Wednesday, May 27, 2026

KATIBU MKUU-UTUMISHI AWAITA DODOMA WAKUU WA IDARA NA VITENGO VYA UTAWALA NA USIMAMIZI WA RASILIMALIWATU SERIKALINI.

Na Antonia Mbwambo na Eric Amani-Dodoma

Tarehe 26 Mei, 2026

Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI,   Bw. Juma Mkomi, amewasisitiza Wakuu wa Idara na Vitengo vya Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu Serikalini kushiriki kikao kazi muhimu kilichopangwa kufanyika tarehe 1-3 Juni, 2026 katika ukumbi wa mabele hall jijini Dodoma.

Bw. Mkomi ametoa msisitizo huo Mei 26, 2026 wakati wa Mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI uliopo Mtumba jijini Dodoma

“Natoa wito kwa Wakuu wa Idara na vitengo vya Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu kuhudhuria wao wenyewe katika kikao hicho bila kukosa kwakuwa kikao hiki kitakuwa na maelekezo mahususi ya kuboresha utendaji kazi.” Bw. Mkomi alisema.

Aidha, Bw. Mkomi amebainisha kuwa kikao hicho kitajadili na kufafanua kuhusu matumizi ya Mifumo mbalimbali ya kidijiti ikiwemo e-uhamisho, e-watumishi, e-utendaji, e-mrejesho na hr-assesment kwa kuzingatia shabaha za vipaumbele vya Taifa kuelekea dira 2050.

Ameongeza kuwa kikao hicho kitatoa nafasi ya kujadili kuhusu changamoto na mafanikio yaliyopo katika utawala na usimamizi wa rasilimaliwatu na mapendekezo ya namna bora ya kuzishughulikia changamoto hizo. Pia washiriki watapata fursa ya kubadilishana uzoefu na kuimarisha utendaji kazi katika Taasisi za Umma.

Bw. Mkomi amewataka washiriki kujisajili katika mfumo kupitia link ya tsms.gov.go.tz huku wakizingatia kwamba mwisho wa usajili ni tarehe 29 Juni, 2026.

Vile vile, Wakuu wa Idara na vitengo vya Usimamizi wa Rasilimaliwatu wamesisitizwa kufika katika ukumbi wa Mabele Hall uliopo jijini Dodoma tarehe 31 Mei, 2026 kuanzia saa 4 asubuhi kwa ajili ya kuchukua vitambulishi vyao vitakavyotumika katika kikao hicho.Kikao kazi hicho kitaongozwa na kauli mbiu isemayo; “Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu katika Utumishi wa ulio Sikivu,Jumuishi wenye Matokeo na Uwajibikaji kuelekea Dira 2050”.

Mwandishi wa Habari kutoka kituo cha habari cha ITV Ndg. Michael Msilo akimuuliza swali katibu Mkuu Ofisi ya Rais – UTUMISHI Bw. Juma Mkomi (hayupo pichani) kwenye mkutano na waandishi hao leo Mei 26, 2026 juu ya Kikao kazi cha Wakuu wa Idara za Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu katika Wizara, Idara zinazojitegemea pamoja na Wakala wa serikali za Mtaa kinachotarajiwa kufanyika Juni 1 hadi 3 jijini Dodoma


Baadhi ya Waandishi wa Habari wakimsikiliza katibu Mkuu Ofisi ya Rais – UTUMISHI Bw. Juma Mkomi (Katikati) wakati walipohudhuria mkutano wa waandishi wa habari katika ukumbi wa ofisi hiyo uliyopo Mtumba Jijini Dodoma Mei 26, 2026




Mwandishi wa Habari kutoka kituo cha habari cha BBC Ndg. Ronald Sonyo akimuuliza swali katibu Mkuu Ofisi ya Rais – UTUMISHI Bw. Juma Mkomi (hayupo pichani) kwenye mkutano na waandishi hao leo Mei 26, 2026 juu ya Kikao kazi cha Wakuu wa Idara za Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu katika Wizara, Idara zinazojitegemea pamoja na Wakala wa serikali za Mtaa kinachotarajiwa kufanyika Juni 1 hadi 3 jijini Dodoma  


Baadhi ya Wakurugenzi Wakuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakimsikiliza Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma Bw. Juma Mkomi (hayupo pichani) wakati akifanya mkutano na waandishi wa habari katika ukumbi wa ofisi hiyo leo Mei 26, 2026 Mtumba, Dodoma.




No comments:

Post a Comment