Tuesday, June 7, 2022

MHE. JENISTA ALIPONGEZA SHIRIKA LA MZINGA KUFANYA TAFITI ZA MAZAO YA MSINGI KUKIDHI MAHITAJI YA SOKO LA NDANI NA NJE

 

Na. James K. Mwanamyoto-Morogoro

Tarehe 07 Juni, 2022

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama amelipongeza Shirika la Mzinga kwa kufanya tafiti za mazao ya msingi yanayozalishwa na shirika hilo kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya soko la ndani na nje ya nchi.

Mhe. Jenista ametoa pongezi hizo mjini Morogoro, wakati akizungumza na watumishi wa Shirika la Mzinga kwa lengo la kusikiliza changamoto zinazowakabili na kuhimiza uwajibikaji wa hiari kwa watumishi wa shirika hilo.

Mhe. Jenista amesema kuwa, kitendo cha shirika hilo kufanya tafiti ya mazao ya msingi yanayozalishwa ni muhimu katika kulihudumia soko la ndani na ziada yake itatumika kwenye soko la nje ili kuliingizia taifa fedha za kigeni na kuongeza pato la taifa.

“Nimeambiwa tayari mna mpango mkakati wa uzalishaji na toka mmeanza kuutekeza mmefikia asilimia 86, hivyo ninaliona shirika hili nyeti katika kukuza uchumi wa nchi pindi uzalishaji wake utafikia asilimia 100,” Mhe. Jenista amefafanua.

Mhe. Jenista ameongeza kuwa, uzalishaji ukiongezeka utawezesha upatikanaji wa huduma bora kwa wananchi kwani fedha zitakazopatikana ndio zinamuwezesha Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kuboresha miundombinu ya barabara, afya na elimu.

Kutokana na umuhimu wa kazi zinazofanywa na watumishi wa Shirika la Mzinga, Mhe. Jenista amesema ipo haja ya ofisi yake kupitia muundo wa shirika hilo, viwango cha mishahara ya watumishi na posho ya mazingira magumu ya kazi, lengo likiwa ni kuwapa motisha ili watekeleze majukumu yao kwa ari na ufanisi mkubwa.

Kwa upande wake, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe. Dkt. Stergomena Tax amewataka watumishi wa shirika hilo kuendelea kuchapa kazi kwa bidii na kuendelea kuwa na imani na Serikali ya Awamu ya Sita ambayo imejipambanua kwa vitendo katika kusimamia haki, maslahi na stahiki za watumishi wa umma nchini.

Kwa niaba ya watumishi wa Shirika la Mzinga, Meneja Mkuu wa Shirika la Mzinga Brigedia Jenerali Seif Hamisi amemshukuru Mhe. Jenista kwa kuwatembelea na kuongeza kuwa hana wasiwasi kuhusu utendaji kazi watumishi wake na iwapo watapatiwa posho waliyoiomba watakuwa na tija katika uzalishaji bidhaa muhimu zinazozalishwa na Shirika la Mzinga.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama amefanya kikao kazi na watumishi wa Shirika la Mzinga baada ya kupewa mwaliko na Mhe. Dkt. Stergomena Tax ambaye ni waziri mwenye dhamana ya ulinzi na jeshi la kujenga taifa. 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akizungumza na watumishi wa Shirika la Mzinga wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua shughuli zinazofanywa na shirika hilo mjini Morogoro.

 

Sehemu ya watumishi wa Shirika la Mzinga wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza nao wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua shughuli zinazofanywa na shirika hilo mjini Morogoro.

 

Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe. Dkt. Stergomena Tax akitoa maelezo ya awali kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kuzungumza na watumishi wa Shirika la Mzinga wakati wa ziara ya kikazi ya Mhe. Jenista Mhagama ya kukagua shughuli zinazofanywa na shirika hilo mjini Morogoro.

 

Meneja wa Shirika la Mzinga, Brigedia Jenerali Seif Hamisi, akiwasilisha taarifa ya utekelezaji kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama wakati wa ziara ya kikazi Mhe. Jenista Mhagama ya kukagua shughuli zinazofanywa na shirika hilo mjini Morogoro.

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akimsikiliza Meneja wa Shirika la Mzinga, Brigedia Jenerali Seif Hamisi, baada ya kukagua shughuli zinazofanywa na shirika hilo mjini Morogoro. Anayefuatilia maelezo hayo kwa karibu ni Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe. Dkt. Stergomena Tax.

 


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akiwa katika picha ya pamoja na Menejimenti ya Shirika la Mzinga wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua shughuli zinazofanywa na shirika hilo mjini Morogoro. Wa tatu kutoka kushoto ni Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe. Dkt. Stergomena Tax na wa tatu kutoka kulia ni Meneja wa Shirika la Mzinga, Brigedia Jenerali Seif Hamisi.

 

 

 

 

No comments:

Post a Comment