Monday, January 27, 2025

WATUMISHI WA OFISI YA RAIS-UTUMISHI WASISITIZWA KUZINGATIA ITIFAKI NA DIPLOMASIA KATIKA UTENDAJI KAZI

Na. Mwandishi Wetu

Tarehe 27 Januari, 2025.

Watumishi wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI wamesisitizwa kuzingatia Itifaki na Diplomasia katika utendaji kazi Ili kujenga heshima ya ofisi kwa manufaa ya nchi.

Wito huo umetolewa leo Januari 27, 2025 na Balozi Nelson Lyimo (mstaafu) wakati akifanya wasilisho kuhusu Itifaki na Diplomasia kwa Watumishi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora katika Mji wa Serikali Mtumba, Jijini Dodoma.

Balozi Lyimo amesema, Ofisi ya Rais-UTUMISHI ni muhimu kwa Taifa la Tanzania kwa kuwa inasimamia rasilimaliwatu, hivyo Watumishi wake wanatakiwa kuzingatia Itifaki na Diplomasia wakati wote wanapotekeleza majukumu yao katika ofisi hiyo.

Amewasisitiza Watumishi kuwa wasikivu kwa wateja wanaowahudumia na kuona namna ya kuwasaidia kupata majibu au suluhisho la suala ambalo mteja husika ameliwasilisha.

“Niwaombe kila mtumishi wa ofisi hii ajipime namna anavyotoa huduma kwa wateja kwani ndio kipimo cha tabia njema wakati wa utendaji kazi, jambo ambalo litaenda kuitangaza ofisi vizuri kwa maslahi mapana ya taifa,” amesisitiza Balozi Lyimo.

Akihitimisha mafunzo ya kuwajengea uwezo watumishi hao, Mkurugenzi wa Idara ya Usimamizi wa Rasilimaliwatu na Utawala, Bw. Musa Magufuli alimshukuru Balozi Lyimo kwa kutoa elimu hiyo kwa watumishi hao ambayo itaboresha utendaji kazi kwa watumishi wao.

Ofisi ya Rais-UTUMISHI iliandaa utaratibu wa kutoa mafunzo kwa watumishi wake kila Jumatatu ya wiki kwa lengo la kutoa uelewa kuhusu masuala mbalimbali katika Utumishi wa Umma ili kutekeleza majukumu yao ipasavyo kwa ustawi wa Taifa.

Balozi Nelson Lyimo (mstaafu) akizungumza wakati akiwasilisha mada kuhusu Itifaki na Diplomasia kwenye mafunzo ya kuwajengea uwezo watumishi wa Ofisi ya Rais-UTUMISHI yaliyofanyika katika Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimaliwatu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Musa Magufuli (aliyesimama mbele kulia) akitoa shukrani kwa  Balozi Nelson Lyimo (aliyesimama mbele kushoto) mara baada ya Balozi huyo kuhitimisha mada kuhusu Itifaki na Diplomasia wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo watumishi wa ofisi hiyo yaliyofanyika katika Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.

Sehemu ya Watumishi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, wakifuatilia mafunzo ya kuwajengea uwezo watumishi hao katika masuala ya utendaji kazi yaliyofanyika katika ofisi hiyo iliyopo Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.





No comments:

Post a Comment