Monday, December 14, 2020

MKUCHIKA AWATAKA WATUMISHI WA OFISI YAKE KUANDAA MPANGO MADHUBUTI KUTEKELEZA ILANI YA CCM

 

Na. James K. Mwanamyoto-Dodoma

Tarehe 14 Disemba, 2020

Watumishi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora pamoja taasisi zake wametakiwa kuitekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya Mwaka 2020-2025 katika eneo la Utumishi wa Umma na Utawala Bora ili wananchi wanufaike na huduma zitolewazo na ofisi hiyo.

Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Kapt (Mst) George Mkuchika mara baada ya kupokelewa na Watumishi wa Ofisi yake jijini Dodoma ikiwa ni siku chache tangu ateuliwe na kuapishwa rasmi na Mhe. Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.

Mhe. Mkuchika amesema Ofisi yake na taasisi zote zilizo chini ya Ofisi yake ambazo ni TAKUKURU, MKURABITA, TASAF, Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa, Chuo cha Utumishi wa Umma, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma na Wakala ya Ndege za Serikali zinatakiwa zikae na kuandaa mpango madhubuti wa miaka mitano ili kutekeleza ahadi za masuala ya kiutumishi na Utawala Bora zilizoainishwa katika Ilani ya CCM.

“Watumishi wa Umma tunapaswa kuitumikia Serikali iliyoshinda uchaguzi ambayo ni ya CCM na CCM inayo Ilani iliyoiweka Serikali madarakani, hivyo hatuna budi kuitekeleza,” Mhe. Mkuchika amesisitiza.

Aidha, Mhe. Mkuchika ametoa rai kwa watumishi kuendelea kutoa ushirikiano katika kipindi hiki alichokabidhiwa tena jukumu la kusimamia utekelezaji wa majukumu ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora pamoja na taasisi zilizo chini ya ofisi hiyo.

Kwa upande wake, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi amemuahidi Mhe. Mkuchika na Watumishi ushirikiano katika kuwatumikia Watanzania kama ambayo Mhe. Rais Magufuli anatarajia.

Sanjali na hilo, Mhe. Ndejembi ameomba ushirikiano kutoka kwa Watumishi na Menejimenti kwa ujumla ili kuhakikisha huduma bora inatolewa kwa wananchi.

Mhe. Mkuchika na Mhe. Ndejembi wamepokelewa leo na Watumishi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora tayari kwa kuanza kazi rasmi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Kapt (Mst) George akizungumza na watumishi wa ofisi yake mara baada ya kuripoti rasmi. Kushoto kwake ni Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi. Na kulia kwake ni Katibu Mkuu - UTUMISHI, Dkt. Laurean Ndumbaro. 

Baadhi ya Watumishi wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Kapt (Mst) George mara baada ya kiongozi huyo kuripoti rasmi ofisini kwake jijini Dodoma. 

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akizungumza na watumishi wa ofisi yake (hawapo pichani) mara baada ya kuripoti rasmi na kuanza kazi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Kapt (Mst) George akisalimiana na baadhi ya Wakurugenzi wa ofisi yake mara baada ya kuripoti rasmi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Kapt (Mst) George akiwa katika picha ya pamoja na Wakurugenzi wa Ofisi yake Jijini Dodoma mara baada ya kuripoti rasmi. Kulia kwake ni Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi na Katibu Mkuu-UTUMISHI, Dkt. Laurean Ndumbaro na Kulia kwake ni Naibu Katibu Mkuu, Dkt. Francis Michael.



Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Kapt (Mst) George Mkuchika akimkabidhi nyaraka za kiutumishi Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi mara baada ya Viongozi hao kuripoti rasmi ofisini na kuanza kazi.












Friday, December 11, 2020

SALAMU ZA PONGEZI


 

SERIKALI INAZINGATIA HAKI ZA BINADAMU NA KUPAMBANA NA RUSHWA KATIKA UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU YAKE

 Na. James K. Mwanamyoto-Dodoma

Tarehe 11 Desemba, 2020

Serikali inazingatia haki za binadamu na kupambana na rushwa katika utekelezaji wa majukumu yake ili kuhakikisha taasisi za umma nchini zinatoa huduma bora kwa wananchi na bila upendeleo.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Kapt (Mst) Mhe. George Mkuchika (Mb) alipokuwa akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Peter Pinda kwenye Kongamano la Maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za Binadamu lililofanyika tarehe 10 Desemba, 2020 jijini Dodoma.

Mhe. Mkuchika amesema, suala la haki za binadamu na mapambano dhidi ya rushwa ni mtambuka, ndio maana taasisi zote zinazojishughulisha na utawala bora zimekutana na wadau wa sekta ya umma na binafsi katika Kongamano la Maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za Binadamu mwaka huu ili kujadili na kutoa mapendekezo yatakayoboresha mapambano dhidi ya rushwa na uzingatiaji wa haki za binadamu.

Mhe Mkuchika ameeleza kuwa, uzinduzi wa Maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za binadamu kwa mwaka huu ulifanyika kwa kuzungumza na Waandishi wa Habari ili washiriki kutoa elimu kwa umma dhidi ya rushwa na uzingatiaji wa haki za binadamu.

Taasisi zilizoshiriki kuandaa maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za Binadamu ni Ofisi ya Rais Ikulu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Wizara ya Katiba na Sheria,Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi wa Hesabu za Serikali, Mamlaka ya Kudhibiti Ununuzi wa Umma, Tume ya Utumishi wa Umma na Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora.

Kaulimbiu ya maadhimisho ya mwaka huu ni “Uzingatiaji wa Ahadi ya Uadilifu kwa Viongozi na Watumishi kwa Ustawi wa Utawala Bora na Haki za Binadamu nchini”.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Kapt (Mst) Mhe. George Mkuchika (Mb) akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Peter Pinda kufungua Kongamano la Maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za Binadamu lililofanyika tarehe 10 Desemba, 2020 jijini Dodoma.

Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Peter Pinda akizungumza na washiriki wa  Kongamano la Maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za Binadamu lililofanyika tarehe 10 Desemba, 2020 jijini Dodoma.


Baadhi ya washiriki wa Kongamano la Maadhimisho ya Siku ya Maadili na Haki za Binadamu wakimsikiliza Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Mizengo Peter Pinda kabla ya kufungua kongamano hilo.