Thursday, May 27, 2021

WATUMISHI TOENI HUDUMA NZURI KWA WANANCHI NA WATUMISHI WENZENU ILI WANUFAIKE NA HUDUMA ZITOLEWAZO NA SERIKALI

Na. James K. Mwanamyoto-Kalambo

Tarehe 27 Mei, 2021

Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro amewataka Watumishi wa Umma wa Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo na maeneo mengine nchini kutekeleza kwa vitendo maelekezo ya Mheshimiwa Rais ya kutoa huduma nzuri kwa wananchi na watumishi wenzao ili wanufaike na huduma bora zitolewazo na Serikali yao kupitia Taasisi zake.

Dkt. Ndumbaro ametoa wito huo akiwa kwenye ziara ya kikazi Wilayani Kalambo yenye lengo la kuhimiza uwajibikaji kwa Watumishi wa Umma wilayani humo pamoja na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi hao katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku. 

Dkt. Ndumbaro amewaasa watumishi hao kuwajibika kikamilifu kwa kutoa huduma bora pindi wananchi wanapofuata huduma katika maeneo yao ya kazi kwani wameajiriwa kwa ajili ya kuwahudumia wananchi. 

Akizungumzia changamoto ya utoaji wa huduma kwa baadhi ya watumishi wa makao makuu ya Halmashauri za Wilaya au Taasisi za Umma, Dkt. Ndumbaro amewahimiza watumishi wote waliopo makao makuu kutoa kipaumbele cha utoaji huduma kwa wananchi na watumishi wanaolazimika kusafiri umbali mrefu ili kufuata huduma. 

Dkt. Ndumbaro amefafanua kuwa, kipaumbele cha huduma kikitolewa kwa wananchi na watumishi wanaosafiri umbali mrefu kufuata huduma, hawataingia gharama za malazi kwani watakuwa wamehudumiwa kwa wakati na kurejea katika makazi yao.

“Tumieni saa za kazi ipasavyo kwa kutoa huduma bora kwa wananchi na watumishi wanaolazimika kusafiri umbali mrefu kufuata huduma badala ya kutumia muda mwingi kwenye mambo yasiyo na tija kwa taifa, Dkt. Ndumbaro amesisitiza.” 

Ameongeza kuwa, Watumishi wanaposafiri umbali mrefu kufuata huduma na wasipopatiwa huduma stahiki kwa wakati, watumishi hao wanakosa morali ya kufanya kazi na hatimaye kushindwa kutoa huduma nzuri kwa wananchi hivyo kuibua malalamiko dhidi ya Serikali. 

Akitoa shukrani kwa niaba ya watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo, Mkuu wa TAKUKURU (W) Bi. Lupakisyo Mwakyolile amempongeza Dkt. Ndumbaro kwa kuitembelea wilaya hiyo iliyopo pembezoni, na kumshukuru kwa kusikiliza na kutatua kero na changamoto mbalimbali zilizokuwa zikiwakabili watumishi wa wilaya hiyo kwa muda mrefu. 

Bi. Mwakyolile amesema, ziara ya Dkt. Ndumbaro imejenga morali ya kufanya kazi kwa watumishi wa Wilaya ya Kalambo na kumhakikishia Dkt. Ndumbaro kuwa watachapa kazi kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan anavyosisitiza kupitia kaulimbiu yake isemayo KAZI IENDELEE.

Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro ameanza ziara ya kikazi mkoani Rukwa kwa kuitembelea Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo iliyopo pembezoni ili kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto zinazowakabili watumishi waliopo katika wilaya hiyo ambapo anatarajia kuhitimisha ziara hiyo kesho kwa kuzungumza na Watumishi wa Sekretarieti ya Mkoa wa Rukwa na baadae kuelekea mkoani Katavi kuhimiza uwajibikaji kwa watumishi waliopo katika mkoa huo.

 

 


Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro akizungumza na Watumishi wa Umma wa Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo wakati wa ziara yake ya kikazi Wilayani humo yenye lengo la kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto za watumishi hao. 


Watumishi wa Umma wa Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo wakimsikiliza Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro wakati wa ziara yake ya kikazi Wilayani humo yenye lengo la kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto za watumishi hao. 


Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo Bw. Palela Msongela akiwasilisha taarifa ya utekelezaji ya wilaya yake kwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro wakati wa ziara yake ya kikazi Wilayani humo yenye lengo la kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto za kiutumishi.


Mkurugenzi wa Idara ya Utawala wa Utumishi wa Umma, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bw. Mathew Kirama akijibu hoja za kiutumishi zilizowasilishwa wakati wa ziara ya kikazi ya Dkt. Laurean Ndumbaro ya kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto za watumishi wa Halmashauri Wilaya ya Kalambo. 


Mwalimu Shinuna Khalfan wa Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo akiwasilisha changamoto yake ya kiutumishi kwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro wakati wa ziara ya kikazi ya Katibu Mkuu huyo Wilayani humo yenye lengo la kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto za kiutumishi.


Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro akipitia changamoto na kero zilizowasilishwa kwake na Watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo ili azitatue. 


Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro akijibu hoja zilizowasilishwa na Watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo wakati wa ziara yake ya kikazi Wilayani humo yenye lengo la kuhimiza uwajibikaji na kutatua changamoto za kiutumishi. 


Mkuu wa TAKUKURU Wilaya ya Kalambo, Bi. Lupakisyo Mwakyolile akitoa neno la shukrani kwa niaba ya watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kalambo, mara baada ya Dkt. Ndumbaro kusikiliza na kutatua kero zinazowakabili watumishi wa Halmashauri hiyo.


 

No comments:

Post a Comment