Sunday, August 9, 2020

TAKUKURU HAIKO TAYARI KUCHAFULIWA NA MTUMISHI WAKE ANAYEJIHUSISHA NA RUSHWA NA UBADHIRIFU

Na. James K. Mwanamyoto Mpwapwa

Tarehe 09 Agosti, 2020.

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) haiko tayari kuchafuliwa na mtumishi wake yeyote anayejihusisha na vitendo vya rushwa na ubadhirifu ikizingatiwa kuwa, taasisi hiyo imejenga taswira nzuri kwa wananchi kwa kufanya kazi nzuri ya kupambana na vitendo vya rushwa na ubadhirifu wa rasilimali za umma katika kipindi cha miaka mitano ya utawala wa Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ambaye amejipambanua kwa vitendo kuichukia rushwa.

Hayo yamesemwa jana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Kapt. (Mst) Mhe. George H. Mkuchika, wakati akimkaribisha Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kuzindua Jengo la Ofisi ya TAKUKURU Wilaya ya Mpwapwa.

Mhe. Mkuchika amemhakikishia Makamu wa Rais kuwa, TAKUKURU haitamvumilia mtumishi yeyote atakayeshiriki vitendo vya rushwa na ubadhirifu ambavyo vinakwamisha huduma kwa wananchi na miradi mbalimbali ya maendeleo.

Sanjali na hilo, Mhe. Mkuchika amefarijika kuona TAKUKURU imeshawachukulia hatua watumishi wote wa taasisi hiyo waliohusika na ubadhirifu wa fedha za umma wakati wa ujenzi wa baadhi ya Ofisi za TAKUKURU Wilaya ikiwemo ya Chamwino iliyozinduliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli  tarehe 22 Julai, 2020 ambapo alibaini ubadhirifu huo baada kukagua jengo hilo na kutoridhishwa na thamani ya fedha iliyotumika.

Watumishi wote waliohusika na kubainika kujihusisha na ubadhirifu wamechukuliwa hatua stahiki za kinidhamu na kisheria na watafikishwa mahakamani hivi karibuni, Mhe. Mkuchika amemthibitishia Makamu wa Rais.

Awali, akitoa maelezo kuhusu jengo la Ofisi ya TAKUKURU Wilaya ya Mpwapwa, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Brig Jen. John Julius Mbungo, alisema aliunda tume huru ya uchunguzi iliyobaini ubadhirifu kwenye ujenzi wa Ofisi za TAKUKURU Wilaya ya Chamwino na Mpwapwa na kwenye Ofisi ya Intelijensia Dodoma ambapo tayari TAKUKURU imeshawachukulia hatua za kinidhamu na kisheria kwa waliobanika na watafikishwa mahakamani hivi karibuni.

Kufuatia hatua hiyo, Brig. Jen. Mbungo amemuomba Mhe. Samia Suluhu Hassan kumfikishia taarifa hiyo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli ikiwa ni sehemu ya mrejesho wa utekelezaji wa maelekezo aliyoyatoa pindi alipobaini ubadhilifu huo wakati akizindua Jengo la Ofisi ya TAKUKURU Wilaya ya Chamwino.

 


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akikata Utepe  kuzindua rasmi Jengo la Ofisi ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Wilaya ya Mpwapwa Mkoani Dodoma Agosti 08, 2020.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Kapt. (Mst) Geoge Mkuchika akikamribisha  Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan (hayupo pichani) kuzungumza na Wananchi wa Wilaya ya Mpwapwa wakati wa hafla ya uzinduzi wa Jengo la Ofisi ya TAKUKURU ya wilaya hiyo uliofanyika Agosti 08, 2020.        

Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Brig Jen. John Julius Mbungo akitoa maelezo kuhusu ujenzi wa jengo la Ofisi ya TAKUKURU wilaya ya Mpwapwa kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Kapt. (Mst) Mhe. Geoge Mkuchika wakati wa hafla ya uzinduzi wa Jengo la Ofisi ya TAKUKURU ya wilaya hiyo uliofanyika Agosti 08, 2020.    

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akizungumza na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Kapt. (Mst) Mhe. Geoge Mkuchika wakati wa hafla ya uzinduzi wa Jengo la Ofisi ya TAKUKURU Wilaya ya Mpwapwa Mkoani Dodoma uliofanyika Agosti 08, 2020.        

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akiondoa Kitambaa kuzindua rasmi Jengo la Ofisi ya Taasisi ya Kuzuwia na Kupambana na Rushwa TAKUKURU Wilaya ya Mpwapwa Mkoani Dodoma Agosti 08, 2020.

No comments:

Post a Comment