Monday, March 24, 2025

WAZIRI SIMBACHAWENE : WATENDAJI WAKUU WA SERIKALI ACHENI KUWAONA WAKAGUZI WA NDANI KAMA MAADUI

Na. Lusungu Helela - MWANZA

 

 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.George Simbachawene amewataka  Watendaji Wakuu pamoja na Bodi ya Wakurugenzi  kuacha kuwachukulia Wakaguzi wa Ndani  kama maadui badala yake wawape ushirikiano ili Taasisi zao zisipate  hati chafu.

 

Amesema kumekuwa na kasumba iliyojengeka kwa Watendaji wengi wa Serikali ya kuwaona Wakaguzi hao wa Ndani kama sio Watumishi na wapo pale kwa ajili ya kuharibu mipango yao ilhali wao ni watu muhimu na jicho la Taasisi.

 

Mhe.Simbachawene ametoa kauli hiyo leo Machi 24, 2025 jijini Mwanza wakati akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan kufungua Mkutano wa tatu wa Wakaguzi wa Ndani wa Sekta ya Umma.

 

Amesema Mtendaji  yeyote wa Serikali  anayewatumia vizuri Wakaguzi wa Ndani hawezi kuingia kwenye matatizo ya ubadhirifu wa fedha za umma huku akisisitiza kuwa Wakaguzi hao wapo kwa ajili ya kumsaidia yeye na Taasisi anayoiongoza.

 

"Acheni kuwaona Wakaguzi wa Ndani kama wageni na watu wasiotakiwa kwenye maeneo yenu ya kazi badala yake watumieni ili kuhakikisha fedha za umma zinatumika  kwa ajili ya miradi ya maendeleo iliyokusudiwa.

 

Amesema Wakaguzi wa ndani wanatekeleza jukumu nyeti la kuhakikisha fedha za umma zinatumika kwa busara, uwazi na kwa madhumuni sahihi. " Bila kazi yenu, serikali haiwezi kufanya kazi kwa ufanisi" amesisitiza Simbachawene .

 

Katika hatua nyingine, Mhe.Simbachawene amewataka Wakaguzi hao kuhakikisha wanapata mafunzo ya mara kwa mara ili waweze kuendana na mabadiliko ya matumizi ya kidijitali katika ukaguzi wa fedha hususani katika matumizi ya akili mnemba (AI).

 

Ameongeza kuwa  '' Dunia inabadilika, teknolojia imeleta mageuzi ya jinsi tunavyofanya kazi, na kwa hiyo ukaguzi wa ndani na vyombo vya usimamizi wa taasisi navyo vinapaswa kubadilika.

 

Amesema matumizi ya mifumo hiyo imechangia mageuzi makubwa kwenye taasisi za serikali yenye hatua kubwa zaidi dhidi ya wanaobainika na matumizi mabaya ya fedha za umma.

 

Ameongeza kuwa kesi vikubwa zimechunguzwa na viongozi waliothibitika kuhusika, wameachishwa kazi, wameshtakiwa na fedha zilizochotwa wamezirejesha, akisema huo  ni ujumbe wa wazi kwamba utumishi wa umma ni kuwatumikia watu na sio wa kujinufaisha.

 

Amesema Serikali  imedhamiria kuwa na mfumo wa kuhakikisha  rasilimali zinasimamiwa ipasavyo. 

 

Kwa upande wake, Rais wa Taasisi ya Wakaguzi wa Ndani,  Dkt. Zelia Njeza amesema mahudhurio ya Wakaguzi wa Ndani  ni mazuri lakini kwenye ngazi ya Halmashauri yamekuwa hafifu hali inayochangia wataalamu hao kukosa mafunzo na hivyo kuendelea kufanya makosa yale yale kwenye kaguzi zao.

