Friday, December 4, 2020

SERIKALI KUTUMIA MFUMO WA KIELEKTRONIKI WA MPANGO WA RASILIMALIWATU KUBORESHA USIMAMIZI WA RASILIMALIWATU

 Na. James K. Mwanamyoto

Tarehe 04 Disemba,2020

Serikali imeandaa Mfumo Mahsusi wa Kielektroniki wa Mpango wa Rasilimaliwatu katika Utumishi wa Umma (e-HRP) utakaowezesha Taasisi za Umma nchini kusimamia Rasilimaliwatu vizuri na kupata takwimu sahihi za mahitaji ya watumishi wake.

Hayo yamesemwa leo na Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Francis Michael wakati akifungua kikao kazi cha wadau kujadili mahitaji ya Mfumo wa Kielektroniki wa Mpango wa Rasilimaliwatu kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Rais Utumishi -  Mtumba jijini Dodoma.

Dkt. Michael amefafanua kuwa, mfumo huo utawezesha kubaini mahitaji sahihi ya Rasilimaliwatu kwa wakati wa sasa na baadae ili kuwa na mipango mahususi ya kiutumishi pamoja na matumizi mazuri ya Rasilimaliwatu.

Ameongeza kuwa, matumizi ya mfumo huo utaziwezesha Taasisi za Umma kuwa na watumishi wa kutosha, wenye sifa na uwezo unaotakiwa mahali pa kazi katika utekelezaji wa majukumu ya taasisi zao.

Dkt. Michael amesisitiza kuwa, Sera ya Menejimenti na Ajira katika Utumishi wa Umma ya Mwaka 2008 imeelekeza kila Taasisi ya Umma kuwa na mpango wa kati na mpango wa kila mwaka wa Rasilimaliwatu kulingana na malengo yake kwani  Mpango wa Rasilimaliwatu ni moja ya nyenzo muhimu katika Usimamizi na Menejimenti ya Watumishi.

Kikao kazi hicho cha siku moja kimewajumuisha Wasimamizi wa Rasilimaliwatu kutoka katika Wizara, Idara Zinazojitegemea, Wakala za Serikali, Mashirika ya Umma, Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa, kitaiwezesha Serikali kupata  maoni ambayo yataboresha Mfumo huo wa Kielektroniki wa Mpango wa Rasilimaliwatu katika Utumishi wa Umma

Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Dkt. Francis Michael akifungua kikao kazi cha wadau kujadili mahitaji ya Mfumo wa Kielektroniki wa Mpango wa Rasilimaliwatu kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Rais Utumishi -  Mtumba jijini Dodoma.

Wasimamizi wa Rasilimaliwatu kutoka katika Wizara, Idara Zinazojitegemea, Wakala za Serikali, Mashirika ya Umma, Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa, wakifuatilia mada kuhusu Mpango wa Rasilimaliwatu iliyowasiliswa na Mkurugenzi Msaidizi Idara wa Mipango ya Rasilimaliwatu Dkt. Edith Rwiza ili kutoa fursa kwa wadau hao kutoa maoni ya kuboreresha Mfumo wa Kielektroniki wa Mpango wa Rasilimaliwatu katika Utumishi wa Umma

 


Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Dkt. Francis Michael  akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa kikao kazi cha kujadili mahitaji ya Mfumo wa Kielektroniki wa Mpango wa Rasilimaliwatu kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Rais Utumishi -  Mtumba jijini Dodoma.

 

 

No comments:

Post a Comment