Friday, December 4, 2015

WATENDAJI WATAKAOSHINDWA KUONDOA TAKWIMU CHAFU KUSIMAMISHIWA MISHAHARA


Serikali itawaondoa katika orodha ya malipo ya Serikali Katibu Tawala na Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa watakaoshindwa kusimamia kwa weledi zoezi la kuondoa taarifa zisizotakiwa (chafu) katika Mfumo wa Taarifa za Kiutumishi na Mishahara (HCMIS) kabla ya mwisho wa mwezi Desemba 2015.

Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma Bw. Tixon Nzunda ametoa maelekezo hayo katika kikao kazi kilichoendeshwa kwa njia ya Video (Video Conference)  iliyokutanisha kwa pamoja mikoa kumi na mbili (12) ambayo ni  Arusha, Kagera, Tanga, Tabora, Manyara, katavi, kilimanajaro, Simiyu, Dar es salaam, Rukwa, Mwanza na Mbeya.

Bw. Nzunda katika kikao hicho alisema ni jukumu la waajiri kuhakikisha usimamizi wa rasilimaliwatu ni mzuri ili kuepuka malalamiko miongoni mwa Watumishi na kuwezesha wananchi kupokea huduma kwa kiwango kinachotakiwa kutoka Serikalini.
“Mamlaka ambayo itashindwa kusafisha takwimu chafu watendaji na wahusika wote wataondolewa katika orodha ya malipo kwa sababu watakuwa wameshindwa kutimiza wajibu wao” Bw. Nzunda alisema na kusisitiza kuwa zoezi hilo lifanyike kabla ya mwisho wa mwezi Desemba 2015.

Kaimu Katibu Mkuu Bw. Nzunda alisema ni jambo la msingi kuzingatia misingi ya weledi, uwajibikaji na utalaamu katika kutekeleza majukumu na kutoa tahadhari kwa Maafisi Utumishi wasiowajibika kuchukulia hatua stahiki.

Maelekezo mengine yaliyotolewa kwa Watendaji Wakuu wote wa Serikali ni kuhakikisha kila mtumishi anafika mahala pa kazi saa moja na nusu asubuhi (01:30) na kusaini kitabu muda wa kufika na kutoka.

Watumishi wa Umma kuwa na kitambulisho chenye jina na cheo husika na huduma zinazotolewa ziwe zenye tija na kutolewa kwa wakati. Pamoja na hilo, Ofisi za malalamiko zifanye kazi na kuanzisha dawati la kuwasikiliza wateja.

Vitengo vya Habari Serikalini viimarishwe ili Umma uhabarishwe ipasavyo na kwa wakati kuhusu kazi mbalimbali na huduma zinazotolewa na Serikali.

Watumishi wote wa Umma waweke Ahadi ya Uadilifu kwa Umma wakati wa Wiki ya Uadilifu. Fomu ya kuweka Ahadi ya Uadilifu inapatikana katika Tovuti ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma yenye anuani www.utumishi.go.tz . Ofisi ya Rais-Utumishi itafuatilia utekelezaji wa kiapo hicho.

Pamoja na maelekezo hayo, Bw. Nzunda alifafanua kuhusu mafunzo ndani na nje ya nchi kuwa maagizo yaliyotolewa yanapotoshwa na kusisitiza kuwa safari na mafunzo yenye masilahi kwa nchi yanaruhusiwa kwa kibali kuombwa kwa Mkuu wa Utumishi wa Umma.  
Katibu Mkuu Bw. Nzunda alisisitiza suala la nidhamu katika utendaji kazi na pale inapokiukwa hatua stahiki za kinidhamu zichukuliwe mara moja kwa Watumishi wasiotaka kutumiza wajibu wao.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini

Kny: Katibu Mkuu-Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma

No comments:

Post a Comment