Saturday, January 30, 2021

SHUGHULIKIENI CHANGAMOTO ZA WATUMISHI ILI KUWAONGEZEA ARI YA KUFANYA KAZI- DKT. NDUMBARO


Mary Mwakapenda-Dodoma

Tarehe 30 Januari, 2021

Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro amewataka Wanasheria na Maafisa Utumishi katika taasisi za umma nchini kuwathamini Watumishi wa Umma, kuwaheshimu na kuzifanyia kazi changamoto zinazowakabili lengo likiwa ni kupunguza malalamiko na kuwaongezea ari ya kufanya kazi na hatimaye kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Dkt. Ndumbaro ametoa maelekezo hayo Jijini Dodoma wakati akifunga kikao kazi cha siku mbili kwa Wanasheria na Maafisa Utumishi kutoka Halmashauri 31 nchini kilicholenga kutambua changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wa Sheria ya Utumishi Wa Umma Sura 298 ili kuzitafutia ufumbuzi utakaoboresha utoaji wa huduma kwa Watumishi wa Umma na wananchi.

Dkt. Ndumbaro amesema, Wanasheria na Maafisa Utumishi ni wadau wakubwa wanaoshughulika na masuala ya watumishi, hivyo ni muhimu sana kuwathamini, kuwaheshimu na kutambua changamoto wanazokabiliana nazo na kuzitatua kwani wakishindwa kufanya hivyo watasababisha malalamiko mengi yatakayoweza kushusha morali ya kufanya kazi kwa watumishi hao.

Dkt. Ndumbaro ameeleza kuwa, ili Maafisa hao waweze kushughulikia matatizo ya watumishi kwa ufasaha hawana budi kujiweka kwenye nafasi ya watumishi waliofikwa na matatizo kwani kwa kufanya hivyo watakuwa na moyo wa ya kuwasaidia kutatua na kupunguza malalamiko.

Aidha, Dkt. Ndumbaro amewasisitiza washiriki wa kikao kazi hicho kuzingatia uadilifu, uwajibikaji, utendaji kazi mzuri na uwepo wa sifa stahiki kwa Watumishi wa Umma kama ambavyo Mhe. Rais amekuwa akisisitiza mara kwa mara.

Amefafanua kuwa, Wanasheria na Maafisa Utumishi wanapaswa kuwa wasimamizi wa nidhamu kwa watumishi kwani kama uadilifu hauko kwenye taasisi basi wao ndio watakuwa watu wa kwanza kulaumiwa kwa kutokuwajibika ipasavyo.

Ametolea mfano wa suala la uadilifu katika zoezi la kuwabaini watumishi waliokuwa na vyeti vya kughushi na kusema kuwa kuna baadhi ya Maafisa Utumishi wameshiriki kuwasaidia watumishi waliokutwa na vyeti vya kughushi ili wabakie katika Utumishi wa Umma.

“Katika suala la vyeti vya kughushi kuna baadhi ya Maafisa Utumishi wameshiriki kuwasaidia watumishi waliokutwa na vyeti vya kughushi kwa kunyofoa vyeti kwenye mafaili yao ili wabaki kwenye utumishi wa umma. Sisi ndio tunaosimamia nidhamu, tuwe mfano wa kuigwa katika kuonyesha uadilifu kwa kufanya kazi zetu kwa kuzingatia Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo.” Dkt. Ndumbaro amesisitiza.

Akizungumzia suala la uwajibikaji, Dkt. Ndumbaro amesema Watumishi walio katika ngazi za juu wanawajibika kwa Serikali iliyopo madarakani, kwa watumishi wenzao na kwa wananchi kwa kuwahudumia vizuri bila upendeleo wala chuki ili kujenga taswira nzuri katika jamii.

Pia, Dkt. Ndumbaro amewataka Maafisa Utumishi kuwakumbusha watumishi kufuatilia mara kwa mara taarifa za uwasilishaji wa michango katika Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ili wanapostaafu wasipate usumbufu.

“Suala la mafao ya watumishi, wengi wanajisahau au hawajui mpaka wakati wa kustaafu ndio wanagundua kuwa kuna baadhi ya michango haikuwasilishwa, hivyo ni vema kuwakumbusha watumishi kufuatilia michango yao kabla ya kustaafu ili kama kuna michango haijawasilishwa ifanyiwe kazi mapema.” Dkt. Ndumbaro ameongeza.

Kikao kazi hicho kiliandaliwa na Kitengo cha Huduma za Sheria cha Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ambapo mada zifuatazo ziliwasilishwa; Sheria ya Utumishi wa Umma Sura 298, Kanuni za Utumishi wa umma, Taratibu za Ushughulikiaji wa Masuala ya Kinidhamu, Ushughulikiaji wa Ajali kazini kwa ajali zilizotokea kabla ya Juni 2016 na Ushughulikiaji wa Mafao kwa Watumishi wa Umma.

Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Dkt. Laurean Ndumbaro akizungumza na Wanasheria na Maafisa Utumishi kutoka Halmashauri 31 nchini (hawapo pichani) wakati akifunga kikao kazi cha siku mbili Jijini Dodoma kilicholenga kutambua changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wa Sheria ya Utumishi Wa Umma Sura 298 ili kuzitafutia ufumbuzi na kuboresha utoaji wa huduma kwa Watumishi wa Umma. Kushoto kwake ni Mkurugenzi wa Usimamizi wa Rasilimaliwatu, ACP Ibrahim Mahumi na kulia kwake ni Mkurugenzi wa Huduma za Sheria, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Hilda Kabissa


Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Dkt. Laurean Ndumbaro akisisitiza jambo kwa Wanasheria na Maafisa Utumishi kutoka Halmashauri 31 nchini (hawapo pichani) wakati akifunga kikao kazi cha siku mbili Jijini Dodoma kilicholenga kutambua changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wa Sheria ya Utumishi Wa Umma Sura 298 ili kuzitafutia ufumbuzi na kuboresha utoaji wa huduma kwa Watumishi wa Umma. 


Baadhi ya washiriki wakimsikiliza Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-UTUMISHI, Dkt. Laurean Ndumbaro wakati akifunga kikao kazi cha siku mbili kwa Wanasheria na Maafisa Utumishi kutoka Halmashauri 31 nchini Jijini Dodoma kilicholenga kutambua changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wa Sheria ya Utumishi Wa Umma Sura 298 ili kuzitafutia ufumbuzi na kuboresha utoaji wa huduma kwa Watumishi wa Umma.


Mmoja wa washiriki Bw. Baraka Kilagu kutoka Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, akichangia mada wakati wa kuhitimisha kikao kazi cha siku mbili cha Wanasheria na Maafisa Utumishi kutoka Halmashauri 31 nchini kilichofanyika Jijini Dodoma kwa lengo la kutambua changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wa Sheria ya Utumishi Wa Umma Sura 298 ili kuzitafutia ufumbuzi na kuboresha utoaji wa huduma kwa Watumishi wa Umma.

 

 

No comments:

Post a Comment