Tuesday, October 26, 2021

SITARAJII KUSIKIA MTUNZA KUMBUKUMBU NA NYARAKA ANAVUJISHA SIRI ZA SERIKALI-Mhe Mchengerwa


Na. Nasra H. Mondwe-Arusha

Tarehe 26 Oktoba, 2021

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa amewataka Watunza Kumbukumbu na Nyaraka katika taasisi za umma kutekeleza majukumu yao kwa weledi ili kujiepusha na uvujishaji wa siri za serikali.

Mhe. Mchengerwa ametoa wito huo wakati akifungua Mkutano wa 9 wa Chama cha Taaluma ya Menejimenti ya Kumbukumbu na Nyaraka Tanzania katika ukumbi wa ACC jijini Arusha.

Mhe. Mchengerwa amesema, dhamana waliyonayo Watunza Kumbukumbu ni kubwa, hivyo ni vema wakazingatia Sheria, Kanuni na Taratibu za utunzaji wa kumbukumbu pamoja na viapo vyao kwasababu utoaji wa siri za Serikali ni kosa kubwa kisheria na kwa mujibu wa taratibu za Utumishi wa Umma.

Waziri Mchengerwa amewaasa washiriki wa Mkutano huo kuhakikisha wanajiepusha na siasa na mambo mengine yanayosababisha kutoa siri za Serikali.

Mhe. Mchengerwa amesisitiza kuwa, Serikali ya Awamu Sita inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan inathamini mchango wa Watumishi wa Umma na itaendelea kulinda maslahi yao ikiwa ni pamoja na kutatua changamoto zinazowakabili Watunza Kumbukumbu, hivyo hakuna sababu ya watumishi kutoa siri za Serikali na badala yake wanapaswa kuwa waadilifu kiutendaji na kuwa watiifu kwa Serikali yao.

Akizungumzia juu ya stahiki mbalimbali za Watumishi wa Umma, Mhe Mchengerwa amewaagiza waajiri wote kuhakikisha wanalipa stahili zote za watumishi ikiwepo madai ya malimbikizo ya mishahara na kuongeza kuwa wanapaswa kutenga muda wa kusikiliza kero za watumishi na kuzitafutia uvumbuzi.

Mhe. Mchengerwa amewasisitiza waajiri kuheshimu kada zote kwani kila kada ina umuhimu wake katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku ya Serikali.

 “Waajiri ziheshimuni kada zote, msidharau kada za watu wa chini kwani hawa ni watu muhimu katika utekelezaji wa majukumu yetu na sisi kama Serikali tutaendelea kuzipigania kada hizi,” Mhe. Mchengerwa amesisitiza.

Akimkaribisha Mhe. Mchengerwa kufungua mkutano huo, Mwenyekiti wa Chama cha Taaluma ya Menejimenti ya Kumbukumbu na Nyaraka Tanzania (TRAMPA), Bi. Josephine Manase amesema lengo la chama chao ni kujengeana uwezo na kupeana hamasa ya utekelezaji wa majukumu kwa ufanisi ili kutoa mchango katika utekelezaji wa majukumu ya Serikali ya kila siku.

Aidha, Bi. Manase amemuomba Mhe. Mchengerwa kwa nafasi ya uongozi aliyonayo kukisaidia chama chake kumuomba Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kuwa Mgeni Rasmi katika Mkutano ujao wa 10 wa Chama cha Taaluma ya Menejimenti ya Kumbukumbu na Nyaraka Tanzania utakaofanyika Zanzibar, ikizingatiwa kuwa kazi ya kwanza ya Mhe. Rais ilikuwa ni ya utunzaji wa kumbukumbu Serikalini.

Mkutano huo wa siku tatu unaongozwa na kauli mbiu isemayo “Imarisha Utunzaji wa Kumbukumbu na Nyaraka ili kuwezesha Uwazi, Uwajibikaji na Utawala Bora katika Kutoa Huduma kwa Umma.”

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa akizungumza na washiriki wa mkutano mkuu wa 9 wa Chama cha Taaluma ya Menejimenti ya Kumbukumbu na Nyaraka Tanzania alipokuwa akifungua mkutano huo jijini Arusha. 


Baadhi ya washiriki wa mkutano mkuu wa 9 wa Chama cha Taaluma ya Menejimenti ya Kumbukumbu na Nyaraka Tanzania wakimsikiliza   Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa (hayupo pichani) alipokuwa akifungua mkutano huo jijini Arusha.


Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Dkt. Francis Michael akitoa ufafanuzi wa masuala ya kiutumishi wakati wa mkutano mkuu wa 9 wa Chama cha Taaluma ya Menejimenti ya Kumbukumbu na Nyaraka Tanzania jijini Arusha. 


Mwenyekiti wa Chama cha Taaluma ya Menejimenti ya Kumbukumbu na Nyaraka Tanzania, Bi. Josephine Manase akielezea lengo la mkutano wa chama chao kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa kufungua mkutano mkuu wa 9 wa Chama cha Taaluma ya Menejimenti ya Kumbukumbu na Nyaraka Tanzania jijini Arusha. 


Katibu wa Chama cha Taaluma ya Menejimenti ya Kumbukumbu na Nyaraka Tanzania, Bw. Francis Mathias akitambulisha makundi ya washiriki wa mkutano wa mkuu wa 9 wa Chama cha Taaluma ya Menejimenti ya Kumbukumbu na Nyaraka Tanzania jijini Arusha. 


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa akipokea tuzo kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan ya kutambua mchango mahili wa Mhe. Rais katika kuendeleza taaluma ya menejimennti ya utunzaji wa kumbukumbu na nyaraka na kwa uongozi wa uwazi na uwajibikaji, wakati wa mkutano mkuu wa 9 wa Chama cha Taaluma ya Menejimenti ya Kumbukumbu na Nyaraka Tanzania jijini Arusha.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa akipokea tuzo kutambua mchango wake wa kuunga mkono juhudi za utunzaji wa kumbukumbu na nyaraka katika Utumishi wa Umma wakati wa mkutano mkuu wa 9 wa Chama cha Taaluma ya Menejimenti ya Kumbukumbu na Nyaraka Tanzania jijini Arusha.


Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Dkt. Francis Michael akipokea cheti kwa niaba ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora cha kutambua mchango wa Ofisi hiyo kwa Watunza Kumbukumbu na Nyaraka wakati wa mkutano mkuu wa 9 wa Chama cha Taaluma ya Menejimenti ya Kumbukumbu na Nyaraka Tanzania jijini Arusha. 


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Watendaji kutoka taasisi za umma walioshiriki mkutano mkuu wa 9 wa Chama cha Taaluma ya Menejimenti ya Kumbukumbu na Nyaraka Tanzania mara baada ya kufungua mkutano huo jijini Arusha. 


 

No comments:

Post a Comment