 

Amesema mkutano huo utafanyika kwa muda wa siku tano ambapo zaidi ya washiriki 800 watajifunza mbinu mbalimbali za ukaguzi ikiwemo  matumizi ya akili mnemba kwenye ukaguzi na hii inatokana na mabadiliko makubwa yanayotokea duniani kote katika ukaguzi wa fedha za umma.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.George Simbachawene akikabidhiwa tuzo ya kuthamini mchango kwa Wakaguzi wa ndani kutoka kwa Rais wa Taasisi ya Wakaguzi wa Ndani, Dkt. Zelia Njeza wakati akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan baada ya kufungua Mkutano wa tatu wa Wakaguzi wa Ndani wa Sekta ya Umma


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.George Simbachawene akizungumza wakati akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan baada ya kufungua Mkutano wa tatu wa Wakaguzi wa Ndani wa Sekta ya Umma  

Rais wa Taasisi ya Wakaguzi wa Ndani, Dkt.  Zelia Njeza akizungumza kabla ya kumakribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.George Simbachawene kuzungumza na Wakaguzi wa Ndani  wakati akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan baada ya kufungua Mkutano  huo wa tatu jijini Mwanza

Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Sengerema , Mhe. Senyi Ngaga  akizungumza na Wakaguzi wa Ndani kabla Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.George Simbachawene kuzungumza na Wakaguzi wa Ndani  wakati akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan baada ya kufungua Mkutano  huo wa tatu jijini Mwanza



Sehemu ya Wakaguzi wa Ndani wakimsikiliza  Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.George Simbachawene kuzungumza na Wakaguzi wa Ndani  wakati akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan baada ya kufungua Mkutano  huo wa tatu jijini Mwanza

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.George Simbachawene (katikati) akiwa ameongoza na  baadhi ya wenyeji wa Mkutano wa tatu wa Wakaguzi wa Ndani kwa ajili ya kufungua mkutano huo wakati akimwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan unaofanyika jijini Mwanza. Kulia ni Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Sengerema , Mhe. Senyi Ngaga na kushoto ni Rais wa Taasisi ya Wakaguzi wa Ndani,  Dkt. Zelia Njeza

UTUMISHI WASISITIZWA KUYAFAHAMU KIKAMILIFU MAADILI YA MSINGI YA OFISI NA KUYAZINGATIA KATIKA UTENDAJI

Na. Veronica Mwafisi-Dodoma

Tarehe 24 Machi, 2025

Watumishi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wamesisitizwa kuyafahamu kwa ufasaha maadili ya msingi ya Ofisi hiyo na kuyazingatia katika utekelezaji wa majukumu yao ili kufikia lengo la utoaji wa huduma bora kwa umma.

Hayo yamesemwa leo Machi 24, 2025 kwa nyakati tofauti na Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Xavier Daudi pamoja na Mwanasaikolojia Dkt. Chris Mauki wakati wa mafunzo yanayofanyika kila Jumatatu kwa watumishi wa ofisi hiyo kwenye Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.

Naibu Katibu Mkuu Daudi amesema ni wakati sasa wa watumishi hao kubadilika kiutendaji, “tubadilike ili tuwatumikie wadau wetu kwa weledi, tumepata somo zuri la mabadiliko ya utamaduni, mabadiliko haya yaanze na sisi na sio kwa kulazimishwa.” Amesisitiza.

Aidha, Bwana Daudi ametoa wito kwa watumishi hao kuwekeza katika maeneo mbalimbali ikiwemo katika taasisi za fedha ili watakapofikia umri wa kustaafu wasipate changamoto zozote katika kuendesha maisha yao nje ya utumishi wa umma.

