Tuesday, October 12, 2021

MHESHIMIWA RAIS ANATAKA WATUMISHI WA UMMA KUFANYA KAZI KWA UADILIFU BILA KUSHINIKIZWA-Mhe. Mchengerwa

Na. James K. Mwanamyoto-Dodoma

Tarehe 12 Oktoba, 2021

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa amewataka Watumishi wa Umma kuwa na utamaduni wa kufanya kazi kwa uadilifu bila kushinikizwa wakati wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kama ambavyo Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa akisisitiza.

Mhe. Mchengerwa ametoa wito huo leo ofisini kwake, wakati wa mkutano wake na Waandishi wa Habari uliolenga kutoa mrejesho wa masuala ya kiutumishi yaliyojitokeza wakati wa ziara yake ya kikazi aliyoifanya hivi karibuni katika Mikoa ya Mwanza, Mara na Simiyu.

Mhe. Mchengerwa amesema, Mhe. Rais amedhamiria kuwa na watendaji waadilifu, hivyo ofisi yake imejipajipanga kuhakikisha watumishi wote wa umma wanasimamia vema fedha zinazotolewa kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo.

Ameongeza kuwa, Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan atajisikia fahari kuona  Watumishi wa Umma wanatekeleza majukumu yao kikamilifu bila kushinikizwa na viongozi wao.

“Inawezekana wapo baadhi ya watumishi wanataka kutekeleza wajibu wao kwa kushinikizwa jambo ambalo Mhe. Rais halitaki kwani anataka kila mtumishi awajibike bila kusimamiwa,” Mhe. Mchengerwa amesisitiza.

Aidha, Mhe. Mchengerwa amewataka Watumishi wa Umma nchini kuzingatia maelekezo ya Mhe. Rais kuhusu utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO 19 aliyoyatoa tarehe 10 Oktoba, 2021.

Amewaasa Watumishi wa Umma kutekeleza mpango huo kwa weledi, uadilifu na uzalendo ili ukamilike kwa wakati na kuwa na manufaa kwa wananchi na maendeleo ya taifa kwa ujumla.

“Kama ambavyo Mhe. Rais amesisitiza, muda wa utekelezaji wa mpango huo ni miezi 9 tu, hivyo hakutakuwa na muda wa nyongeza,” Mhe. Mchengerwa amefafanua.

Mhe. Mchengerwa amesema, Watumishi wa Umma waliopewa dhamana ya kusimamia mradi huo wanapaswa kutekeleza mradi kwa weledi na uzalendo ili kumuenzi Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Mchango wa Watumishi wa Umma katika Utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO ni muhimu kwa maendeleo na ustawi wa taifa. 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa (wapili kutoka kulia) akizungumza na Waandishi wa Habari (hawapo pichani) leo jijini Dodoma kuhusu mrejesho wa masuala ya kiutumishi yaliyojitokeza wakati wa ziara yake ya kikazi aliyoifanya katika Mikoa ya Mwanza, Mara na Simiyu.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.Deogratius Ndejembi (aliyesimama) akimkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa wakati wa kikao cha Mhe. Mchengerwa na Waandishi wa Habari kilichofanyika leo jijini Dodoma kuhusu mrejesho wa masuala ya kiutumishi yaliyojitokeza wakati wa ziara yake ya kikazi aliyoifanya katika Mikoa ya Mwanza, Mara na Simiyu. 


Baadhi ya Watendaji wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa alipokuwa akizungumza na Waandishi wa Habari leo jijini Dodoma kuhusu mrejesho wa masuala ya kiutumishi yaliyojitokeza wakati wa ziara yake ya kikazi aliyoifanya katika Mikoa ya Mwanza, Mara na Simiyu.


Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro (aliyesimama) akitoa neno la utangulizi kabla ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa kuzungumnza na Waandishi wa Habari leo jijini Dodoma kuhusu mrejesho wa masuala ya kiutumishi yaliyojitokeza wakati wa ziara yake ya kikazi aliyoifanya katika Mikoa ya Mwanza, Mara na Simiyu.



No comments:

Post a Comment