Thursday, April 28, 2022

WATAALAM WA TEHAMA SERIKALINI WATAKIWA KUPATA KIBALI CHA MAMLAKA YA SERIKALI MTANDAO KABLA YA KUTEKELEZA MIRADI YA TEHAMA ILI KUTOPOTEZA MAPATO YA SERIKALI

 Na. Veronica Mwafisi-Dodoma

Tarehe 28 Aprili, 2022

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama amezitaka Taasisi zote za Umma nchini kupata kibali cha Mamlaka ya Serikali Mtandao kabla ya kutekeleza Miradi ya TEHAMA ili kuondoa changamoto ya kutowasiliana na kubadilishana taarifa kwa mifumo hiyo na hatimaye kupoteza mapato ya Serikali.

Akifungua kikao kazi cha Wakuu wa Idara na Vitengo vya TEHAMA Serikalini jijini Dodoma, Mhe. Jenista amesema iwapo utekelezaji wa Mifumo na Miundombinu ya TEHAMA utawianishwa na kuwezesha ubadilishanaji wa taarifa ndani ya taasisi za umma na baina ya taasisi za umma, utoaji wa huduma kwa njia ya mtandao utakuwa ni kichocheo muhimu katika kufikia maendeleo yanayokusudiwa kwa taifa.

Mhe. Jenista amesema Serikali ilianzisha Mamlaka ya Serikali Mtandao kupitia Sheria ya Serikali Mtandao Na. 10 ya Mwaka 2019, na kuipa jukumu la kusimamia, kuratibu na kuendeleza utekelezaji wa Serikali Mtandao, pamoja na kusimamia uzingatiaji wa Sheria, Kanuni, Viwango na Miongozo ya Serikali Mtandao katika Taasisi za Umma.

Amesema pamoja na uanzishwaji wa Mamlaka hiyo bado kumekuwa na changamoto mbalimbali ikiwemo mifumo isiyowasiliana au kubadilishana taarifa ndani ya taasisi, na kati ya taasisi na taasisi, urudufu wa mifumo miongoni mwa Taasisi za Serikali yenye viwango na gharama tofauti zisizo na uhalisia, huduma za Serikali Mtandao kutowafikia wananchi wote hasa wa vijijini na kuongezeka kwa matishio ya usalama wa taarifa katika mifumo na Miundombinu ya TEHAMA.

Kutokana na changamoto hiyo, Mhe. Jenista, ameiagiza Mamlaka ya Serikali mtandao kuhakikisha mifumo inayofanana inaunganishwa na ile isiyofanana inaboreshwa na kubadilishana taarifa ifikapo tarehe 30 Septemba, 2022.

Aidha, Mhe. Jenista amewataka wataalam hao kujenga mifumo ya utoaji huduma ambayo ni rafiki kwa watumiaji ili kila mwananchi aweze kunufaika na huduma zinazotolewa na Serikali kwani mifumo hiyo inajengwa kwa ajili ya kuwahudumia wao.

Mhe. Jenista amesema, Serikali imeamua Utumishi wa Umma kuwa wa kidijitali katika maeneo yote ya utendaji kazi hivyo, ushirikiano mkubwa unahitajika kutoka kwa Wataalam wa TEHAMA kwani wao ndio wanaoweza kusaidia lengo hilo kufikiwa.

“Kwa niaba ya Serikali niwaombe Wataalam wa TEHAMA mvae uzalendo, muwajibike kwa hiari bila kushurutishwa, ili muweze kutuvusha na kuwa na Serikali ya kidijitali kwa utoaji wa huduma bora kwa umma.” Mhe. Jenista amesisitiza.

Akizunguzia umuhimu wa TEHAMA Serikalini, Mhe. Jenista amesema Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2025, Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2021/22 - 2025/26) na Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2020 kwa pamoja zinatambua nafasi ya TEHAMA katika kufikia malengo ya Taifa na hivyo kusisitiza haja ya ongezeko la matumizi yake katika utendaji wa shughuli za Serikali na utoaji huduma kwa Umma.

