Tuesday, October 7, 2014

UTUMISHI YATINGA ROBO FAINALI YA SHIMIWI KWA KISHINDO

Kikosi cha timu ya mpira wa Pete ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma katika picha ya pamoja kabla ya kuisambaratisha timu ya Mahakama na kutinga robo fainali ya michezo ya SHIMIWI katika Uwanja Jamhuri mjini Morogoro.

Mchezaji wa Ofisi ya Rais, Utumishi Anna Msulwa (GA) akijiandaa kufunga wakati Utumishi ilipoipeleka mchamchaka timu ya Mahakama kwa kuibugiza Pete 56 dhidi ya 14 ya Mahakama katika mchezo uliochezwa katika Uwanja wa Jamhuri, Morogoro.

Raha ya mchezo ushindi, ndivyo wanavyoonekana baadhi ya washabiki wa timu ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi  wa Umma wakisema wakati timu yao ikicheza na Mahakama katika Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.

Wachezaji wa timu ya Utumishi wakiwadhibiti wachezaji wa Mahakama wasifunge katika goli lao katika mchezo wa SHIMIWI uliochezwa katika uwanja wa Jamhuri.
Timu ya Mpira wa Pete ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma imeifungashia virago katika mashindano ya SHIMIWI  timu ya Mahakama kwa ushindi wa Pete 56 dhidi ya 14.
Utumishi iliibuka na ushindi huo mkubwa katika mechi za hatua ya kumi na sita bora ambapo mshindi husonga mbele.
Kwa ushindi huo, Utumishi imefanikiwa kuingia robo fainali katika mchezo utakaochezwa kesho kwa kupambana na jirani zake Hazina.
Mchezo ulioiwezesha Utumishi kutinga robo fainali uliongezwa makali na wachezaji wake Fatuma Machenga (GS) aliyewashushia Mahakama mvua ya Pete 26, akifuatiwa na Anna Msulwa (GA) aliyefunga Pete 4 hivyo kuhitimisha nusu ya kwanza kwa idadi ya Pete 30 dhidi ya 7 za Mahakama.
Kipindi cha pili mambo yaliiendea  mrama Mahakama kwa kuzidiwa kila hali ambapo Utumishi ilizidi kuibugiza magoli. Ushirikiano wa Wachezaji Fatuma Machenga (GS) na Anna Msulwa (GA) uliitupa Mahakama nje ya mashindano kwani hadi kipenga cha mwisho wachezaji hao walishaandika ushindi mnono kila mmoja akifunga Pete 47 na 9, hivyo Utumishi kuibuka mshindi kwa jumla ya Pete 56 dhidi ya 14 za Mahakama.
Mara baada ya filimbo ya mwisho, mchezaji wa Mahakama Veronica Ndasi (GK) alikubali kuwa timu yao ilizidiwa kimchezo “ wapinzani wetu wako vizuri zaidi kimchezo na wametutoa”.
Ndasi alisema Utumishi walijiandaa vizuri hata hivyo nao Mahakama walitoa upinzani kimchezo hivyo mashabiki wasikate tamaa.
Kapteni wa Utumishi Elizabeth Fusi (C) aliwapongeza wachezaji wenzake na kuahidi kuendeleza kipigo hicho hicho kwa timu ya Hazina katika mchezo wa robo fainali. 
Mashindano ya 38 ya SHIMIWI yanayowahusisha watumishi wa Serikali katika michezo tofauti tofauti yanafanyika mkoani Morogoro katika viwanja mbalimbali.

No comments:

Post a Comment