Thursday, February 10, 2022

MHE. NDEJEMBI KUONGOZA KIKAO CHA UTATUZI WA MIUNDOMBINU ILIYOHARIBIKA KWENYE MRADI WA NYUMBA ZA WATUMISHI MOROGORO

Na. Mary L. Mwakapenda-Morogoro

Tarehe 10 Februari, 2022

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi ameazimia kufanya kikao na Watumishi Housing, TARURA, MORUWASA, TANESCO na wakazi wa Kata ya Mkundi mkoani Morogoro wanaoishi kwenye nyumba za Mradi wa Watumishi Housing ili kutatua changamoto ya miundombinu iliyoharibiwa na mvua kwenye nyumba hizo za gharama nafuu zilizojengwa kwa ajili kuwapangisha na kuwauzia Watumishi wa Umma na wanachama wa Mifuko ya Hifadhi za Jamii.

Mhe. Ndejembi amefanya uamuzi huo akiwa mkoani Morogoro baada ya kukagua Mradi wa nyumba zilizojengwa na Watumishi Housing katika Kata ya Mkundi mjini Morogoro na kukuta miundombinu ya eneo hilo imeharibika kutokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha mkoani humo.

Naibu Waziri Ndejembi amesema atafanya kikao hicho siku ya Jumamosi ya tarehe 19 Februari, 2022 ili kuwawezesha wakazi wengi wa eneo hilo ambao ni Watumishi wa Umma kushiriki kikamilifu.

Akiwa katika ukaguzi wa miundombinu ya eneo hilo, Mhe. Ndejembi amejionea madhara ya mvua zinazoendelea kunyesha katika eneo hilo na kusababisha nyumba hizo kuingiliwa na maji ya mvua ambayo imebomoa ukuta na mfereji wa kuzuia maji kuingia katika makazi hayo na hatimaye kuharibu nyumba mbili pamoja na vitu vya ndani vya nyumba hizo.

Mara baada ya kumaliza ukaguzi wa maeneo yaliyoathirika na mvua zinazoendelea kunyesha, Mhe. Ndejembi alikagua pia sehemu ambapo mkusanyiko wa maji unaanzia na kuona kuna umuhimu wa kuzishirikisha taasisi nyingine na wananchi ili kuweza kulimaliza kabisa tatizo hilo.

Ili kukabiliana na athari zilizojitokeza kabla ya kufanyika kwa kikao rasmi cha utatuzi wa tatizo la uharibifu wa miundombinu ya eneo hilo, Mhe. Ndejembi amemuagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Watumishi Housing, Dkt. Fred Msemwa kuhakikisha anachukua hatua za haraka za kuimarisha miundombinu ya ndani ya makazi hayo ambayo imeharibika, ikiwa ni pamoja na kuendelea kushirikiana na taasisi nyingine katika kutafuta suluhu ya kudumu kabla ya kikao chake alichoelekeza kufanyika Februari 19, 2022.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Watumishi Housing Dkt. Fred Msemwa ameahidi kuyafanyia kazi maagizo ya Mhe. Ndejembi ili kuwawezesha wakazi wa eneo hilo kuwa na miundombinu imara itakayohimiri changamoto ya mvua nyingi zinazoendelea kunyesha katika eneo hilo.

Chanzo kikubwa cha kuharibika kwa miundombinu kwenye kata hiyo ya Mkundi mjini Morogoro ni barabara zinazozunguka eneo hilo kukosa mitaro ya maji hali inayopelekea mkondo wa maji kuelekea katika eneo la makazi ya watu.



Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akitoa maelekezo baada ya kukagua na kuona changamoto ya miundombinu ya eneo la Mradi wa nyumba zilizojengwa na Watumishi Housing katika Kata ya Mkundi mjini Morogoro.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akiangalia uharibifu wa miundombinu ya barabara uliosababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha kwenye eneo la Mradi wa nyumba zilizojengwa na Watumishi Housing katika Kata ya Mkundi mjini Morogoro.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akielekea kukagua miundombinu ya eneo la Mradi wa nyumba zilizojengwa na Watumishi Housing katika Kata ya Mkundi mjini Morogoro.



Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akiangalia uharibifu wa miundombinu uliosababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha kwenye Mradi wa nyumba zilizojengwa na Watumishi Housing katika Kata ya Mkundi mjini Morogoro.

 

No comments:

Post a Comment