Mhe. Jenista amewataka wataalam hao wa TEHAMA kujifunza kwa nchi za Malaysia, Singapore na Korea ya Kusini walivyopiga hatua katika maendeleo ya TEHAMA na kuongeza kuwa kabla yao, Tanzania ilipiga hatua katika suala la TEAHAMA lakini leo wao wako mbele yetu.

Mhe. Jenista ameipongeza Mamlaka ya Serikali Mtandao kwa kuandaa kikao kazi hicho muhimu ambacho pamoja na mambo mengine kinawakumbusha Wataalam wa TEHAMA umuhimu wa uzingatiaji wa Sheria ya Serikali Mtandao Na. 10 ya Mwaka 2019 na kuelekeza kufanyika kwa kikao kazi kama hicho kila mwaka ambacho pia kitawatambua wanaofanya vizuri katika kuzingatia Sheria ya Serikali Mtandao na wanaosizingatia sheria watatajwa lengo likiwa ni kutaka wote wazingatie sheria.

Kikao kazi hicho ambacho ni cha pili kufanyika tangu kutungwa kwa Sheria ya Serikali Mtandao Na. 10 ya Mwaka 2019, kimeshirikisha Wakuu wa Idara na Vitengo vya TEHAMA 486 kutoka kwenye Wizara, Taasisi za Umma, Idara zinazojitegemea, Mamlaka, Wakala,  Mikoa, Majiji, Manispaa na Halmashauri za Wilaya.

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akifungua kikao kazi cha siku mbili cha Wakuu wa Idara na Vitengo vya TEHAMA Serikalini jijini Dodoma


Sehemu ya Wakuu wa Idara na Vitengo vya TEHAMA Serikalini wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama (hayupo pichani) alipokuwa akifungua kikao kazi cha siku mbili cha Wakuu wa Idara na Vitengo vya TEHAMA Serikalini jijini Dodoma


Kaimu Katibu Mkuu-UTUMISHI, Bw. Hassan Kitenge akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kufungua kikao kazi cha siku mbili cha Wakuu wa Idara na Vitengo vya TEHAMA Serikalini jijini Dodoma



Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA), Mhandisi Benedict Ndomba akielezea lengo la kikao kazi cha siku mbili cha Wakuu wa Idara na Vitengo vya TEHAMA Serikalini kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kabla ya Mhe. Jenista kufungua kikao kazi hicho jijini Dodoma.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akiwa katika kikao kazi cha siku mbili cha Wakuu wa Idara na Vitengo vya TEHAMA Serikalini jijini Dodoma. Wa kwanza kulia kwake ni Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Bw. Hassan Kitenge na wa kwanza kushoto kwake ni Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) Mhandisi Benedict Ndomba. 


Mkurugenzi wa TEHAMA, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Bw. Priscus Kiwango akitoa neno la shukrani kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama mara baada ya Waziri Jenista kufungua kikao kazi cha siku mbili cha Wakuu wa Idara na Vitengo vya TEHAMA Serikalini jijini Dodoma.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Wakuu wa Idara na Vitengo vya TEHAMA Serikalini mara baada ya kufungua kikao kazi cha Wakuu wa Idara na Vitengo vya TEHAMA Serikalini jijini Dodoma. Wa kwanza kulia kwake ni Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Bw. Hassan Kitenge na wa kwanza kushoto kwake ni Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) Mhandisi Benedict Ndomba. 


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akiwasili kwenye ukumbi wa Chuo cha Sayansi ya Kompyuta, habari na mawasiliano Chuo Kikuuu Dodoma   kufungua kikao kazi cha Wakuu wa Idara na Vitengo vya TEHAMA Serikalini jijini Dodoma. Wa kwanza kulia kwake ni Kaimu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Bw. Hassan Kitenge na wa kwanza kushoto kwake ni Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) Mhandisi Benedict Ndomba. 



No comments:

Post a Comment