Wednesday, October 20, 2021

HALMASHAURI ZATAKIWA KUANDAA MPANGO WA RASILIMALIWATU NA URITHISHANAJI MADARAKA UTAKAOBORESHA UTENDAJI KAZI KATIKA UTUMISHI WA UMMA

 Na. Veronica E. Mwafisi-Dodoma

Tarehe  20 Oktoba, 2021

Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bw. Hassan Kitenge amezitaka Halmashauri kuandaa Mpango wa Rasilimaliwatu na Urithishanaji Madaraka ili kuwezesha taasisi za umma kutoa huduma bora na endelevu.

Bw. Kitenge amesema hayo leo Jijini Dodoma, wakati akifungua mafunzo ya kuandaa Mpango wa Rasilimaliwatu na Urithishanaji Madaraka kwa Maafisa Utumishi Waandamizi wa Halmashauri za Mikoa ya Mara, Kigoma, Singida na Dodoma. 

Amesema, kutokana na Sheria ya Utumishi wa Umma ya Mwaka 2002 na Sera ya Menejimenti ya Ajira ya Mwaka 2008, waajiri katika Wizara na Taasisi za umma  wamepewa sehemu kubwa ya majukumu  ya kusimamia masuala muhimu yanayohusu watumishi wao, hivyo Mpango wa Rasilimaliwatu na Urithishanaji Madaraka ni nyenzo muhimu katika usimamizi wa watumishi.

Amefafanua kuwa, bila kuwa na jitihada na mipango mahususi, Halmashauri zinaweza kuwa na watumishi wachache  wenye sifa na uwezo wa kujaza nafasi za madaraka pindi zitakapokuwa wazi, hivyo kuwepo kwa mipango hiyo kutawezesha  kusimamia rasilimaliwatu kwa utaratibu mzuri pamoja na kubaini mahitaji na upatikanaji  wa rasilimaliwatu kwa wakati.

“Halmashauri zinatakiwa kuwa na watumishi wa kutosha wenye sifa na uwezo unaotakiwa mahali pa kazi ili kuleta tija na kuboresha utendaji kazi kwa lengo la kutoa huduma bora kwa umma,” Bw. Kitenge amesisitiza.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Mkurugenzi Msaidizi Rasilimaliwatu – TAMISEMI, Bw. Marko Masaya, ameishukuru Ofisi ya Rais-UTUMISHI kwa kuandaa mafunzo hayo ambayo yatawasaidia kuandaa Mipango ya Rasilimaliwatu na Urithishanaji Madaraka kwa usahihi.

Bw. Masaya amemhakikishia Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais UTUMISHI kuwa Ofisi ya Rais – TAMISEMI kama wasimamizi wa Mamlaka ya Serikali za Mitaa watahakikisha maelekezo ya Ofisi ya Rais – UTUMISHI yanatekelezwa kikamilifu.

Akimkaribisha Kaimu Katibu Mkuu-UTUMISHI kufungua mafunzo hayo, Kaimu Mkurugenzi Idara ya Uendelezaji Rasilimaliwatu, Ofisi ya Rais – UTUMISHI, Dkt. Edith Lwiza amesema mafunzo hayo yanafanyika kwa muda wa wiki moja na yanashirikisha washiriki kutoka Halmashauri za Sekretarieti za Mikoa ya Mara, Kigoma, Singida na Dodoma.

Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bw. Hassan Kitenge akifungua Mafunzo ya Kuandaa Mpango wa Rasilimaliwatu na Urithishanaji Madaraka kwa Maafisa Utumishi Waandamizi wa Halmashauri  za Mikoa ya Mara, Kigoma, Singida na Dodoma yanayofanyika katika Ukumbi wa VETA jijini Dodoma.


Kaimu Mkurugenzi Idara ya Uendelezaji Rasilimaliwatu Ofisi ya Rais – UTUMISHI, Dkt. Edith Lwiza, akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bw. Hassan Kitenge kufungua Mafunzo ya Kuandaa Mpango wa Rasilimaliwatu na Urithishanaji Madaraka kwa Maafisa Utumishi Waandamizi wa Halmashauri za Mikoa ya Mara, Kigoma, Singida na Dodoma yanayofanyika katika Ukumbi wa VETA jijini Dodoma.


Baadhi ya washiriki wa Mafunzo ya Kuandaa Mpango wa Rasilimaliwatu na Urithishanaji Madaraka wakimsikiliza Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bw. Hassan Kitenge (hayupo pichani) wakati akifungua mafunzo hayo yanayofanyika katika Ukumbi wa VETA jijini Dodoma.


Mwakilishi wa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Mkurugezi Msaidizi Rasilimaliwatu – TAMISEMI, Bw. Marko Masaya, akiishukuru Ofisi ya Rais-UTUMISHI kwa kuandaa Mafunzo ya Kuandaa Mpango wa Rasilimaliwatu na Urithishanaji Madaraka kwa Maafisa Utumishi Waandamizi wa Halmashauri za Mikoa ya Mara, Kigoma, Singida na Dodoma yanayofanyika katika Ukumbi wa VETA jijini Dodoma.


Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Bw. Hassan Kitenge akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa Mafunzo ya Kuandaa Mpango wa Rasilimaliwatu na Urithishanaji Madaraka kwa Maafisa Utumishi Waandamizi wa Halmashauri za Mikoa ya Mara, Kigoma, Singida na Dodoma yanayofanyika katika Ukumbi wa VETA jijini Dodoma.



No comments:

Post a Comment