Wednesday, November 16, 2022

MILIONI 264.3 ZA TASAF ZATUMIKA KUSOGEZA HUDUMA ZA AFYA KWA WANANCHI WA KIJIJI CHA IKELU KAMA ALIVYOELEKEZA MHE. RAIS

 

Na. James K. Mwanamyoto-Makambako

Tarehe 16 Novemba, 2022

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama amesema, milioni 264.3 zilizotolewa na Serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) zimetumika kujenga zahanati ya Kijiji cha Ikelu iliyopo katika Halmashauri ya Mji Makambako na nyumba ya watumishi wa zahanati hiyo ili kutekeleza maelekezo ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ya kusogeza huduma za afya karibu na wananchi.

Mhe. Jenisa amesema hayo, mara baada ya kukagua ujenzi wa zahanati ya Kijiji cha Ikelu na nyumba ya watumishi wa zahanati hiyo, akiwa kwenye ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini unaoratibiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) katika Halmashauri ya Mji Makambako.

Mhe. Jenista amesema kuwa, kutokana na maombi ya wananchi wa Kijiji cha Ikelu, Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa mapenzi yake aliridhia milioni 264.3 zitumike kutatua changamoto ya kukosekana kwa huduma za afya kwa wananchi wa kijiji hicho.

“Mhe. Rais kupitia fedha za TASAF alielekeza ijengwe zahanati na nyumba ya watumishi wa zahanati hiyo ili kuondoa tatizo la ukosefu wa zahanati na nyumba ya watumishi wa afya ambao wana jukumu la kuhakikisha wananchi wanakuwa na afya bora itakayowawezesha kushiriki shughuli mbalimbali za maendeleo,” Mhe. Jenista amefafanua.

Akizungumzia ubora wa zahanati na nyumba ya watumishi iliyojengwa, Mhe. Jenista amesema kuwa amekagua maendeleo ya ujenzi wa mradi huo wa zahanati na nyumba hiyo ya watumishi, na kubaini kuwa miradi yote miwili imejengwa kwa ubora na viwango vinavyotakiwa kwa kuzingatia thamani ya fedha iliyotumika.

Sanjari na hilo, Mhe. Jenista amesema, Serikali haitoishia katika ujenzi wa zahanati na nyumba ya watumishi pekee kwani Mhe. Rais ameiagiza TASAF kuleta vifaa tiba ili kuhakikisha huduma ya afya ya mama na mtoto pamoja na wananchi kwa ujumla zinapewa kipaumbe kama ambavyo Serikali ya Awamu ya Sita imekusudia.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Mhe. Kissa Kasongwa amesema wananchi wa Kijiji cha Ikelu wanamshukuru sana Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwajengea zahanati na nyumba ya watumishi, kwani awali kijiji hicho hakikuwa na zahanati wala kituo cha afya kilicho karibu, hivyo zahanati iliyojengwa itakuwa ni msaada kwa akina mama waliokuwa wakisafiri umbali mrefu kufuata huduma za afya ya uzazi.

Naye, Bi. Flora Wimile kwa niaba ya Afisa Mtendaji, akiwasilisha taarifa ya Utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini  katika Kijiji cha Ikelu, amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia TASAF kutumia  shilingi milioni 264.3 ili kutatua changamoto ya upatikanaji wa huduma ya afya ambayo imekuwa ikiwakabili wananchi wa Kijiji cha Ikelu kwa muda mrefu.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akizungumza na walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini na wananchi wa Kijiji cha Ikelu, Halmashauri ya Mji Makambako mkoani Njombe wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF Makambako.

 

Sehemu ya Walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini na Wananchi wa Kijiji cha Ikelu, Halmashauri ya Mji Makambako mkoani Njombe wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama alipokuwa akizungumza nao wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF Makambako.


        

 

Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Mhe. Kissa Kasongwa akizungumzia utekelezaji wa miradi ya TASAF katika wilaya yake kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kuzungumza na walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini na wananchi wa Kijiji cha Ikelu, Halmashauri ya Mji Makambako wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri Jenista ya kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF Makambako.


 

Mwakilishi wa Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Ikelu, Halmashauri ya Mji Makambako, Bi. Flora Wimile akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini katika Kijiji cha Ikelu, Halmashauri ya Mji Makambako wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama ya kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF Makambako.


 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akielekea kukagua zahanati ya Kijiji cha Ikelu, Halmashauri ya Mji Makambako mkoani Njombe mara baada ya kukagua nyumba ya watumishi wa zahanati hiyo wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF Makambako.

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akipitishwa kwenye mchoro wa  zahanati ya Kijiji cha Ikelu, Halmashauri ya Mji Makambako mkoani Njombe wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF Makambako.


 

Mwonekano wa nyumba ya watumishi wa afya wa zahanati ya Kijiji cha Ikelu, Halmashauri ya Mji Makambako iliyojengwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).


 

Mwonekano wa zahanati ya Kijiji cha Ikelu, Halmashauri ya Mji Makambako iliyojengwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).


 


No comments:

Post a Comment