji jambo ambalo linahatarisha amani iliyopo.

Kwa upande wake, Mratibu wa MKURABITA, Dkt. Seraphia Mgembe amesema uzinduzi wa jengo la masijala ni kiashiria cha wananchi wa Kijiji cha Manyemba kuwa karibu na maendeleo na kuongeza kuwa, mara baada ya MKURABITA kuwapimia mashamba wananchi wa kijiji hicho tayari wameshawapatia mafunzo kwa kushirikiana na benki ya NMB na CRDB ya namna gani wanaweza kutumia hati kupata mikopo.

Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge (MKURABITA) umeendelea kuwa ni sehemu ya utatuzi wa migogoro mingi ya ardhi nchini hususani katika maeneo ya vijijini.

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Abdallah Chaurembo (Mb) akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Manyemba wilayani Chamwino wakati wa ziara ya kikazi ya kamati yake wilayani humo, iliyolenga kukagua utekelezaji wa shughuli za Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge (MKURABITA).


Baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Manyemba wilayani Chamwino wakimsikiliza Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Abdallah Chaurembo (hayupo pichani) wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo wilayani humo, iliyolenga kukagua utekelezaji wa shughuli za Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge (MKURABITA).


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Manyemba wilayani Chamwino, wakati wa ziara ya kikazi ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, iliyolenga kukagua utekelezaji wa shughuli za Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge (MKURABITA) wilayani humo.


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Abdallah Chaurembo (Mb) akimkabidhi hati mmoja wa wananchi wa Kijiji cha Manyemba wilayani Chamwino wakati wa ziara ya kikazi ya kamati yake wilayani humo, iliyolenga kukagua utekelezaji wa shughuli za Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge (MKURABITA). Anayeshuhudia ni Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb).


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Abdallah Chaurembo (Mb) akizindua jengo la masijala ya ardhi la Kijiji cha Manyemba wilayani Chamwino wakati wa ziara ya kikazi ya kamati yake wilayani humo, iliyolenga kukagua utekelezaji wa shughuli za Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge (MKURABITA). Wengine ni Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi na Mratibu wa MKURABITA, Dkt. Seraphia Mgembe.


Mkurugenzi wa Urasimishaji MKURABITA, Bi. Jane Lyimo akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya MKURABITA kwa wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo katika Kijiji cha Manyemba wilayani Chamino iliyolenga kukagua utekelezaji wa shughuli za MKURABITA.


Mratibu wa MKURABITA, Dkt. Seraphia Mgembe akieleza manufaa ya utekelezaji wa Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge (MKURABITA) katika Kijiji cha Mayemba wilayani Chamwino, mara baada ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhitimisha ziara ya kikazi wilayani Chamwino.


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Mhe. Abdallah Chaurembo akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa kamati yake pamoja na wananchi wa Kijiji cha Manyemba wilayani Chamwino waliokabidhiwa hati, mara baada ya kamati yake kuhitimisha ziara ya kikazi wilayani humo iliyolenga kukagua utekelezaji wa shughuli za MKURABITA.



No comments:

Post a Comment