Saturday, January 22, 2022

MHE. NDEJEMBI AELEKEZA TRILIONI 2.2 ZA TASAF ZILIZOTOLEWA NA MHE. RAIS ZITUMIKE KUWASAIDIA WAZEE, WANAWAKE, WALEMAVU NA VIJANA

 Na. Veronica Mwafisi-Songwe

Tarehe 22 Januari, 2022

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi amewataka waratibu wa TASAF kuhakikisha trilioni 2.2 zilizotolewewa na Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya Kuzinusuru Kaya Maskini zinatumika ipasavyo kuboresha maisha ya wazee, wanawake, walemavu na vijana walio katika kaya hizo.

Mhe. Ndejembi amesema, anatamani kuona walengwa wa TASAF wanasimamiwa vizuri ili wawe na vikundi vya ujasiriliamali ambavyo vitapata mkopo wa asilimia 10 katika Halmashauri na kutumia mikopo hiyo na ruzuku wanayoipata kunyanyua maisha yao kiuchumi.

“Walengwa wa TASAF wakiwemo wazee, wanawake, walemavu na vijana wakiunda vikundi na kujishughulisha na ujasiriamali watakuwa kwenye mazingira mazuri ya kujikwamua kutoka katika hali duni waliyonayo,” Mhe. Ndejembi amefafanua.

Aidha, Mhe. Ndejembi amewataka waratibu wa TASAF kuhakikisha wanashirikiana na wataalam wa Idara za kilimo, mifugo na maendeleo ya jamii kuwatembelea walengwa wa TASAF mara kwa mara ili kuwapatia ujuzi na utaalamu utakaowasaidia kuwa na vikundi bora vitakavyowawezesha kuboresha maisha yao.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji waTASAF Bw. Oscar Maduhu amemshukuru Mhe. Rais Samia Sulluhu Hassan, kwa kuwapatia kiasi kikubwa cha fedha kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi huo wa TASAF.

Bw. Maduhu amesema, katika kuhakikisha mradi huo wa TASAF unatekelezwa vizuri, wamejipanga kuhakikisha wanawawezesha walengwa kuondokana na lindi la umaskini na kuwa na hali bora ya maisha.

Mhe.  Ndejembi amehitimisha ziara yake ya kikazi katika mikoa ya Rukwa na Songwe aliyoifanya kwa lengo la kuhimiza uwajibikaji kwa Watumishi wa Umma na kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kuzinusuru Kaya Maskini.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akifafanua jambo kwa wandishi wa habari kuhusu ziara ya kikazi aliyoifanya katika mikoa ya Rukwa na Songwe iliyokuwa na lengo la kuhimiza uwajibikaji kwa Watumishi wa Umma na kukagua utekelezaji wa miradi wa TASAF katika mikoa hiyo.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akisikiliza swali toka kwa mwandishi wa habari kuhusu ziara yake ya kikazi aliyoifanya katika mikoa ya Rukwa na Songwe iliyokuwa na lengo la kuhimiza uwajibikaji kwa Watumishi wa Umma na kukagua utekelezaji wa miradi wa TASAF katika mikoa hiyo.


Muwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF, Bw. Oscar Maduhu (Wakwanza kushoto) akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya utekelezaji wa mradi wa TASAF katika mikoa ya Rukwa na Songwe mara baada ya kukamilika kwa ziara ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi ya kukagua utekelezaji wa miradi wa TASAF katika ya mikoa hiyo.




No comments:

Post a Comment