Tuesday, November 15, 2022

MHE. NDEJEMBI AKEMEA TABIA YA WAAJIRI SERIKALINI KUFICHA BARUA ZA UHAMISHO WA WATUMISHI WA UMMA ZILIZORIDHIWA NA MAMLAKA

Na. Veronica E. Mwafisi-Kigoma

Tarehe 15 Novemba, 2022

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi amekemea tabia ya baadhi ya waajiri katika Taasisi za Umma kuficha barua za uhamisho wa watumishi wa umma ambao Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma ameridhia na kutoa kibali cha uhamisho ili wakautumikie umma katika maeneo mengine ya nchi ambayo mamlaka imeona kuna uhitaji.

Akizungumza na Watumishi wa Umma wa Halmashauri ya Manispaa Kigoma Ujiji na Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma, Mhe. Ndejembi amesema, waajiri na Maafisa Utumishi wanapaswa kutenda haki kwa watumishi wa umma ambao wanastahili kuhama baada ya kupatiwa kibali cha uhamisho na mwenye mamlaka ambaye ni Katibu Mkuu-UTUMISHI, na si kufichiwa barua zao za uhamisho kwa lengo la kukwamisha mchakato wa uhamisho.

 “Waajiri na Maafisa Utumishi tendeni haki kwa watumishi wa umma ambao wanastahili kuhama baada ya uhamisho wao kuridhiwa na mamlaka, tusifiche barua zao kwani kitendo hicho kinakwenda kinyume na mamlaka na ni kinyume cha Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo ya Utumishi wa Umma iliyopo,” Mhe. Ndejembi amesisitiza.

Mhe. Ndejembi ameongeza kuwa, wapo watumishi wa umma ambao wamefanya kazi kwa muda mrefu katika kituo kimoja cha kazi, hivyo mamlaka kupitia Ofisi ya Katibu Mkuu-UTUMISHI ikaamua kumpeleka mtumishi huyo katika eneo lingine la kazi ili abadili mazingira ya kazi ambayo yatamuongezea ufanisi kiutendaji, lakini baadhi ya waajiri hukwamisha uhamisho huo wakati mamlaka iliridhia baada ya kufanya uchambuzi yakinifu.

Aidha, Mhe. Ndejembi amewataka waajiri katika Taasisi za Umma kutopitisha barua za kuomba uhamisho za watumishi ambao ni ajira mpya, kwani ajira zao hazina muda mrefu na baadhi yao wanakuwa hawajathibitishwa kazini, hivyo kutotimiza kigezo cha kutumikia miaka mitatu tangu waajiriwe.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kigoma, Mhe. Ester Mahawe amemshukuru Mhe. Ndejembi kwa kuhimiza uwajibikaji, kutoa ufafanuzi wa masuala mbalimbali ya kiutumishi ikiwa ni pamoja na kutatua kero na changamoto mbalimbali zilizokuwa zikiwakabili watumishi walio katika wilaya yake.

Mhe. Mahawe, amewahimiza watumishi wa umma walio katika eneo lake la utawala, kufanya kazi kwa bidii na weledi kama alivyoelekeza Mhe. Ndejembi ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono kwa vitendo Kaulimbiu ya KAZI IENDELEE ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.

Naye, Mtumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma Ujiji, ambaye ni Afisa Utumishi, Bw. Stafordi Bidebuye amemshukuru Mhe. Ndejembi kwa kwa kutoa ufafanuzi wa masuala mbalimbali ya kiutumishi, ikiwa ni pamoja na kutatua kero na changamoto zilizokuwa zikiwakabili watumishi wa Halmashauri hiyo kwa muda mrefu.

Mhe. Bidebuye amesema kupitia elimu ya masuala ya kiutumishi waliyoipata kutoka kwa Mhe. Ndejembi, anaamini Mkoa wa Kigoma utafunguka katika kila sekta na kupata maendeleo chini ya uongozi makini wa Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi ameanza ziara ya kikazi mkoani Kigoma yenye lengo kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi wa umma pamoja na kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kuzinusuru Kaya Maskini nchini unaoratibiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akizungumza na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma na watumishi wa Halmashauri ya Manispaa Kigoma Ujiji (hawapo pichani), akiwa katika ziara yake ya kikazi yenye lengo kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa umma walio katika halmashauri hizo.


Watumishi wa Umma wa Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma na watumishi wa Halmashauri ya Manispaa Kigoma Ujiji wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (hayupo pichani), alipokuwa akizungumza nao wakati wa ziara yake ya kikazi iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa halmashauri hizo.


Mkuu wa Wilaya ya Kigoma, Mhe. Ester Mahawe akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi kuzungumza na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma na watumishi wa Halmashauri ya Manispaa Kigoma Ujiji (hawapo pichani), wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa umma walio katika halmashauri hizo.


Afisa Mifugo, Kilimo na Uvuvi wa Manispaa ya Kigoma Ujiji, Bw. Evans Mdee akiwasilisha hoja kwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (hayupo pichani), wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma na watumishi wa Halmashauri ya Manispaa Kigoma Ujiji.

 

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Deogratius Ndejembi (katikati) akisikiliza hoja iliyokuwa ikiwasilishwa na mtumishi wa Manispaa ya Kigoma, wakati wa ziara yake ya kikazi iliyolenga kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi wa umma wa Halmashauri hiyo. Kushoto kwake ni Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Kigoma, Bw. Ntime Mwalyambi na kulia kwake ni Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Mhe. Ester Mahawe.




 

  

No comments:

Post a Comment