Wednesday, November 2, 2022

UANZISHWAJI WA MFUKO WA UWEKEZAJI WA PAMOJA WA ‘FAIDA FUND’ NI MATOKEO YA UTAWALA BORA WA RAIS SAMIA SULUHU HASSAN

Na. James K. Mwanamyoto-Dar es Salaam

Tarehe 02 Novemba, 2022

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi amesema, mfuko wa uwekezaji wa pamoja wa FAIDA FUND ulioanzishwa na Serikali kupitia Watumishi Housing Investments (WHI), ni matokeo ya utawala bora wa Rais wa Awamu ya Sita Mhe. Samia Suluhu Hassan uliolenga kuwawezesha Watanzania wenye kipato cha chini kuwekeza ili kupata mitaji itakayoboresha maisha yao.

Mhe. Ndejembi amesema hayo jijini Dar es Salaam, wakati akizindua mauzo ya vipande vya mfuko wa uwekezaji wa pamoja wa FAIDA FUND ulioanzishwa na Watumishi Housing Investments (WHI) iliyo chini ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Mhe. Ndejembi amesema, Serikali ya Awamu ya Sita inaongoza kwa kusimamia misingi ya utawala bora na ndio maana kupitia Watumishi Housing Investments (WHI) imekuja na mfuko huu wa FAIDA FUND ambao ni wa uhakika zaidi kwa wananchi kuwekeza kwani fedha yao inakuwa kwenye mikono salama.

“Tumeoneshwa mfumo hapa ambao umetengenezwa na Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) ambao unamuwezesha mwananchi kufuatialia fedha yake na kuona faida atakayoipata, hivyo unamhakikishia mwananchi usalama wa vipande alivyonunua ili kuwekeza,” Mhe. Ndejembi amesisitiza.

Mhe. Ndejembi ameongeza kuwa, uwepo wa Benki ya CRDB kama msimamizi wa masuala yote ya uwekezaji wa fedha kwenye mfuko huo wa FAIDA FUND unaondoa mashaka na hofu ya wananchi wenye kipato cha chini wenye nia ya kuwekeza kwenye mfuko huo.

Aidha, Mhe. Ndejembi amesema kuwa FAIDA FUND ni fursa kubwa sana kwa watumishi wa umma wanaotamani kuingia katika uwekezaji kwani siku za nyuma uwekezaji ulikuwa ukitafsiriwa ni kwa watu wenye kipato kikubwa, lakini kupitia kiwango rafiki cha uwekezaji kilichowekwa na FAIDA FUND kinafungua milango ya watumishi wa umma kuwekeza.

“Kiwango cha awali cha uwekezaji kuanzia shilingi 10,000/= ambacho FAIDA FUND imekuja nacho kinamuwezesha mtumishi wa umma kufungua akaunti na kuendelea kuwekeza kwa shilingi 5,000/=, pia kinayawezesha kuwekeza makundi mengine yanayofanya kazi katika sekta isiyo rasmi yakiwemo ya bodaboda, mama lishe na mengineyo,” Mhe. Ndejembi amefafanua.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko, Mitaji na Dhamana (CMSA), Bw. Charles Shirima amesema mfuko wa FAIDA FUND umepata idhini ya mamlaka hiyo kuendeshwa na kuongeza kuwa, ni mmoja wa mfuko wa uwekezaji wa pamoja unaowezesha wawekezaji wa aina zote wakiwemo wadogo, wa kati na wakubwa kuwekeza kwa lengo la kupata faida na kuchangia katika uchumi wa nchi.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa Watumishi Housing Investments (WHI), Dkt. Fred Msemwa ambaye taasisi yake imeanzisha mfuko huo wa FAIDA FUND amesema kuwa, FAIDA FUND itawawezesha watu wenye kipato kidogo kuweka akiba itakayozaa na baadae kuuza vipande vyake na kununua kiwanja au nyumba au kufanya shughuli nyingine ya kiuchumi kadiri atakavyoona yafaa.

Mfuko wa FAIDA FUND ni mpango ulio wazi ambao unatoa fursa ya uwekezaji kwa Watanzania hasa wa kipato cha chini kupitia uwekezaji katika vipande ili kupata mapato shindani kupitia ukuaji wa mitaji na kutengeneza utamaduni wa kuwekeza katika Masoko ya Mitaji na Fedha. 



Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akizungumza na wadau jijini Dar es salaam wakati akizindua mauzo ya vipande vya mfuko wa uwekezaji wa pamoja wa FAIDA FUND ulioanzishwa na Watumishi Housing Investments (WHI) ili kuwawezesha Watanzania wenye kipato cha chini kupata mitaji itakayoboresha maisha yao.

Baadhi ya wadau wa Watumishi Housing Investments (WHI) wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (hayupo pichani) wakati akizindua mauzo ya vipande vya mfuko wa uwekezaji wa pamoja wa FAIDA FUND jijini Dar es Salaam, ulioanzishwa na WHI ili kuwawezesha Watanzania wenye kipato cha chini kupata mitaji itakayoboresha maisha yao.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akizindua mauzo ya vipande vya mfuko wa uwekezaji wa pamoja wa FAIDA FUND jijini Dar es Salaam, ulioanzishwa na Watumishi Housing Investments (WHI) ili kuwawezesha Watanzania wenye kipato cha chini kupata mitaji itakayoboresha maisha yao.


Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Watumishi Housing Investments (WHI) CPA Hosea Kashimba akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi kuzindua mauzo ya vipande vya mfuko wa uwekezaji wa pamoja wa FAIDA FUND jijini Dar es Salaam, ulioanzishwa na WHI ili kuwawezesha Watanzania wenye kipato cha chini kupata mitaji itakayoboresha maisha yao.


Mkurugenzi Mtendaji wa Watumishi Housing Investments (WHI), Dkt. Fred Msemwa akieleza manufaa ya mfuko wa uwekezaji wa pamoja wa FAIDA FUND kabla ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi kuzindua mauzo ya vipande vya mfuko huo jijini Dar es Salaam, ulioanzishwa na WHI ili kuwawezesha Watanzania wenye kipato cha chini kupata mitaji itakayoboresha maisha yao.


Mwakilishi wa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko, Mitaji na Dhamana (CMSA), Bw. Charles Shirima akiwasilisha salamu za Mtendaji Mkuu wa CMSA wakati wa  uzinduzi wa mauzo ya vipande vya mfuko wa uwekezaji wa pamoja wa FAIDA FUND jijini Dar es Salaam, ulioanzishwa na WHI ili kuwawezesha Watanzania wenye kipato cha chini kupata mitaji itakayoboresha maisha yao.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akifuatilia maelezo ya namna mfumo wa FAIDA FUND unavyofanya kazi.


 

No comments:

Post a Comment