Monday, August 18, 2025

KATIBU MKUU MKOMI ASISITIZA DHANA YA URITHISHANAJI MADARAKA KWA WATUMISHI WA UMMA NCHINI

 Na. Mwandishi Wetu- Dodoma

 Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, UTUMISHI, Bw. Juma Mkomi ameitaka Idara ya Uendelezaji Rasilimaliwatu katika Ofisi hiyo kuongeza nguvu katika eneo la mafunzo ya umuhimu wa  Urithishanaji wa madaraka kwa Watumishi wa Umma huku akiwataka Wakurugenzi na Wakuu wa Taasisi nchini kuwaandaa watumishi wao ili waweze kuwa viongozi wazuri hapo baadaye

 Amesema Kiongozi mzuri ni yule anayewaandaa watumishi walio chini yake kuwa viongozi wazuri katika siku za usoni huku akionya dhana potofu iliyojengeka kuwa ukiwaandaa watumishi walio chini yako wataichukua nafasi uliyonayo

 Amesema Serikali ina Taasisi nyingi ambazo zinahitaji watumishi hao walioandaliwa vizuri na kwa muda mrefu

 Bw. Mkomi ametoa kauli hiyo leo Jumatatu Agosti 18, 2025 katika ofisi hiyo iliyopo Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma wakati akizungumza na watumishi wa Ofisi hiyo  mara baada ya kutolewa kwa mafunzo ya Uongozi,  ikiwa ni muendelezo wa mafunzo hayo ambayo hutolewa  kila wiki kwa Watumishi   kwa  lengo la  kuboresha utendaji kazi wao

 Amesema endapo kutakuwa na utamaduni huo wa kurithishana madaraka, watumishi watakaoandaliwa wataenda kuwa viongozi mahali pengine na sio lazima wabaki hapo hapo.  

 Awali Mwezeshaji wa Mafunzo hayo ya Uongozi, Dkt. Ntangeki Nshala amesema Uongozi sio lazima uwe unawaongoza watu bali ni kuonesha uwezo ulionao katika eneo ulilopo

 Amesema  uongozi ni suala binafsi na msukumo uliopo ndani ya mtu ndio maana uongozi unatofautiana katika ya mtu na mtu

 Amesema uongozi ni kuonesha njia,kujaribu  na kujiamini katika kufanya maamuzi popote ulipo na sio lazima uwe na cheo fulani

 Aidha Dkt. Nshala amesema Watumishi wanahitaji kuwa na ujasiri  na ndoto kubwa ya kufanya  chochote wanachohitaji   huku akionya tabia ya watu wengi ya kushindwa kuonesha uwezo wao kwa kisingizio cha uroho wa madaraka 

 Amesema Watumishi waliowengi mara baada ya kuajiriwa husahau kusudi la ndoto zao na hivyo hujikuta wakiishi ili mradi kwa sababu hali zao za kiuchumi huwa zimeimarika kidogo 

 " Ukiwa huna ujasiri huwezi kufanya mambo makubwa na hivyo  wengi hujikuta  wakijidumaza" amesisitiza Dkt. Nshala 

 Kufuatia hatua hiyo, Dkt. Nshala amesisitiza watumishi kujitambua na kuwa na dira na maono  ya kutaka kuwa nani katika kazi na kwenye jamii kwa ujumla 

 

Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais,  UTUMISHI Bw.Juma Mkomi akizungumza na Watumishi wa Ofisi anayoingoza mara baada ya Mwezeshaji wa mafunzo ya Uongozi, Dkt.Ntangeki kuhitimisha  kutoa mafunzo hayo
Mwezeshaji wa mafunzo ya Uongozi, Dkt. Ntangeki Nshala akitoa mafunzo hayo  kwa Watumishi wa Ofisi ya Rais, UTUMISHI na Utawala Bora katika ofisi hiyo iliyopo Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma

Baadhi ya Wakurugenzi wa Idara mbalimbali  pamoja na Watumishi wa Ofisi ya Rais,UTUMISHI na Utawala Bora wakifuatilia mafunzo yaliyokuwa yanaendelea kutolewa  katika Ofisi hiyo


Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais,  UTUMISHI Bw. Juma Mkomi  akikabidhiwa  moja ya kitabu cha masuala ya Uongozi kutoka kwa Mwezeshaji wa mafunzo Dkt. Nshala mara baada ya kutoa mafunzo ya Uongozi kwa watumishi wa Ofisi anayoiongoza

Baadhi ya Wakurugenzi kutoka Ofisi ya Rais, UTUMISHI na Utawala Bora  wakiwa na Mwezeshaji wa mafunzo Dkt.Ntangeki Nshala wakipata maelezo ya  vitabu mbalimbali alivyowahi kuandika .

Wakurugenzi wa Idara na Vitengo katika Ofisi ya Rais, UTUMISHI na Utawala Bora wakionesha muitikio wao juu ya mafunzo yaliyotolewa Ofisini hapo kwa kununua vitabu vinavyoelezea masuala ya Uongozi vilivyoandikwa na Dkt. Nshala.


 

 

  

No comments:

Post a Comment