Friday, February 21, 2025

NAIBU WAZIRI SANGU ARIDHISHWA NA UTEKELEZAJI WA MIRADI YA MAENDELEO KUPITIA TASAF






 

NAIBU WAZIRI SANGU ARIDHISHWA NA UTEKELZAJI WA MIRADI YA TASAF MKOANI IRINGA

Na Lusungu Helela- IRINGA

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu ameridhishwa na utekelezaji wa miradi ya maendeleo iliyotekelezwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) mkoani Iringa huku akiitaka Mikoa mingine kuiga mfano wa Iringa kwenye matumizi bora ya  fedha za Mfuko huo.

Mhe.Sangu ametoa  pongezi hizo leo baada ya kutembelea na kukagua ujenzi  wa Kituo cha Afya cha Isele kilichopo Kata ya Mlenge, Halmashauri ya Manispaa ya  Iringa kinachoendelea kujengwa na TASAF.
Kituo hicho  cha Afya hadi kukamilika kwake  kitakuwa na uwezo wa kuwahudumia zaidi ya wananchi 12,000 na  kimelenga kupunguza vifo vya akina mama wajawazito pindi wanapojifungua pamoja na wagonjwa wengine.

Mhe. Sangu amesema Kituo hicho ni  moja ya vituo 15 vya Afya vya kimkakati  vinavyojengwa nchi nzima kupitia mradi wa  TASAF kwa mwaka wa fedha 2025/2026 

Amesema ujenzi wa vituo hivyo ni  kielelezo cha umakini wa Chama Cha Mapinduzi ( CCM)  katika kutekeleza Ilani yake ili kuhakikisha upatikanaji wa huduma  za afya  kwa wananchi wote pasipo kujali mazingira wanayoishi lengo likiwa ni kupunguza vifo hususan vya akina mama wanapojifungua.

Ninawapongeza wananchi wa Isele licha ya kuletewa fedha za ujenzi wa kituo hiki na TASAF  lakini nanyi mmejitolea kiasi cha Sh. milioni 19 na mmeshiriki kwenye kazi za kuchimba msingi pamoja na kusogeza mchanga, hii ni ishara ya uhitaji na utayari wa kukitumia Kituo hiki, amesisitiza Mhe.Sangu 

 Nimejionea majengo ikiwemo wodi la akina mama wajawazito pamoja na wodi ya wagonjwa wa kawaida  yana ubora na thamani ya fedha inaonekana, hongereni sana kwa usimamizi makini " 

Katika hatua nyingine, Mhe.Sangu ameridhishwa na ujenzi wa vivuko vya watembea kwa miguu vilivyojengwa katika maeneo korofi katika mitaa ya Ndwika na Kitwilu katika Manispaa ya Iringa  ambavyo vimekuwa msaada mkubwa kwa wanafunzi kwani walikuwa hawawezi kwenda shule pindi mvua ikinyesha.

"Watoto wetu walikuwa hawawezi kuvuka mvua ikinyesha, shughuli za kiuchumi pia zilikuwa zinasimama kwani wa upande wa pili  walikuwa hawawezi kuja kwetu na sisi tulikuwa hatuwezi kwenda upande wa pili" amesema Juma Mwakarobo mmoja wa wakazi wa eneo Kitwilu.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata hiyo, Mhe. Msafiri Nzalamoto  ametumia fursa hiyo kumshukuru Rais Mhe. Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kukubali kutoa fedha za ujenzi wa Kituo hicho katika eneo analoliongoza huku akibainisha kuwa Kituo hicho kitakuwa mkombozi kwa wananchi wake hususan akina mama wajawazito ambao wengi wao walikuwa wakipoteza maisha kutokana na kukosekana kwa huduma hiyo.

Ujenzi wa Kituo hiki umekuja wakati muafaka tunaahidi kukitunza ili kuhakikisha maono ya Rais wetu Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kupunguza vifo vya akina mama wajawazito yanatimia kwa wananchi wa Isele" amesema Mhe. Nzalamoto.

Awali Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF ambaye pia ni Mhandisi wa Miradi ya TASAF  Mhandisi Emmanuel Chuwa  alisema utekelezaji wa miradi unalengo la kuboresha huduma za kijamii katika maeneo ya wananchi Mkoani Iringa

 



Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu akizungumza leo na wananchi wa mtaa wa Kitwilu katika Halmashauri ya Manispaa ya Iringa mara baada ya kukagua na kutembelea miradi ya maendeleo iliyotekelezwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu akizungumza leo na wananchi wa kijiji cha Isele katika Halmashauri ya Manispaa ya Iringa mara baada ya kukagua na kutembelea Kituo cha Afya ikiwa ni moja ya  mradi ya maendeleo unaotekelezwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).



Sehemu ya wananchi wa Mtaa wa Ndyuka na Kitwilu katika  Halmashauri ya Manispaa ya Iringa wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu mara baada kutembelea na kukagua kivuko cha watembea kwa miguu 


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu akiwa ameongozana na wananchi wa Kijiji cha Isele mara baada ya kutembelea na kukagua Kituo cha Afya cha Isele kinachoendelea kujengwa katika eneo hilo. 
Baadhi ya majengo ya Kituo cha Afya cha Isele yanayojengwa kwa ufadhili wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) katika Halmashauri ya Manispaa ya Iringa. 



 Baadhi ya wananchi wa Mtaa wa Ndyuka na Kitwilu katika  Halmashauri ya Manispaa ya Iringa wakimshangilia Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu mara baada kutembelea na kukagua kivuko cha watembea kwa miguu 

 Baadhi ya wananchi wa Mtaa wa Ndyuka na Kitwilu katika  Halmashauri ya Manispaa ya Iringa wakimshangilia huku wakiagana naye  Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu mara baada kutembelea na kukagua kivuko cha watembea kwa miguu