Friday, December 18, 2020

MILIONI 569 ZA TASAF KUWANUFAISHA WANANCHI WILAYANI CHATO KWA KUJENGA KITUO CHA AFYA

 

Na. James K. Mwanamyoto – Chato

Tarehe 19 Disemba, 2020

Wananchi wa Kijiji cha Nyabilezi na maeneo ya jirani Wilayani Chato watanufaika na huduma za afya zitakazotolewa katika Kituo cha afya cha Nyabilezi baada Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kuchangia kiasi cha shilingi milioni 569 kwa lengo la kuboresha huduma za afya kwa wananchi wa eneo hilo.

Mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa kituo hicho cha afya, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Kapt. (Mst) Mhe. George Mkuchika amesema kiasi hicho cha fedha kilichotolewa na TASAF kitakuwa na mchango mkubwa katika kuboresha huduma za afya.

Kutokana na umuhimu wa kituo hicho, Mhe. Mkuchika amewahimiza Viongozi Wilayani Chato kukamilisha ujenzi wa kituo hicho cha afya ifikapo tarehe 30 Machi, 2021 kama ilivyopangwa ili wananchi wapate huduma ya afya inayostahili.

Aidha, Mhe. Mkuchika amewapongeza wananchi wa kijiji cha Nyabilezi kwa kutoa mchango wa fedha na kushiriki katika shughuli mbalimbali za ujenzi wa kituo hicho cha afya kwa kuchota maji, kusomba mchanga, kokoto na mawe.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Chato, ambaye pia ni Waziri wa Nishati, Mhe. Medard Kalemani ameishukuru Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kupitia TASAF kwa kutoa fedha za ujenzi wa kituo hicho cha afya ambacho kikikamilika kitakuwa na mchango mkubwa katika utoaji wa huduma za afya katika Kijiji cha Nyabilezi na maeneo jirani.

Pamoja na pongezi hizo, Mhe. Kalemani amemuomba Mhe, Mkuchika kupitia TASAF kujenga kituo kingine cha afya katika Kijiji cha Makurugusi ili kupunguza msongamano wa wananchi watakaofuata huduma za afya katika Kituo cha Nyabilezi.

Awali, Kituo cha Afya cha Nyabilezi kata ya Bukome kilikuwa ni Zahanati, hivyo kutokana na umuhimu wa huduma za afya katika kata hiyo, TASAF imetoa kiasi cha fedha cha shilingi milioni 569 ili kukidhi uhitaji wa huduma za afya.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Kapt. (Mst) Mhe. George Mkuchika akizungumza na Wananchi wa Kijiji cha Nyabilezi na maeneo ya jirani Wilayani Chato watakaonufaika na huduma za afya zitakazotolewa katika Kituo cha afya cha Nyabilezi mara baada ya kukagua ujenzi wa kituo hicho. Kushoto kwake ni Mbunge wa Jimbo la Chato, ambaye pia ni Waziri wa Nishati, Mhe. Medard Kalemani na kulia kwake ni Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhandisi Mhe. Robert Gabriel Luhumbi.



Baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Nyabilezi na maeneo ya jirani Wilayani Chato wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Kapt. (Mst) Mhe. George Mkuchika (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza nao mara baada ya kukagua ujenzi wa kituo cha afya cha Nyabilezi Wilayani Chato. 


Mganga Mkuu wa Wilaya ya Chato, Dkt. Benedicto Ngaiza akisoma taarifa ya ujenzi wa Kituo cha afya cha Nyabilezi kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Kapt. (Mst) Mhe. George Mkuchika alipotembelea kituo hicho ili kukagua maendeleo ya ujenzi.


Kaimu Mtendaji Mkuu wa TASAF, Bw. Paul Kijazi akielezea mchango wa TASAF katika ujenzi unaoendelea katika kituo cha Nyabilezi Wilayani Chato. Kushoto kwake ni Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhandisi Mhe. Robert Gabriel Luhumbi.


Mbunge wa Jimbo la Chato, ambaye pia ni Waziri wa Nishati, Mhe. Medard Kalemani akimshukuru Mhe. Mkuchika kwa taasisi yake ya TASAF kutoa mchango katika ujenzi wa kituo cha afya cha Nyabilezi Wilayani Chato. Kulia kwake ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Kapt. (Mst) Mhe. George Mkuchika na Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhandisi Mhe. Robert Gabriel Luhumbi.


Mkuu wa Mkoa wa Geita, Mhandisi Mhe. Robert Gabriel Luhumbi, akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Kapt. (Mst) Mhe. George Mkuchika kuzungumza na wananchi wa Kijiji cha Nyabilezi na maeneo ya jirani mara baada ya Waziri huyo kukagua maendeleo ya ujenzi wa Kituo cha afya cha Nyabilezi Wilayani Chato.

 


No comments:

Post a Comment