Thursday, June 23, 2022

IDARA YA KUMBUKUMBU NA NYARAKA YAFANYA USAFI KITUO CHA MABASI DODOMA KUADHIMISHA WIKI YA UTUMISHI WA UMMA NA KUTEKELEZA KAULIMBIU YA KAZI IENDELEE


Na. James K. Mwanamyoto-Dodoma

Tarehe 23 Juni, 2022

Watumishi wa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa wamefanya usafi katika Kituo Kikuu cha Mabasi jijini Dodoma, ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, 2022 pamoja na kutekeleza kwa vitendo Kaulimbiu ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ya KAZI IENDELEE ambayo imekuwa ni chachu ya kuleta maendeleo katika taifa.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Bw. Firimin Msiangi akiwa katika eneo la Kituo Kikuu cha Mabasi Dodoma ambapo amewaongoza watumishi wa idara yake kufanya usafi katika kituo hicho.

Bw. Msiangi amesema kuwa, idara yake imeshiriki kufanya usafi katika eneo hilo kuungana na wananchi katika shughuli za kijamii kwani usafi ni muhimu na ni sehemu ya utekelezaji wa Kaulimbiu ya Mhe. Rais ya KAZI IENDELEE ambayo ni dira ya mafanikio katika sekta zote.

“Leo tumekuja hapa kufanya usafi katika stendi hii kuu ya Mabasi Dodoma ili kuliweka jiji la Dodoma katika hali ya usafi kwani mazingira ni afya, na ni sehemu ya utekelezaji wa kaulimbiu ya KAZI IENDELEE,” Bw. Msiangi amesisitiza.

Aidha, Bw. Msiangi amesema, shughuli hiyo ya usafi waliyoifanya ni utekelezaji wa maelekezo ya Katibu Mkuu-UTUMISHI, Dkt. Laurean Ndumbaro aliyezitaka taasisi zote za umma nchini kuadhimisha Wiki ya Utumishi wa Umma, 2022 kwa kushiriki shughuli mbalimbali za kijamii ili kujenga mahusiano mazuri na umma.

“Pamoja na kufanya kazi zetu za msingi maofisini, Katibu Mkuu-UTUMISHI alitutaka tushirikiane na wananchi katika shughuli mbalimbali za kijamii ili kuleta tija kwenye utoaji wa huduma kwa wananchi ikiwa ni pamoja na kuendeleza jitihada za Mhe. Rais za kuijali jamii,” Bw. Msiangi amefafanua. 

Kwa upande wake, mmoja wa watumishi wa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Bi. Joyce Maro amesema, wamefanya usafi katika stendi kuu ya mabasi Dodoma ili kuweka mazingira safi yatakayowaepusha  wananchi na magonjwa mbalimbali, kama ambavyo Mhe. Rais amekuwa akisisitiza usafi wa mazingira ili kuwa na taifa la watu wenye afya bora watakaoshiriki shughuli za maendeleo. 

Naye, Afisa Habari wa Kituo Kikuu cha Mabasi Dodoma, Bi. Qeen Mwasunga amesema, menejimenti ya kituo chake imefurahishwa na kitendo cha watumishi wa Idara ya Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa kufanya usafi kwenye eneo la kituo hicho jambo ambalo limemkumbusha ushiriki wa usafi wa mazingira, hivyo ametoa wito kwa taasisi nyingine kushiriki shughuli za mbalimbali za kijamii.

 

Mkurugenzi wa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Bw. Firimin Msiangi akieleza azma ya idara yake kufanya usafi eneo la Kituo Kikuu cha Mabasi Dodoma kama sehemu ya Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, 2022. 


Mkurugenzi wa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Bw. Firimin Msiangi akifanya usafi na watumishi wa idara yake katika Kituo Kikuu cha Mabasi Dodoma ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, 2022. 


Baadhi ya watumishi wa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa wakifanya usafi eneo la Kituo Kikuu cha Mabasi Dodoma ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, 2022. 


Mtumishi wa Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Bi. Joyce Maro katika kufanya usafi eneo la Kituo Kikuu cha Mabasi Dodoma ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, 2022.

 


Afisa Habari wa Kituo Kikuu cha Mabasi Dodoma, Bi. Qeen Mwasunga akiwashukuru  watumishi wa Idara ya Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa kwa kufanya usafi kwenye eneo la kituo hicho ikiwa ni sehemu ya mchango wao katika jamii. 


 

No comments:

Post a Comment