Thursday, June 22, 2017

“NIDHAMU IWE NAMBA MOJA KATIKA UTUMISHI WA UMMA” DKT NDUMBARO



Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro akisisitiza jambo kwa Watendaji na watumishi wa Mkoa wa Mwanza wakati wa kikao kazi na watumishi hao ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2017.


Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro, akifuatilia taarifa ya utekelezaji ya Mkoa wa Mwanza iliyokuwa ikiwasilishwa na Katibu Tawala Msaidizi Rasilimaliwatu wa Mkoa wa Mwanza, Bw. Projestus Rubanzibwa (hayupo pichani) alipokutana na Watendaji wa Sekretarieti ya mkoa wa Mwanza ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2017. 

Sehemu ya Watendaji na Watumishi wa Mkoa wa Mwanza wakimsikiliza Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza nao wakati wa kikao kazi na watumishi hao ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2017. 

Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais - Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro ameelekeza suala la nidhamu katika Utumishi wa Umma ni namba moja na lipewe uzito unaostahili ili kujenga Utumishi wa Umma wenye uadilifu.
Dkt. Ndumbaro aliyasema hayo wakati akizungumza na Watendaji na Watumishi wa Umma mikoa ya Singida, Shinyanga na Mwanza ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma 2017.
Alisema Watumishi wanaokiuka maadili ya Utumishi wa Umma wasionewe aibu bali wachukuliwe hatua zinazostahili haraka iwezekanavyo kwa mujibu wa Sheria, Kanuni, Taratibu na miongozo iliyopo katika Utumishi wa Umma.
“Ni lazima hatua za kinidhamu zichukuliwe mapema kwa mtumishi asiye na maadili kwani bila kufanya hivyo tutajenga Utumishi wa Umma usio na maadili kwa siku zijazo,” Dkt. Ndumbaro alisema na kuongeza kuwa mtumishi wa Umma anapofanya kosa ni lazima lifanyiwe kazi na mwajiri wake katika kituo cha kazi alichopo badala ya kumhamishia katika kituo kingine.
Aidha, Dkt, Ndumbaro amewataka waajiri kuwapongeza watumishi wanaofanya vizuri katika utumishi wao ili kujenga nidhamu ya utendaji kazi.
“Tusifikirie kutoa adhabu tu kwa Watumishi wa Umma wasio na maadili bali tunatakiwa kutambua mchango na ubunifu wa wale wanaofanya vizuri kwa kuwapongeza. Tuelewe kuwa kuwapongeza watumishi wa umma sio lazima tuwape fedha, bali kuwatambua kwa kuwapa vyeti vya utendaji mzuri na kuwaandikia barua za pongezi kwa kutambua juhudi zao katika kuwahudumia wateja hivyo kuwapa morali ya kuendelea kufanya kazi kwa kuzingatia weledi na bidii zaidi, aliongeza.
Kwa upande mwingine Dkt. Ndumbaro amewataka Waajiri kupitia taarifa za Watumishi mara kwa mara ili kuweka kumbukumbu ya taarifa sahihi na safi katika Mfumo wa Taarifa za Kiutumishi na Mishahara (HCIMS).
“Waajiri katika Utumishi wa Umma ni jukumu lenu kuwakumbusha na kushirikiana na Maafisa Utumishi kupitia taarifa za watumishi mara kwa mara na kuwaondoa katika mfumo wa HCIMS Watumishi wa Umma ambao hawastahili kuwepo ili kuepukana na suala la watumishi hewa na taarifa zisizo sahihi (chafu).” Dkt. Ndumbaro alisisitiza.
Wiki ya Utumishi wa Umma huadhimishwa kila mwaka na kufikia kilele chake tarehe 23 Juni ambapo mwaka huu inaadhimishwa kwa viongozi mbalimbali katika Utumishi wa Umma kukutana ili kufanyia kazi masuala ya Menejimenti ya Rasilimaliwatu katika Utumishi wa Umma, pamoja na wadau ili kusikiliza changamoto mbalimbali zinazowakabili katika huduma wanazopokea, ndani na nje ya utumishi wa umma ili kuleta mabadiliko zaidi katika Utoaji huduma na kufikia malengo ya nchi.







No comments:

Post a Comment