“Tunashukuru tumepata pia elimu ya uwekezaji, kutoka Watumishi Housing Investments (WHI) nawashauri tuwekeze, tunaweza tukaanza kuwekeza kidogo kidogo mpaka ukifika muda wa kustaafu utakuwa umewekeza kwa kiasi kikubwa.” Amesisitiza Bw. Daudi

Awali, Mkurugenzi wa Fedha na Utawala-WHI, Bw. Pascali Massawe wakati akiwasilisha mada kuhusu Mfuko wa Uwekezaji wa Pamoja wa FAIDA FUND amesema lengo la kuanzishwa kwa mfuko huo ni kuwanufaisha Watanzania wote wa kipato cha chini, kati na cha juu ambao wamekuwa wakikabiliana na changamoto ya kupata mtaji wa kuwekeza kwenye masoko ya fedha na mitaji kwa ajili ya kuendesha shughuli mbalimbali za kiuchumi. 

Bw. Massawe amesema, gawio la Mfuko wa Faida linaleta tija kwa watu wote ambao watawekeza kwenye Mfuko huo kwa lengo la kujikwamua kiuchumi, hivyo WHI inaendelea kutoa elimu kwa watumishi wa umma na wananchi ili wajitokeze kwa wingi kununua vipande katika mfuko huo.

“Mfuko wa Faida ni salama kwa watu wote ambao wanataka kuepuka upotevu wa fedha, hivyo natoa wito kwa watumishi wote wa umma na wananchi kujitokeza kununua vipande ili wanufaike na uwekezaji katika mfuko huu,” Bw. Massawe amesisitiza.

Kwa upande wake, Mtaalam wa Saikolojia, Dkt. Chris Mauki wakati akiwasilisha mada kuhusu mabadiliko ya utamaduni, amesema endapo Watumishi wa Umma watakuwa na utamaduni wa kuzingatia maandiko waliyojiwekea kwenye taasisi basi wananchi watanufaika kwa kupata huduma bora kwa ustawi wa taifa.

 “Tumejiwekea maandiko mengi sana lakini hatuyafuati, tuna Dira, Dhima na Maadili ya Msingi katika Ofisi yetu, hivyo ili twende vizuri katika utendaji inabidi kuyazingatia haya,” Dkt. Mauki amesisitiza.

Dkt. Mauki ameongeza kuwa utamaduni unajengwa na mambo mengi ikiwemo tabia, matendo, miendendo, imani, alama, desturi na hadithi, hivyo amewaomba kujitathmini na kuwajibika pasipo kushurutishwa katika kuwatumikia Watanzania.

Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Xavier Daudi akisisitiza jambo wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo na kuimarisha utendaji kazi kwa watumishi wa ofisi hiyo yaliyofanyika katika Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.


Sehemu ya Wakurugenzi na Watumishi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, wakifuatilia mafunzo kuhusu mfuko wa uwekezaji wa pamoja wa FAIDA FUND yaliyofanyika katika ofisi hiyo iliyopo Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.


Mkurugenzi wa Fedha na Utawala-WHI, Bw. Pascali Massawe akiwasilisha mada kuhusu mfuko wa uwekezaji wa pamoja wa FAIDA FUND wakati wa mafunzo kwa watumishi wa ofisi hiyo yaliyolenga kuwajengea uwezo na kuimarisha utendaji kazi.


Mtaalam wa Saikolojia, Dkt. Chris Mauki akifafanua jambo kwa Wakurugenzi na Watumishi wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI wakati akiwasilisha mada kuhusu Utamaduni wa Taasisi au Ofisi kwenye mafunzo yanayotolewa katika ofisi hiyo lengo la kuwajengea uwezo na kuimarisha utendaji kazi.


Sehemu ya Wakurugenzi na Watumishi wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI, wakifuatilia mafunzo ya kuwajengea uwezo na kuimarisha utendaji kazi yaliyofanyika katika ofisi hiyo iliyopo Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.


Sehemu ya Wakurugenzi na Watumishi wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI, wakifuatilia mafunzo ya kuwajengea uwezo na kuimarisha utendaji kazi yaliyofanyika katika ofisi hiyo iliyopo Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.


Sehemu ya Watumishi wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI, wakifuatilia mafunzo ya kuwajengea uwezo na kuimarisha utendaji kazi yaliyofanyika katika ofisi hiyo iliyopo Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.



Wednesday, March 19, 2025