Wednesday, October 1, 2014

UTUMISHI YAANZA MASHINDANO YA SHIMIWI 2014 KWA KISHINDO

Kapteni wa timu ya mpira wa Pete ya Utumishi Elizabeth Fusi (c) mwenye mpira akikatiza kati ya wachezaji wa timu ya Wizara ya Kilimo wakati wa mechi ya mashindano ya SHIMIWI yanayoendelea katika kiwanja cha Jamhuri mjini Morogoro.

Mchezaji wa timu ya mpira wa Pete ya Utumishi Fatuma Machenga (GS) akiwa hewani na mpira  huku mpinzani wake wa timu ya Wizara ya Kilimo (GK) akishangaa wakati wa mpambano wa SHIMIWI uliofanyika katika kiwanja cha Jamhuri mjini Morogoro.

Vuta nikuvute ya kudaka mpira kati ya Wachezaji wa timu ya Mpira wa Pete ya Ofisi ya Rais-Utumishi na Wizara ya Kilimo katika mashindano ya SHIMIWI yanayoendelea katika kiwanja cha Jamhuri mjini Morogoro.
Timu ya netiboli ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma imeanza mashindano ya SHIMIWI 2014 kwa kuifunga timu ya Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika magori 57 dhidi ya 18.
Ikicheza kwa kujiamini ndani ya Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro iliwachukua takribani sekunde 7 kufunga goli la kwanza kupitia kwa mchezaji Monica Aloyce (GS) lililoamsha shangwe na ndelemo kwa wapenzi wa mchezo huo.
Ustadi wa Monica Aloyce (GS) aliyefunga magori 16 kwa kushirikiana na Anna Msulwa (GA) aliyefunga magori  9 uliisaidia Utumishi kupata magori 25 dhidi ya matano (5) ya kilimo katika kipindi cha kwanza cha mchezo huo.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi hali iliyopelekea kocha wa Utumishi kumpumzisha mchezaji Monica Aloyce (GS) na nafasi yake kuchukuliwa na Fatuma Machenga (GS) aliyebadilisha hali ya mchezo kwa kufunga magori 27.
Akizungumza mara baada ya mchezo kumalizika,kocha wa Wizara ya kilimo Bi. Rabia Mohamed alikiri kuwa timu yake ilikuwa na mapungufu kwenye safu ya Ulinzi hali iliyopelekea timu yake kupoteza mchezo.
“Timu yangu haikucheza vizuri kwenye safu ya ulinzi hivyo nitafanya marekebisho ya mapungufu yaliyojitokeza ili tupate ushindi katika mechi inayofuata” alisema Bi. Rabia.

Naye,kocha wa Utumishi Bw. Methew Kambona aliwapongeza wachezaji wake kwa kucheza vizuri kwa kiwango kinachoridhisha,aidha Bw. Kambona alisema kuwa timu yake imejipanga vizuri na kuhaidi kuibuka kinara katika mashindano hayo.

No comments:

Post a Comment