Tuesday, December 22, 2020

WATUMISHI SEKRETARIETI YA AJIRA WATAKIWA KUFANYA KAZI KWA UADILIFU ILI KUTENDA HAKI KWA WAOMBAJI WA AJIRA


Na. James K. Mwanamyoto – Morogoro

Tarehe 22 Disemba, 2020


Watumishi wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma wametakiwa kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia maadili na uwajibikaji ili kutenda haki kwa kila mwombaji wa ajira Serikalini ambaye ana sifa za kupata kazi kwa mujibu wa nafasi husika zinazotangazwa na Taasisi mbalimbali za umma.

Wito huo umetolewa jana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Kapt. (Mst) George H. Mkuchika (Mb) wakati akifungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma kilichofanyika mjini Morogoro.

Mhe. Mkuchika amewasisitiza watumishi hao kuendelea kuzingatia Uadilifu, Sheria, Kanuni na Taratibu zinazosimamia Utumishi wa Umma nchini kwani kazi wanayoifanya ni nyeti na inagusa maisha ya watu, hivyo inahitaji watu waadilifu, wapenda haki na ambao ni mfano wa kuigwa na jamii kwa uadilifu.

Akizungumzia utoaji wa huduma kwa wateja, Mhe. Mkuchika amesema, ni muhimu watumishi wa Sekretarieti ya Ajira kuwahudumia wateja wao kwa lugha nzuri kwani ndio nyenzo muhimu katika utoaji wa ajira.

“Tumieni lugha nzuri na zenye staha kwa kuwasikiliza na kuwahudumia vizuri wateja wenu kwani nyie ndio lango kuu la kuingiza watu katika Utumishi wa Umma, hivyo mienendo yenu ndio picha ya aina ya watumishi watakaopatikana kwa ajili ya kuja kusimamia utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo inayofanywa na Serikali”, Mhe. Mkuchika amefafanua.

Mhe. Mkuchika amewahimiza watumishi hao, kufanya kazi kwa kushirikiana na waajiri kwani jukumu walilopewa la kuendesha mchakato wa ajira ni kwa niaba ya waajiri hivyo ni muhimu wakashirikiana kuhakikisha mchakato wa ajira unakwenda vizuri na kwa wakati na hatimaye kupata watumishi wenye sifa stahiki ambao watalisukuma gurudumu la maendeleo ya Taifa kwa kasi zaidi.

Aidha, Mhe. Mkuchika amewataka watumishi wa Sekretarieti ya Ajira kurahisisha mchakato wa ajira kwa kuongeza matumizi ya TEHAMA katika kuchuja waombaji wa kazi, hatua hiyo ni kuunga mkono jitihada za Mhe. Rais kuhimiza matumizi ya TEHAMA ikizingatiwa kuwa, suala hili amelipa uzito mkubwa mpaka kuliundia Wizara.

Akizungumzia kuhusu matumizi ya TEHAMA, Katibu wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma Bw. Xavier Daudi amesema, Mifumo ya TEHAMA imeiwezesha ofisi yake kuthibiti matumizi ya vyeti vya kughushi katika uendeshaji wa mchakato wa ajira Serikalini kwa kushirikiana na Mamlaka nyingine zenye dhamana katika sekta za elimu na mafunzo katika zoezi la uhakiki.

Bw. Daudi ameongeza kuwa, kupitia mifumo ya kiutendaji ya TEHAMA wamewawezesha waombaji kazi kupata na kufuatilia taarifa za matangazo ya kazi kupitia teknolojia rahisi ya simu za kiganjani popote alipo mteja ikiwemo mitandao ya kijamii ambayo imewapunguzia adha wafuatiliaji wa fursa za ajira kwani taarifa zinawafakia popote walipo.

Kuhusiana na suala la uadilifu, Bw. Daudi amesema Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma imejiwekea malengo kuhakikisha wanaoajiriwa  katika Taasisi za Umma wanakuwa na sifa ya uadilifu na uwajibikaji.

 


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Kapt. (Mst) George H. Mkuchika (Mb) akizungumza na watumishi wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma wakati akifungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi la ofisi hiyo kilichofanyika jana mjini Morogoro.




Baadhi ya wajumbe wa Baraza la Wafanyakazi la Sekretarieti ya Maadili katika Utumishi wa Umma wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Kapt. (Mst) George H. Mkuchika (Hayupo pichani) wakati akifungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi la ofisi hiyo kilichofanyika jana mjini Morogoro.



Katibu wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma, Bw. Xavier Daudi akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya ofisi yake kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Kapt. (Mst) George H. Mkuchika (Hayupo pichani) kabla ya Waziri huyo kufungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi la ofisi hiyo kilichofanyika jana mjini Morogoro.


Katibu Tawala Mkoa wa Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Emmanuel Kalobelo akitoa neno la shukrani kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Kapt. (Mst) George H. Mkuchika mara baada ya Waziri huyo kufungua kikao cha Baraza la Wafanyakazi la Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma kilichofanyika jana mjini Morogoro.


 

No comments:

Post a Comment