Tuesday, June 14, 2022

MHE. JENISTA AMPA SIKU MOJA MTENDAJI WA KIJIJI CHA BUKULU WILAYANI KONDOA KUHAKIKISHA MLENGWA WA TASAF ANAPATA RUZUKU

Na. James K. Mwanamyoto-Kondoa

Tarehe 14 Juni, 2022

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama (Mb) ametoa siku moja kwa Mtendaji wa Kijiji cha Bukulu katika Halmashauri ya Wilaya ya Kondoa kuhakikisha mlengwa wa TASAF kijijini humo, Bw. Laurent Chebu anapewa ruzuku yake na kumpatia taarifa ya utekelezaji wa agizo hilo.

Mhe. Jenista ametoa maelekezo hayo wakati akizungumza na walengwa wa TASAF na wananchi wa Kijiji cha Bukulu wilayani Kondoa akiwa kwenye ziara ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini wilayani humo.

Mhe. Jenista amesema akiwa katika ukaguzi wa utekelezaji wa miradi ya TASAF hupenda kusikiliza shuhuda za walengwa pamoja na changamoto zinazowakabili, hivyo baada ya kusikia changamoto ya Bw. Laurent Chibu kutopata ruzuku ameamua kutoa maelekezo kwa Mtendaji wa Kijiji ili mlengwa huyo apate haki yake.

“Mtendaji nimekuuliza hapa na umekiri kwamba Bw. Laurent Kibu hajapata ruzuku yake kwasababu yeye na mwenzeke walikuwa safarini, hivyo nikupa muda wa kushughulikia suala hili mpaka kesho jioni na unipigie simu wewe mwenyewe kunieleza kuwa mlengwa huyu ameshapewa na wengine ambao bado wapewe ruzuku zao,” Mhe. Jenista amesisitiza.

Waziri Jenista amewataka watendaji na waratibu wa TASAF kote nchini kuhakikisha fedha zinazotolewa na Serikali kwa ajili ya walengwa wa TASAF zinawafikia walengwa kwa wakati, kama ambavyo Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ilivyokusudia.

Katika kuhakikisha ruzuku inawafikia walengwa kwa wakati, Mhe. Jenista amewataka walengwa wa TASAF kujisajili kwenye mfumo wa kidigitali wa simu ili waweze kuhawilishiwa ruzuku zao kupitia mitandao ya simu, na hatimaye kuondokana na changamoto ya kutopokea ruzuku zao kwa wakati.

“Watendaji na waratibu wa TASAF nisingependa kusikia mlengwa wa TASAF hajapewa ruzuku yake, iwe kwasababu ya kutokuwepo wakati wa dirisha au sababu nyingine yoyote ile kwani lengo la TASAF ni kuwawezesha walengwa kuboresha maisha yao,” Mhe. Jenista amefafanua.

Akieleza namna TASAF ilivyoboresha maisha yake, mlengwa wa TASAF wa Kijiji cha Bukulu, Bi. Rukia Kasi amesema ruzuku aliyoipata imemuwezesha kununua mbuzi na kuku wa kufuga, kusomesha watoto pamoja na kukarabati nyumba anayoishi na mme wake ambaye ni mlemavu wa macho.

Mlengwa mwingine wa TASAF wa Kijiji cha Bukulu, Bi. Mwanaidi Dohu amesema kuwa TASAF imemuwezesha kununua ng’ombe, kujenga nyumba ya kuishi, kuchimba kisima cha maji na kujishughulisha na kilimo cha migomba.

Naye, Bw. Abdilahi Ally ambaye ni mlengwa wa TASAF Kijiji cha Bukulu amesema licha ya ulemavu wake TASAF imemuwezesha kusomesha watoto wanne waliohitimu kidato cha nne na mmoja amemaliza kidato cha sita hivyo anaishukuru Serikali kupitia TASAF kwa kumuwezesha kumudu gharama za kuwasomesha watoto wake.

Serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) katika mwaka wa fedha 2021/2022 imetoa kiasi cha shilingi bilioni 2.6 katika Wilaya ya Kondoa kwa ajili ya kutekeleza Mpango wa Kuzinusuru Kaya Maskini wilayani humo.

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama akizungumza na walengwa wa TASAF na wananchi wa Kijiji cha Bukulu wilayani Kondoa wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini Wilayani humo.


Walengwa wa TASAF na wananchi wa Kijiji cha Bukulu wilayani Kondoa wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza nao wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri huyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini Wilayani humo.


Mkuu wa Wilaya ya Kondoa Dkt. Hamis Mkanachi akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama kuzungumza na walengwa wa TASAF na wananchi wa Kijiji cha Bukulu wilayani humo wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri huyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini Wilayani humo.


Mlengwa wa TASAF Kijiji cha Bukulu, Bw. Laurent Chebu akiwasilisha hoja yake kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama wakati akizungumza na walengwa wa TASAF na wananchi wa Kijiji cha Bukulu wilayani Kondoa wakati wa ziara ya kikazi ya Waziri huyo ya kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini Wilayani humo.


Mlengwa wa TASAF wa Kijiji cha Bukulu wilayani Kondoa, Bi. Rukia Kasi akieleza namna TASAF ilivyomuwezesha kuboresha maisha yake. 

Mlengwa wa TASAF wa Kijiji cha Bukulu wilayani Kondoa, Bw. Abdilahi Ally akieleza namna TASAF ilivyomuwezesha kuboresha maisha yake. 


 

No comments:

Post a Comment