Wednesday, July 7, 2021

ZIARA YA MARAIS NA MAWAZIRI WAKUU WASTAAFU KUTEMBELEA MIRADI YA KIMKAKATI ILIANDALIWA NA MHE. RAIS ILI KUWAWEZESHA WASTAAFU HAO KUJIONEA MCHANGO WALIOUTOA WAKATI WA UONGOZI WAO - Mchengerwa


Na. James K. Mwanamyoto-Dar es Salaam

Tarehe 07 Julai, 2021

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema ziara ya siku mbili ya Marais na Mawaziri Wakuu Wastaafu ya kutembelea Mradi wa Kufua Umeme kwa Nguvu za Maji wa Julius Nyerere na wa Ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR), iliandaliwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ili kutoa fursa kwa viongozi hao wastaafu wa kitaifa kuona maendeleo ya mchango walioutoa wakati wa uongozi wao ikiwa ni pamoja kuwapa fursa ya kushuhudia hatua ambayo Serikali imefikia katika ujenzi wa miradi hiyo mikubwa ya kimkakati.

Mhe. Mchengerwa amesema hayo jijini Dar es Salaam mara baada ya viongozi hao wastaafu wa kitaifa kuhitimisha ziara yao ya kujionea maendeleo ya ujenzi wa miradi hiyo mikubwa ya kimkakati inayotekelezwa na Serikali.

Mhe. Mchengerwa amempongeza Rais wa Awamu ya Sita, Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuwaandalia ziara hiyo mahususi Waheshimiwa Marais na Mawaziri Wakuu wastaafu ambao wakati wa uongozi wao walitoa mchango mkubwa katika kujenga misingi imara ya utekelezaji wa miradi hiyo ya kimkakati yenye tija katika uchumi wa taifa.

Mhe. Mchengerwa amesema, Marais na Mawaziri Wakuu wastaafu wamefurahi kuona mawazo na mapendekezo waliyoyatoa kuhusu utekelezaji wa miradi hiyo yamefanyiwa kazi kikamilifu na Serikali ya Awamu ya Tano na kuendelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozo makini wa Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan.

Waziri Mchengerwa amefafanua kuwa, Serikali ya Awamu ya Sita inaendeleza miradi ya kimkakati iliyokusudiwa kutekelezwa na Marais Wastaafu na kuongeza kuwa, mipango ya utekelezaji wa miradi hiyo ya kimkakati ilianza muda mrefu wakati wa utawala wa Waheshimiwa Marais hao wastaafu.

“Mipango yote ya kuwa na miradi ya kimkakati ilianza wakati wa uongozi wa Baba wa Taifa Mwalimu Julius K. Nyerere na kuendelezwa na Marais wote wastaafu na hivi sasa inaendelea kutekelezwa na Rais Samia Suluhu Hassani,” Mhe. Mchengerwa amesisitiza. 

Akijibu swali la Mwandishi wa Habari kuhusu mchango wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora katika usimamizi wa utekelezaji wa miradi ya kimkakati, Mhe. Mchengerwa amesema kuwa ofisi yake inahusika katika usimamizi wa miradi hiyo kwani wanaosimamia miradi hiyo ni Watumishi wa Umma ambao wameajiriwa na Serikali ili kuwatumikia watanzania.

Sanjari na hilo, Mhe. Mchengerwa amesema kuwa, Mhe. Rais ameelekeza miradi yote ya kimkakati ikamilike kwa wakati hivyo akiwa ni msaidizi wa Mhe. Rais katika kutekeleza jukumu la usimamizi wa masuala ya kiutumishi na utawala bora, ofisi yake inawajibika kusimamia utekelezaji wa miradi hiyo ya kimkakati  ili wananchi ambao ndio walengwa wakuu wanufaike na miradi hiyo kiuchumi.

Kutokana na maelekezo hayo ya Mhe. Rais, Mhe. Mchengerwa amesema hakutakuwa na nyongeza ya muda ili kukamilisha miradi hiyo ya kimkakati, hivyo amewataka watendaji katika wizara zinazosimamia ujenzi wa Mradi wa Kufua Umeme kwa Nguvu za Maji wa Julius Nyerere na wa Ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) kuhakikisha wanatekeleza wajibu wao kikamilifu ili kuwezesha miradi hiyo ikamilike kwa wakati.

Ziara hiyo ya Viongozi wastaafu wa Kitaifa iliyolenga kuwawezesha kuona maendeleo ya ujenzi wa miradi ya kitaifa ya kimkakati ilihudhuriwa na Rais Mstaafu Mhe. Ali Hassan Mwinyi, Rais Mstaafu Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete na Mawaziri wakuu wastaafu ambao ni Mhe. Cleopa Msuya, Mhe. John Malecela na Mhe. Mizengo Pinda.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa akizungumza na Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam, mara baada ya Waheshimiwa Marais na Mawaziri Wakuu wastaafu kuhitimisha ziara yao ya siku mbili kujionea maendeleo ya ujenzi wa miradi mikubwa ya kimkakati inayotekelezwa na Serikali.


Marais wastaafu Mhe. Ali Hassan Mwinyi na Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete wakiwa na Mawaziri Wakuu wastaafu Mhe. John Malecela na Mhe. Peter Pinda wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi wengine mbele ya andaki ambalo reli ya kisasa (SGR) imepita eneo la Kilosa mkoani Morogoro.

 

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete akizungumza na Waandishi wa Habari eneo la Kilosa Morogoro wakati wa ziara ya viongozi wakuu wastaafu wa kitaifa ya kujionea maendeleo ya Reli ya Kisasa (SGR) inayojengwa na Serikali.



Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete akisaini kitabu cha wageni akiwa safarini kurejea jijini Dar es Salaam ndani ya treni inayotoa huduma ya usafiri kwa kutumia Reli ya Kisasa (SGR) inayojengwa na Serikali.

Watendaji wa Serikali waliombatana na Marais wastaafu Mhe. Ali Hassan Mwinyi na Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete na Mawaziri Wakuu wastaafu Mhe. John Malecela na Mhe. Peter Pinda wakiingia na viongozi hao kwenye moja ya andaki ambalo reli ya kisasa (SGR) imepita eneo la Kilosa mkoani Morogoro.



Watendaji wa Serikali waliombatana na Marais wastaafu Mhe. Ali Hassan Mwinyi na Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete na Mawaziri Wakuu wastaafu Mhe. John Malecela na Mhe. Peter Pinda wakiwa ndani ya andaki ambalo reli ya kisasa (SGR) imepita eneo la Kilosa mkoani Morogoro.


 

No comments:

Post a Comment