Thursday, September 5, 2024

MHE. SANGU: UADILIFU NI MSINGI WA USALAMA WA TANZANIA

Na. Mwandishi Wetu

Septemba 5, 2024

“Tuwawajibishe au kuachana na watumishi wasiokuwa waadilifu kwa kuwa sisi ndio tunaotakiwa kusimamia uadilifu lakini miongoni mwetu tunakuwa na watu wasiokuwa waadilifu”

Maneno hayo yamesemwa na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Deus Sangu wakati akiongea na viongozi na watumishi wa TAKUKURU makao makuu Dodoma.

Amewakumbusha Viongozi na watumishi hao kuwa suala la uadilifu limeandikwa hata katika vitabu vya dini zote ambapo likizingatiwa kwa usahihi amani na utulivu hutamalaki miongoni mwa wananchi.

Alisema, TAKUKURU ni taasisi muhimu na nyeti katika taifa la Tanzania na msingi wake ni Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lengo ikiwa ni kuzuia na kupambana na rushwa katika jamii. Hivyo, Viongozi na watumishi wote wa Umma wakiongozwa na TAKUKURU hawanabudi kumuunga mkono Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mapambano hayo.

Mhe. Sangu ametoa rai kwa TAKUKURU kuangalia kwa kwa makini eneo la Ununuzi wa Umma ambapo zaidi ya asilimia 70 ya bajeti ya Serikali inaelekezwa katika eneo hilo. Hivyo, eneo hilo lazima litazamwe na kupewa kipaumbele ili kuziba mianya ya rushwa.

Aliongeza kuwa, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amepeleka fedha nyingi kwenye miradi ya maendeleo Tanzania nzima, hivyo ameielekeza TAKUKURU kufuatilia na kusimamia vyema miradi hiyo ili kuhakikisha inatekelezwa kwa mujibu wa mikataba.

Naye, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, Ikulu Bw. Mululi Majula Mahendeka amesema TAKUKURU ni muhimu kwa usalama wa nchi hasa katika kuzuia na kupambana na rushwa.

“Rushwa ikishamili na usalama wa nchi unateteleka kwa kuwa wananchi wanakosa imani na Serikali yao, hivyo  ametoa wito  kwa watumishi hao kufanya kazi kwa juhudu na maarifa ili Serikali iendelee kuiaminika kwa umma” alisisitiza Bw. Mahendeka.

Alibainisha kuwa, usiri na utengano sambamba ni jambo la msingi katika uendeshaji wa shughuli za Serikali na mambo hayo yasipozingatiwa na kutiliwa mkazo yanaweza kubomoa msingi wa umoja wa Taifa ambao uliwekwa na unaendelea kusimamiwa vyema na Viongozi wetu wakuu.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Bw. Crispin Chalamila alimuahidi Mhe. Sangu kupata ushirikiano wa dhati kutoka kwa Viongozi na Watumishi wa TAKUKURU ili kutekeleza majukumu aliyopewa kwa ufanisi.

Pia, alimuomba Mhe. Sangu kufikisha salaamu za shukurani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu akizungumza na Watumishi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wakati wa ziara yake ya kikazi iliyofanyika jijini Dodoma.

Baadhi ya Watendaji na Watumishi na wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza nao wakati wa ziara yake ya kikazi.

Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Bw. Crispin Chalamila akielezea utekelezaji wa majukumu ya ofisi hiyo kwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Deus Sangu (hayupo pichani) wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo iliyofanyika jijini Dodoma.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu (kushoto) akimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Bw. Crispin Chalamila (hayupo pichani) wakati akielezea utekelezaji wa majukumu ya ofisi hiyo alipofanya ziara ya kikazi. Kulia ni Katibu Mkuu-IKULU, Bw. Mululi Majula Mahendeka.

 

Baadhi ya Watumishi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza nao wakati wa ziara yake ya kikazi.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu akipokea baadhi ya vitendea kazi vya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wakati alipofanya ziara ya kikazi katika ofisi hiyo jijini Dodoma kwa lengo la kufuatilia utekelezaji wa majukumu na kuhimiza uwajibikaji.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu akisalimiana na baadhi ya Viongozi na Watumishi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wakati alipowasili katika ofisi hiyo kwa ziara ya kikazi jijini Dodoma.

Kwaya ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ikitoa elimu kupitia nyimbo wakati Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu alipofanya ziara katika ofisi hiyo kwa lengo la kufuatilia utekelezaji wa majukumu na kuhimiza uwajibikaji.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Watendaji wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) baada ya kuhitimisha ziara yake ya kikazi katika ofisi hiyo iliyopo jijini Dodoma.






No comments:

Post a Comment